Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na
Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa (Mb) akizungumza na
wahitimu na wananchi waliohudhuria mahafali ya 30 ya Chuo cha
Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) yaliyofanyika katika Kampasi ya
Mtwara.
Kaimu Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma
Tanzania (TPSC), Dkt. Emmanuel Shindika akitambulisha makundi ya
wahitimu wakati wa mahafali ya 30 ya chuo hicho yaliyofanyika katika
Kampasi ya Mtwara.
Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Chuo cha Utumishi wa Umma
Tanzania (TPSC) Dkt. Charles Msonde akitoa neno la utangulizi wakati
wa mahafali ya 30 ya chuo hicho yaliyofanyika katika Kampasi ya
Mtwara.
Baadhi ya wanafunzi bora waliohitimu Chuo cha Utumishi wa Umma
Tanzania (TPSC) wakiwa mbele ya meza kuu mara baada ya
kukabidhiwa vyeti na zawadi wakati wa mahafali ya 30 ya chuo hicho
yaliyofanyika katika Kampasi ya Mtwara.
Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa (Mb) akiwa katika picha ya pamoja na menejimenti ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) na baadhi ya wahitimu wa mahafali ya 30 ya chuo hicho yaliyofanyika katika Kampasi ya Mtwara.
Baadhi ya wahitimu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) wakimsikiliza mgeni rasmi, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa (hayupo pichani) wakati wa mahafali ya 30 ya chuo hicho yaliyofanyika katika Kampasi ya Mtwara.
Wahitimu wa mahafali ya 30 wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania
(TPSC) wametakiwa kuwa waadilifu, wachapakazi na wazalendo kwa nchi
yao, watakapokuwa wanatekeleza majukumu yao kwa ajili ya maslahi ya
Taifa.
Wito huo umetolewa na Dkt. Mwanjelwa alipokuwa akiwatunuku vyeti
wahitimu hao katika mahafali yaliyofanyika Chuo cha Utumishi wa Umma
Tanzania, Kampasi ya Mtwara.
Mhe. Dkt. Mwanjelwa amesema, waajiri wote nchini wanatambua umahiri
wa utendaji kazi wa wahitimu wanaotoka Chuo cha Utumishi wa Umma,
hivyo amewataka wahitimu hao kuendelea kujenga taswira nzuri ya chuo
kwa kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na weledi.
Mhe. Dkt. Mwanjelwa ameongeza kuwa, sasa ni wakati muafaka kwa
wahitimu hao kuonyesha utofauti wao kiutendaji na wahitimu wengine
ambao hawakupata fursa ya kusoma Chuo cha Utumishi wa Umma.
Mhe. Dkt. Mwanjelwa amewahimiza wahitimu hao, kufanya kazi kwa
ufanisi na kuwa wabunifu katika utendaji kazi ili kukidhi mahitaji ya
wananchi na kuendana na kasi ya Serikali ya Awamu ya Tano
inayoongozwa na Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli ambaye anaiishi kwa
vitendo kaulimbiu yake ya HAPA KAZI TU.
Mhe. Dkt. Mwanjelwa amewakumbusha wahitimu kuchukua tahadhari dhidi
ya ugonjwa wa UKIMWI na magonjwa mengine ya kuambukizwa ambayo
yanahatarisha nguvu kazi yao kwani elimu na maarifa waliyoyapata
yatakuwa hayana maana, iwapo watashindwa kuyatumia kutokana na
matatizo ya kiafya ambayo yanaepukika.
Kutokana na umuhimu wa mafunzo yanayotolewa na chuo, Mhe. Dkt.
Mwanjelwa kwa msisitizo, ametoa rai kwa waajiri wote nchini kuendelea
kukitumia Chuo cha Utumishi wa Umma kuwajengea uwezo watumishi wa
umma ili waweze kutekeleza majukumu yao kikamilifu na hatimaye kutoa
huduma bora kwa wananchi.
Aidha, Mhe. Dkt. Mwanjelwa ametumia fursa hii, kuwaasa watumishi wa
Chuo cha Utumishi wa Umma kushirikiana na kufanya kazi kwa bidii, na
amewaonya kutojenga makundi ambayo kimsingi yatakwamisha utendaji
kazi na maendeleo ya chuo kwa ujumla.
Naye, Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Chuo cha Utumishi wa Umma
Tanzania, Dkt. Charles Msonde amesema bodi ya taaluma ilipitia kwa kina
taarifa za matokeo za wahitimu wote na kujiridhisha pasipo shaka yoyote
kuwa, wanastahili kutunikiwa vyeti.
Dkt. Msonde amesema, waajiri mbalimbali wamethibitisha kwamba,
wahitimu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania wamekuwa ni bora
kiutendaji katika maeneo yao ya kazi na kuongeza kuwa, ni lengo la chuo
kuwaandaa wanafunzi wote wanaopata mafunzo TPSC kuwa lulu katika
soko la ajira.
Awali, Kaimu Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma
Tanzania (TPSC), Dkt. Emmanuel Shindika amewataka wahitimu kuitumia
elimu waliyoipata kwa manufaa yao na taifa kwa ujumla, na
amewapongeza waelekezi katika kampasi zote kwa kuwapa mafunzo bora
wahitimu hao, ikiwa ni pamoja na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi
wa Umma na Utawala Bora kwa mchango wake katika kukiboresha chuo
hicho.
Jumla ya wahitimu 2686 walitunukiwa vyeti vya awali, astashahada,
stashahada na shahada ya uzamili katika fani za Utunzaji wa
Kumbukumbu, Uhazili, Sheria, Menejimenti ya Rasilimaliwatu, TEHAMA,
Utawala wa Umma, Manunuzi na Ugavi.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...