Na Mathew Kwembe, Mtwara
Michuano ya UMISSETA inayoendelea mjini Mtwara imefikia hatua ya nusu fainali kwa upande wa soka wavulana ambapo katika michezo iliyomalizika leo jioni, timu za soka wavulana kutoka mikoa ya Lindi, Ruvuma, Mwanza na Songwe zimefanikiwa kuingia hatua ya nusu fainali baada ya kuwalaza wapinzani wao akiwemo bingwa mtetezi Tanga ambayo ilitolewa na Lindi.
Kwa matokeo hayo timu ya soka wavulana kutoka mkoa wa Lindi itakutana na Ruvuma kwenye nusu fainali ya kwanza inayotarajiwa kucheza kesho saa nane mchana na kufuatiwa na nusu fainali ya pili itakayowakutanisha vigogo Mwanza watakaochuana na timu ngumu ya Songwe.
Timu ya kwanza kuingia hatua ya nusu fainali ilikuwa ni timu machachari ya kutoka  mkoa wa Lindi ambayo iliitoa timu ya mkoa wa Tanga kwa penati 3 kwa 1 baada ya kutoka suluhu ya bila kufungana baada ya dakika tisini za mchezo.
Pambano lingine la robo fainali lilizihusisha timu za kutoka mikoa Ruvuma na Kilimanjaro ambapo timu ya soka ya mkoa wa Ruvuma ambayo inaundwa na wachezaji 8 kutoka kwenye kituo cha michezo cha shule ya sekondari Ruhuwiko iliyopo nje kidogo ya Manispaa ya songea iliwafunga timu ya Kilimanjaro kwa magoli mawili kwa bila.
Katika mechi zilizomalizika jioni hii timu za Songwe na Manyara na Mbeya na Mwanza zilimenyana vikali katika michezo mingine ya robo fainali ambapo Songwe waliwalaza Manyara kwa goli moja kwa sifuri na Mwanza waliifunga Mbeya kwa magoli ya penati 5 kwa 3 ya Mbeya baada ya timu hizo kutoka suluhu ya bila kufungana ndani ya dakika 90 za mchezo.
Hata hivyo Mwanza walikuwa na kila sababu ya kushinda mchezo huo kwani kwenye dakika ya 72 walikosa goli la wazi baada ya penati yao kupanguliwa na golikipa wa Mbeya Gerald Hatson na kuokolewa na mabeki wa timu hiyo.
Mara baada ya mchezo huo, Kocha wa Mwanza Mwalimu Tito Mkami amesema kuwa vijana wake walipambana kufa na kupona lakini akawasifu timu ya Mbeya kwa namna ilivyowasumbua na akakiri kuwa  timu hiyo ngumu kwani iliwapa wakati mgumu wachezaji wake wakati wote wa mchezo.
Aidha Mwalimu Mkami alitoa wito kwa Chama cha soka nchini TFF kutoshirikisha mashindano mengine pindi michuano inayoandaliwa na serikali ya UMISSETA na UMITASHUMTA inapofanyika ili kutosababisha michuano hii kukosa wachezaji muhimu kwa timu zao
Naye nahodha wa timu ya soka ya Mwanza Kimwaga Kalunga ambaye ni Mwanafunzi pekee anayechezea timu hiyo kutoka shule maalum ya soka ya Alliance ambaye alisema kuwa hawaihofii timu ya Songwe bali wanaiheshimu kwani timu zote zilizoingia hatua hiyo ni ngumu.
Mapema kesho asubuhi michezo ya nusu fainali kwa upande wa soka wasichana itachezwa katika viwanja vya chuo cha ualimu Mtwara ambapo mchezo wa kwanza utawakutanisha wababe Dar es salaam watakaotoana jasho na timu kutoka mkoa wa Iringa, na mchezo mwingine utawakutanisha miamba Mwanza watakaochuana na Ruvuma.
Kwa upande wa mpira wa mikono matokeo ya robo fainali ya mchezo huo iliyochezwa leo jioni inaonyesha kuwa timu za Geita  na Unguja wavulana zimefanikiwa kutinga hatua ya nusu fainali na zimepangwa kucheza kesho, huku nusu fainali nyingine itawakutanisha Tanga na Morogoro.
Katika mpira wa mikono wasichana, timu zilizofuzu ni Unguja ambao watakuna kesho na Morogoro na Songwe watakaocheza na Mbeya.
Mchezo mwingine ambazo timu zilizofuzu zimejulikana ni netiboli ambapo timu za Morogoro, Tanga, Dar es salaam na Mwanza zimefuzu hatua hiyo ambapo michezo hiyo itachezwa kesho kwa Tanga kukutana na Mwanza na Morogoro kucheza na Dar es salaam.
Katika mchezo wa kikapu kwa upande wa wavulana timu zilizofuzu hatua ya nusu fainali ni Pwani, Unguja, Tanga na Shinyanga ambapo kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa Pwani itacheza na Unguja na Tanga itachuana na Shinyanga.
Kwa upande wa  mpira wa kikapu wasichana Kilimanjaro itamenyana na Mwanza na Morogoro watacheza na jirani zao Dar es salaam.

Baadhi ya watazamaji wakifuatilia mojawapo ya mechi za robo fainali zilizofanyika leo mjini Mtwara
 Mchezaji wa mpira wa volleyball kutoka Tabora Charles Idrisa akipiga smash kuelekea upande wa timu ya mkoa wa Mbeya kwenye mchezo wa nusu fainali ambapo Tabora waliifunga Mbeya kwa seti 2 kwa 1
 Beki wa kulia wa timu ya soka ya Mbeya Idrisa Hamidu akiondoa mojawapo ya hatari iliyoelekezwa kwenye eneo la lango la timu yake kutoka kwa washambuliaji hatari wa mkoa wa Mwanza wakati wa pambano la robo fainali baina ya timu hizo mbili.
 Makamu mwenyekiti wa FEASA bwana Kariuki Gikonyo ambaye alikuwa mgeni rasmi wa pambano la robo fainali kati ya Mbeya na Mwanza akiwa sambamba na Mwenyekiti wa mashindano ya UMISSETA  Bwana Aaron Sokoni (mwenye kofia) wakiangalia mechi hiyo jana iliyofanyika kwenye uwanja wa chuo cha ualimu Mtwara.
Wachezaji wa timu za mkoa wa Morogoro wakichuana vikali na wenzao wa shinyanga kwenye mchezo wa kikapu wavulana hatua ya robo fainali ambapo shinyanga walishinda pambano hilo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...