Muendelezo wa Kazi za ujenzi wa Mtaro Mkuu wa kupitishia Maji ya Mvua kuunganisha kipande kilichobakia cha Mita kati ya Mia 700 hadi Mia 750 kilichopo baina ya Mikunguni na Sebleni unatarajiwa kuendelea tena kuanzia Tarehe 20 mwezi huu.

Kazi hiyo inayotazamiwa kufanywa ndani ya kipindi cha Miezi Mitatu ilisita kwa muda kutokana na utepetepe wa ardhi uliosababishwa na Mvua kubwa za Masika zilizopita na kupelekea kifaa cha kuchimbia kupata changamoto ya kufanyakazi ipasavyo.

Akitoa ufafanuzi wa Ujenzi wa Mtaro huo mbele ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi hapo Mikunguni, Meneja wa Mradi wa Huduma za Jamii Mijini { ZUSP} Nd. Makame Ali alisema tatizo la kutuama kwa Maji ya Mvua katika meneo ya Mji wa Zanzibar linatarajiwa kuondoka baada ya kukamilika kwa Mradi huo.

Balozi Seif alifanya ziara hiyo maalum kuangalia athari zinazotokana na Ujenzi wa Miundombinu hiyo ya Mtaro kufuatia malalamiko kadhaa aliyokuwa yakitolewa na Wananchi hasa mawasiliano ya bara bara yasiyo rafiki kwa wasafiri wa vyombo tofauti vya moto katika kipindi hichi.

Nd. Makame alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba kuunganishwa kwa kipande hicho cha Mita Mia 700 kutaonyesha matumaini ya kumalizika kwa Mtaro huo unaotokea Bwawa la Mwanakwerekwe, kupita Bwawa la kwa Mtumwa Jeni, kuelekea Bwawa la Sebleni kupitia Mikunguni na hatimae maji ya Mtaro huo kumalizia Bahari ya Kinazini.

Alisema kutokana na uchimbaji wa Mtaro huo kwenda chini umbali mkubwa zaidi ya Mita Nane Wahandisi wa Ujenzi wako wanalazimika kuwa makini katika kuchukuwa tahadhari ya Usalama wa Watu ambao ni jambo la msingi.

Akizungumzia Bara bara za Lami zilizopitishwa Mtaro huo Nd. Makame alisema Wahandisi wa Mradi huo kwa mujibu wa Mkataba wana jukumu la kujenga upya bara bara hizo ili kurejesha uhalisia uliokuwepo wa Miundombinu hiyo ya Mawasiliano.

Alisema changamoto inayokwaza kazi hiyo kwa hatua ya Awamu ya kwanza ya ujenzi wa Bara bara kwenye maeneo yaliyopita Mtaro yaliyokamilika ni uhaba wa kifusi cha kuweka sawa maeneo yaliyoathirika.

Alieleza kwamba juhudi za kuomba kifusi katika Taasisi zinazohusika zimeshachukuliwa na hadi sasa kilichopatikana kimefikia Cubic Mita Mia 150 wakati mahitaji halisi ya kufanikisha kazi hizo kipatikane Kifusi chenye ujazo wa Cubic Mita Elfu 14,000.

Kuhusu mtaro wa zamani wa maji ya mvua uliokuwa ukitumika kutoa maji katika Bwawa la Sebleni Meneja wa Mradi wa Huduma za Jamii Mijini { ZUSP} Nd. Makame Ali alisema jitihada zitafanywa katika kuufanyia marekebisho madogo Mtaro huo ili uendelee kutoa huduma kama kawaida.

Nd. Makame alisema marekebisho hayo yatawezesha maji yote ya Mvua yanayotiririka kutoka maeneo mbali mbali ya Mitaa ya Ng’ambo yaliyojirani na Mtaro huo maji yake yatiririke na kuingia Mtaro Mkuu katika eneo la Kwa Abass Hussein.

Akiridhika na kazi kubwa ya mafanikio iliyofanywa na Wahandisi wa Ujenzi wa Mtaro huo Mkuu wa Maji ya Mvua, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema ni vyema kwa Wataalamu wa Ujenzi kuwa na utaratibu wa kuwaeleza Wananchi hatua wanayofikia katika Miradi wayayoitekeleza.

Balozi Seif alisema utaratibu huo utasaidia kuondosha malalamiko yanayotolewa na Wananchi hasa pale wakati wa ujenzi wa Miundombinu unaposita na kuleta usumbufu kwao bila ya kupatiwa Taarifa yoyote.

Akitoa shukrani kwa niaba ya Wananchi wa Maeneo yaliyopita Mtaro huo Mkuu wa Maji ya Mvua, Mkuu wa Mkoa Mjini Magharibi Mh. Ayoub Mohamed Mahmoud alisema Serikali ya Mkoa itaendelea kuwaelimisha Wananchi kujenga Utamaduni wa kufuata utaratibu wa hifadhi ya Taka taka Mitaani.

Mh. Ayoub alisema kuachiliwa kuzagaa ovyo kwa taka taka mbali ya kutishia afya za Wakaazi wake lakini pia kunaweza kusababisha uharibifu wa Miundombinu iliyojengwa na Serikali kwa gharama kubwa ili iwahudumie Wananchi wake.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar katika ziara hiyo alipata wasaa wa kuangalia eneo la Mtaro hapo Mikunguni ambalo haliko rafiki kwa Waendesha vyombo vya moto kipindi hichi, kuangalia Mtaro hapo Kwa Abass Hussein na kutumia muda wa kuukagua hadi ulikoishia katika eneo la Kinazini.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi pamoja na Mkuu wa Moa Mjini Magharibi Mh. Ayoub Mohamed Mahmoud wakikagua Mtaro Mkuu wa Maji ya Mvua katika eneo la Kwa Abass Hussein hadi Kinazini.
 Muonekano wa Barabara ya Mikunguni iliyofumuliwa kwa kupitisha Ujenzi wa Mtaro Mkuu wa Maji ya Mvua unaoelekea Kwa Abass Hussein na kuishia Kinazini.
 Mhandisi Mshauri wa Ujenzi wa Madaraja Mhandisi John Nyaroko akimfahamisha Balozi Seif hatua zinakazochukuliwa za kutia zege kwenye Daraja la Kinazini kunusuri kasi ya Maji ya Mavua yatakayokuwa yakipita kwenye Mtaro Mkuu. Picha na – OMPR – ZNZ.
 Balozi Seif akiwaagiza Waandisi wa Miradi ya Ujenzi Nchini kutoa Taarifa kwa Wananchi hatua za utekelezaji wa Miradi yao kila wakati hasa pale inapotokezea hitilafu ya kukwama kwa Miradi hiyo.
 Meneja wa Mradi wa Huduma za Jamii Mijini { ZUSP} Nd. Makame Ali akimueleza Balozi Seif hatua zitakazochukuliwa kumaliza Mtaro Mkuu wa Maji ya Mvua hapo Mikunguni kipande kidogo kilichobakia.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...