Mratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma wa Hospitali ya wilaya ya Tunduru Dkt Mkasange Kihongole akiongea na wazazi wa kijiji cha Mchuluka kata ya Mchuluka wakati wa zoezi la uchunguzi wa vimelea vya ugonjwa Kifua kikuu kwa watoto chini ya umri wa miaka mitano ikiwa ni kampeni ya wilaya hiyo kutokomeza ugonjwa huo.
====
Serikali wilayani Tunduru,imewaagiza viongozi wa Halmashauri ya wilaya ya Tunduru kuwafuatilia kwa karibu watumishi wake juu ya utendaji wao ili kubaini kama kweli wanawajibika katika kuwatumikia Wananchi.
Agizo hilo limetolewa mwishoni mwa wiki na Mkuu wa wilaya hiyo Juma Homera , katika kikao chake na wanawake wa kijiji cha Mchuluka waliokusanyika katika Zahanati ya kijiji hicho wakipata huduma ya Kliniki.
Pia Mkuu wa wilaya alizindua zoezi la uchunguzi wa ugonjwa wa kifua kikuu kwa watoto chini ya umri wa miaka mitano iliyoendeshwa na kitengo cha kifua kikuu Hospitali ya wilaya ya Tunduru ikiongozwa na Dkt Mkasange Kihongole.
Alisema, lengo la Serikali ni kuona watumishi wa umma wanakwenda vijijini kwa wananchi ili kusikiliza na kutatua kero zao.
Homera alisema,ni vema watumishi watumishi wa Umma kila mara kutenga muda kwa ajili ya kutembelea wananchi kwa ajili ya kutatua kero zao, badala ya kutumia muda mwingi kukaa ofisini jambo linalolalamikiwa sana na wananchi ambao bado wanakabiliwa na changamoto nyingi za maisha hususani kwenye upatikanaji wa huduma mbalimbali za kijamii.
Alisema,Serikali haitakuwa na msalie mtume kwa watumishi wazembe na wale wanaofanya kazi kwa mazoea kwani itahakikisha inachukua hatua pale wanaposhindwa kuleta ufanisi sehemu za kazi.
Homera alisema, baadhi ya watendaji wa Serikali kuanzia ngazi ya vijiji hadi wilaya wameshindwa kutumia nafasi zao ikiwemo kutatua kero za wananchi, badala yake wanasubiri hadi viongozi wa wilaya na mkoa wafike jambo ambalo limezidisha kuongezeka kwa matatizo katika jamii.
Homera,amewataka wazazi kuhakikisha wanapeka watoto wao kliniki kwa ajili ya uchunguzi Afya za watoto wao na kujiepusha tabia ya kuwapa Dawa bila kupata vipimo vya Daktari.
Alisema,Serikali ya awamu ya tano inaendelea kuboresha Sekta ya Afya kwa kujenga Zahanati,vituo vya Afya,Hospitali,vifaa Tiba na kuajiri watumishi, na hayo yanafanyika kama mpango wa kupunguza vifo vitokanavyo na ukosefu wa Huduma za Matibabu.
Mkuu wa wilaya,ameonya tabia ya wanawake wa wilaya hiyo kuzaa katika umri mdogo ili kuepuka matatizo wakati wa kujifungua ambayo imekuwa chanzo cha kuongezeka kwa vifo kwa akina mama.
Alisema, wilaya ya Tunduru imekuwa kwenye wakati mgumu hasa kwa wasichana wanaopata mimba katika umri mdogo chini ya miaka 16 kutokana na mila na Tamaduni na kupiga marufuku ngoma za usiku ambazo zinachangia sana wasichana wadogo kubakwa na kutiwa mimba.
Mratibu wa kifua kikuu na ukoma wa wilaya ya Tunduru Dkt Mkasange Kihongole alisema,Serikali kwa kushirikiana na jamii inayo wajibu wa kuzuia mambukizi ya ugonjwa wa Kifua kikuu kwa watoto chini ya umri wa miaka 5 kwa kuvuta Sigara,Tumbaku, na hata Bangi akiwa amemshika mtoto.
Alisema,ugonjwa wa Kifua kikuu licha ya kusababisha vifo lakini pindi mtoto anapougua hata mzazi anakosa muda wa kufanya kazi za kiuchumi ikiwemo kwenda shambani hivyo kuchangia umaskini katika ngazi ya familia.
Amewataka wanawake wajawazito kuwa na mazoea ya kwenda Kliniki mara kwa mara kwa ajili ya kupata ushauri wa kitaalam na kuhakikisha wanajifungulia kwenye vituo vya kutolea huduma ili kuokoa maisha yao.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...