Na Karama Kenyunko, Michuzi TV
BODI ya Taifa ya Parole imeiomba Serikali kuiongezea fedha za uendeshaji wa shughuli zake, ili waweze kukidhi mahitaji ya utendaji wa kazi wa mikoa na Taifa kwa sababu fedha zinazotengwa na bajeti hazitoshelezi katika utendaji wa kazi zao.
Aidha, imeshauri Waziri wa Mambo ya Ndani, kuyafanyia kazi majalada yanayowasilishwa na bodi hiyo kutoka magereza mbalimbali kwani bila kufanya hivyo baadhi ya wafungwa wanaotakiwa kunufaika kumaliza vifungo wakiwa ndani.
Mwenyekiti wa bodi ya Parole, Augustine Mrema ambae amemaliza muda wake leo Julai 16,2019, ameyasema hayo nyumbani kwake Salasala Jijini Dar es Salaam, wakati akisoma taarifa ya utekelezaji wa sheria ya bodi za parole kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia Julai, 2016 hadi Julai 15,2019
Amesema, bajeti finyu imepelekea ukosefu wa vitendea kazi vya kuweza kuwafikisha maeneo mbali mbali hasa katika magereza ili kuzungumza na wafungwa.
" Bodi ya Parole inaomba pikipiki 30 ambazo zitagawiwa kwa Mikoa yote Tanzania bara ili maafisa wa Parole waweze kutekeleza majukumu yao vizuri," amesema
Pia wameiomba vyama visivyo vya kiserikali, taasisi mbali mbali na watu wenye mapenzi mema kushiriki kikamilifu katika zoezi la kuwarekebisha wafungwa na kusaidia bodi za parole ili wafungwa wanapoachiwa huru na kurudi kwenye familia zao wawe wamerekebeshika.
Amesema, bodi hiyo imefanikiwa kwa kiasi kikubwa katika kutekeleza majukumu yake katika kipindi chote hicho cha miaka mitatu lichabya changamoto kadhaa zilizojitokeza ambazo ziko nje ya uwezo wa bodi hiyo.
Aidha, Mrema amemshukuru Rais wa Tanzania, John Magufuli kwa kumpa nafasi hiyo, akisema katika miaka mitatu wafungwa 742 kati yao 720 walipendekezwa na 648 waliachiliwa kwa msamaha wa Parole.
Amesema, wafungwa wote walioachiliwa kwa mpango wa Parole hakuna hata mmoja aliyevunja masharti na kurudishwa gerezani, kujihusisha au kuhusishwa na vitendo vya uhalifu.
Akijibu swali iwapo atateuliwa tena na Rais kwa nafasi hiyo atakubali, amesema "yeye ni nani mpaka amkatalie Rais" amesema Mrema
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...