Na Woinde Shizza, Michuzi Tv, Arusha
MTOTO mwenye umri wa miaka miwili Mercy Nyari amefariki dunia baada ya mwili wake kuteketea kwa moto baada ya nyumba aliyokuwa akiishi kuungua.
Nyumba hiyo ya Eliud Nyari iliyoko eneo la Loita Nkwamala katika kata ya Nkwandrua wilayani Meru mkoani Arusha imeungua leo asubuhi na kusababisha kifo hicho.
Akizungumza kuhusu kuungua kwa nyumba hiyo, Mwenyekiti wa Kijiji cha Loita Dikson Kaaya amesema mtoto huyo aliachwa nyumbani mwenyewe na mama yake mzazi , kitu kilichomsababishia kifo maana alikosa msaada wakati moto huo ulivyokuwa unawaka.
"Wakati moto unawaka katika nyumba hiyo hakukuwa na mtu yeyote na mtoto alikuwa ameachwa ndani na mama yake, hivyo alikosa msaada wa mtu wa kumsaidia ndio maana umauti ulimkuta,na kwa kweli ukiangalia mwili wake umeteketea kabisa,"amesema.
Amefafanua moto huo umewaka leo asubuhi pasipo kujulikana chanzo kutokana na nyumba hiyo kutokuwa na umeme au kitu chochote kinachohusisha hatari ya kuwepo kwa moto hali iliyoleta taharuki kwa familia.
Mmoja wa majirani wa nyumba hiyo Mchungaji Tegemea Mbise amesema wao walishangaa kuona moto huo umeanza kuwaka gafla. Pia amesema kinachowashangaza zaidi nyumba hiyo iliyoungua haina umeme, hivyo ni jambo linalotia hofu zaidi.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Jerry Muro akiambatana na baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na usalama walifika eneo la tukio na kukuta tayari moto huo umeshateketeza nyumba hiyo na kuanguka chini huku mali zote zikiwa zimeteketea na kusababisha familia ya watu saba kukosa makazi .
Muro mbali na kutoa pole amesema Serikali ya Wilaya kwa kushirikiana na wadau wamejitolea kuijenga nyumba nyingine ndogo kwa ajili ya familia hiyo na kutoa chakuka cha kuwasaidia kwa muda wa wiki moja.
Pia Muro amewataka wananchi kutowaacha watoto na watu wasiojiweza majumbani pasipo kuwa na watu wa kuwasaidia ili kuepeshua madhara yanayoweza kujitokeza.
Hata hivyo kutokana na mwili huo kuharibiwa , familia ya mtoto huyo pamoja na Serikali wameamua kuuzika mwili huo na kisha kuacha hatua za uchunguzi ziendelee.
Baadhi ya wananchi waliojitokeza kuangalia tukio hilo la moto lilillosababisha kifo cha mtoto mmoja
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...