Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imeendesha warsha maalum kwa wadau kutoka sekta mbalimbali kisiwani Pemba kuhusu huduma za hali ya hewa katika bahari ya Hindi ili kuboresha uelewa wa matumizi sahihi ya taarifa zitolewazo na TMA.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo, mgeni rasmi Mhe. Hemed Suleiman Abdala ambaye pia ni mkuu wa mkoa Pemba Kusini aliwataka washiriki kutambua lengo la semina ni pamoja na kupata uelewa wa matumizi sahihi ya utabiri wa hali ya hewa na tahadhari za kila siku zinazotolewa na TMA ili kukidhi malengo ya huduma hizo nchini.
Katika hotuba yake mgeni rasmi alisisitiza kwa kutambua mchango mkubwa toka TMA katika kuboresha uelewa wa wadau toka katika sekta mbalimbali hapa nchini juu ya matumizi sahihi ya taarifa za hali ya hewa na kufurahishwa na hatua ya kufika kisiwani Pemba.
“Napenda kuishukuru na kuipongeza TMA kwa kuandaa na kufanikisha warsha hii muhimu kufanyika kisiwani Pemba kwani itasaidia kutuepusha na maafa hususani wavuvi, hasa wale wachache wanaofanya shughuli zao kwa mazoea na kupelekea kukumbwa na maafa” alisema mkuu wa mkoa wa Pemba.
Aidha alimalizia kwa kuwataka washiriki wawe mabalozi wazuri katika maeneo yao ya kazi kwa kutoa elimu hiyo muhimu ambayo itasaidia kujiepusha na maafa yanayoweza kujitokeza.
Washiriki
wa warsha ya wadau wa huduma za hali ya hewa majini kwenye picha ya
pamoja na mgeni rasmi Mhe. Hemed Suleiman Abdala (mwenye suti nyeusi)
ambaye pia ni mkuu wa mkoa Pemba Kusini, iliyofanyika Tarehe 21-22 Juni,
2019
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...