Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joachim Wangabo amewaasa wafanyakazi mkoani
Rukwa kupunguza matumizi ya simu za mikononi kwaajili ya shughuli
binafsi nje na majukumu ya kazi hasa muda wa kazi wanapokuwa ofisini
wakiendelea kutekeleza majukumu yao ya kila siku.
Amesema kuwa dhamira ya serikali ya awamu ya tano ni kumtumikia
mwananchi kwa nguvu zote hivyo kila mfanyakazi anapaswa kuongeza bidii
katika kufanya kazi, lakini kutumia simu na kuacha kuwahudumia
wananchi kwa wakati mfanyakazi anakuwa anapata mshahara ambao
hausmtahili kutokana na kutotumia muda wake alioajiriwa kwa ufanisi.
“ Ndugu wafanyakazi, hizi simu zimekuwa ni changamoto kubwa sana
sehemu zetu za kazi, unakuta mtu badala ya kufanya kazi, hata kutoa
huduma kwa mwananchi yeye “ana-chat” kwenye simu, vidole viko kwenye
simu, yeye na simu, simu na yeye, kazi haziendi na kama zinakwenda
basi zinakwenda kwa mapungufu, kunakuwa hakuna ufanisi na umakini,
suala hili la simu tuliangalie sana ndugu waajiri pamoja na
waajiriwa,” alisisitiza
Ameongeza kuwa wafanyakazi wamekuwa wakidai maslahi kuliko kupima
uwajibikaji wao katika kazi ambazo wanapaswa kuzitekeleza na hali
inayopelekea kuzorota kwa kazi nyingi kutokana na wafanyakazi
kujishughulisha na matumizi ya simu za mkononi kuliko kuwajibika.
Ameyasema hayo katika maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani
ambayo kimkoa katika mkoa wa Rukwa yalifanyika katika viwanja vya
mpira mji mdogo wa Laela, Wilaya ya Sumbawanga alipokuwa akitoa
ufafanuzi wa maeneo nane yenye kulenga kuimarisha utendaji wa kazi ili
kuleta maslahi kwa wananchi pamoja na wafanyakazi katika maeneo yao ya
kazi, ikiwemo uwajibikaji, kushughulikia kero za wananchi, uadilifu,
usimamizi wa miradi, ubunifu, ushirikiano,kupambana na Rushwa,na
kuunda mabaraza ya kazi.
Wakati akisoma risala ya wafanyakazi kwa mgeni rasmi katibu wa
shirikisho la vyama huru vya wafanayakazi (TUCTA) Mkoani Rukwa Nashoni
Kabombwe alisema kuwa kuna baadhi ya waajiri hawataki kabisa zoezi la
kupata wafanyakazi bora kwenye taasisi zao lifanyike kwa kisingizio
kwamba hawana fedha wala zawadi yoyote ya kuwalipa.
Katika kushinikiza hilo alisema, “kiwango cha zawadi kwa wafanyakazi
bora zinazotolewa na baadhi ya waajiri ni kidogo na hakiendani na
mabadiliko ya kiuchumi TUCTA inawataka waajiri kuanzia sasa kiwango
cha chini cha zawadi kiwe shilingi 500,000 au kitu chenye thamani
isiyopungua fedha hiyo.”
Kwa upande wake Afisa mfawidhi wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA)
katika mikoa ya Rukwa na Katavi Oscar Ngaluka katika mwaka wa fedha
2017/2018 Tume ilipokea jumla ya migogoro ya kikazi 127, wakati
iliyomalizwa katika hatua ya usuluhishi ni 93, na inayoendelea na
migogoro ni 10 na kuongeza kuwa sekta inayoongoza kwa migogoro mahala
pa kazi katika mikoa ya Rukwa na Katavi ni ujenzi wa barabara.
“Sababu zinazoweza kumfanya mfanyakazi afungue mgogoro wake katika
Tume ni pamoja na kuachishwa kazi bila ya kuwepo sababu ya kufaa na
utaratibu wala kosa, mwajiri kuzuia vyama vya wafanyakazi kutekeleza
majukumu yao ya kichama, madai ya stahili mbalimbali na manyanyazo
sehemu za kazi,” Alisema.
Kauli mbiu ya siku ya wafanyakazi ni “Tanzania ya Uchumi inawezekana,
wakati wa mishahara na maslahi bora kwa wafanyakazi ni sasa” ambapo
Tanzania nzima ina vyama vya wafanyakazi 31 huku Mkoa wa Rukwa ukiwa
na vyama vya wafanyakazi 9.
Baadhi ya watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo wakipita na bango lao katika maadhimisho ya sherehe ya siku ya Wafanyakazi bora iliyofanyika katika viwanja vya mpira mji mdogo laela Wilayani Sumbawaga.
Mkuu wa mkoa wa Rukwa Joachim Wangabo akimkabidhi Michale Mongomongo dereva wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa cheti pamoja na shilingi laki tatu ikiwa ni zawadi ya mfanyakazi bora katika sherehe za siku ya wafanyakazi 2019 Mkoani Rukwa.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joachim Wangabo (waliokaa mwenye skafu) katika picha ya pamoja na baadhi ya wafanyakazi bora (waliosimama) katika sherehe ya siku ya Wafanyakazi bora iliyofanyika katika viwanja vya mpira mji mdogo laela Wilayani Sumbawaga.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...