Na Ramadhani Ali – Maelezo Zanzibar
Hali ya kiuchumi inayowakabili wagonjwa wengi wa maradhi yasiyoambukiza Zanzibar imetajwa kuwa ni changamoto kubwa katika kupata chakula sahihi cha kupunguza makali ya maradhi hayo.

Akitoa matokeo ya utafiti uliofanywa na Kitengo cha maradhi yasiyoambukiza katika mkutano wa wadau wa maradhi hayo, Mratibu wa Kitengo hicho Omar Mwalimu alisema wagonjwa wa maradhi hayo wanatakiwa kula zaidi matunda na mboga mboga na kupunguza kutumia mafuta na vyakula vya uwanga.

Alisema katika utafiti huo wamegundua kuwa wananchi wengi wanaelewa juu ya maradhi hayo na njia za kukabiliana nayo kupitia vyombo vya habari na mikutano mbali mbali lakini hali ya kiuchumi ni kikwazo kwao.

Alieleza kuwa tabia ya wananchi kuchelewa kufanya uchunguzi wa afya zao mpaka wapate mabadiliko makubwa ya mwili ni moja ya tatizo linalowakabili wagonjwa wa maradhi yasiyoambukiza nchini.

Omar Mwalimu alisema upatikanaji wa huduma za matibabu ya maradhi yasiyoambukiza katika baadhi ya vituo vya shamba bado hairidhishi na wagonjwa huvunjika moya na kwenda katika vituo hivyo na huamua kubaki nyumbani ama kufuata huduma hizo Hospitali Kuu ya Mnazimmoja.

Aliongeza kuwa tatizo kubwa lipo kwa wagonjwa wenye tatizo la maradhi ya Saratani kwa vile upatikanaji wa dawa za kutibu maradhi hayo ni ghali na wagonjwa wengi hawana uwezo wa kuzinunua.

Hata hivyo Omar Mwalimu aliwashauri wagonjwa wa maradhi yasiyoambukiza kutafuta ushauri wa madaktari waliosomea kabla ya kutumia dawa mbadala ama kufuata tiba ya mitandao.

Alisema hivi sasa wamejitokeza wajanja wengi mitaani na kwenye mitandao ya kijamii wanaotoa matibabu ya maradhi yasiyoambukiza lakini hawana tiba sahihi ya maradhi hayo.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya maradhi yasiyoambukiza Zanzibar Dk. Said Gharib Bilal alisema maradhi hayo yapo na yamekuwa ni sehemu ya maisha ya wananchi wengi, jambo la msingi ni kuwa na elimu ya kujua namna ya kuishi nayo.

Baadhi ya waathirika wa maradhi yasiyoambukiza walioshiriki mkutano huo uliofanyika Kitengo Shirikishi cha afya ya mama na mtoti Kidongochekundu walisema mara nyingi wanapokwenda kutafuta dawa kwenye vituo vya afya vya karibu vijiji, hawapati dawa ama hupata nusu ya kiwango kinachohitajika.
 Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maradhi yasiyoambukiza Zanzibar (ZNCDA) Said Gharib Bilali akizungumza katika Mkutano wa wadau wa kujadili upatikanaji huduma bora za afya kwa wagonjwa wa maradhi hayo Zanzibar.
 Mkuu wa Kitengo cha Maradhi yasiyoambukiza Zanzibar Omar Mwalim akiwasilisha taarifa ya utafiti wa maradhi yasiyoambukiza katika Mkutano wa wadau uliofanyika Kitengo Shirikishi cha mama na mtoto Kidongochekundu.
 Baadhi ya wajumbe wa Mkutano wa kujadili upatikanaji huduma bora za afya kwa wagonjwa wa maradhi yasiyoambukiza wakifuatilia taarifa ya utafiti uliofanywa kuhusu maradhi hayo.
Mshiriki Amour Kassim kutoka Jumuiya ya ZAMWASO akitoa mchango katika mkutano huo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...