Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga akizungumza na Gilbert Houngbo, Rais wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (International Fund for Agriculture Development – IFAD walipokutana jana Tarehe 20 Mei 2019 Jijini Dodoma. (Picha Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo)



Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Dodoma

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) jana Tarehe 20 Mei 2019 alikutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Mfuko wa Kimataifa na Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Gilbert Houngbo.

Katika mazungumzo hayo Houngbo alisema mfuko huo umetenga zaidi ya sh Billion 127.3 kwa ajili ya kufadhili miradi ya kilimo nchini kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2020.

Alimpongeza Rais Dk John Magufuli pamoja na serikali yake kwa juhudi kubwa alizozifanya katika kukuza uchumi ikiwemo utekelezaji wa miradi inayofadhiliwa na mfuko huo.

Katika mazungumzo yake na Rais Magufuli kabla ya kuzuru Jijini Dodoma Rais huyo wa IFAD alimueleza Dkt Magufuli kuwa baada ya kutenga fedha hizo mfuko huo unasubiri upande wa Tanzania kuainisha maeneo mahususi ya miradi ya kilimo ambako fedha zitaelekezwa.

Kadhalika, alieleza kuwa ana matumaini makubwa kuwa miradi hiyo itafanikiwa kwa kuzingatia Tanzania ni nchi yenye amani na namna serikali ilivyo na dhamira ya maendeleo.

Naye Waziri Hasunga alimuhakikishia kuwa fedha hizo zitakazoelekezwa katika maeneo yenye maslahi mapana ya sekta ya kilimo ikiwemo kuwezesha matumizi ya zana za kilimo katika uzalishaji, kuzalisha mbegu bora za mazao, kutatua changamoto za masoko ya mazao pamoja na kuboresha ufugaji zitakuwa chachu ya kuimarisha kilimo nchini.

Mhe Hasunga alisema kuwa tayari Bajeti ya Matumizi ya kawaida ya wizara ya Kilimo imepitishwa na wabunge hivyo kupitia Mpango wa Pili wa Taifa wa Maendeleo ya Kilimo (ASDP II) umesisitizia mapinduzi ya viwanda na umeitambua Sekta ya Kilimo kuwa muhimili imara kwa ajili ya upatikanaji wa malighafi za viwanda. 

Alisema kiasi hicho kilichotengwa na IFAD itakuwa chachu na chagizo katika kuboresha mustakabali wa kilimo. 

Alisema kupitia Miongozo hiyo ya Kitaifa, pamoja na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015 na Sera ya Kilimo ya mwaka 2013, inayotekelezwa na Wizara kupitia Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo Awamu ya Pili (ASDP II) ambayo inalenga kuleta mageuzi katika Sekta ya Kilimo na kwa kutambua umuhimu wa kuongeza mitaji, teknolojia na ubunifu, Sekta Binafsi inashirikishwa kikamilifu katika utekelezaji wa ASDP II wakulima nchini wataelimika kupitia mbinu bora za kilimo na uzalishaji wenye tija.

IFAD imekuwa katika ushirikiano na serikali ya Tanzania kufuatia uhusiano ulioanza mwaka 1978 na kudumishwa kwa maslahi ya Watanzania.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...