Uingereza imeihakikishia Tanzania kuwa itaendelea kuwa mshirika wake katika masuala mbalimbali ya ubia wa maendeleo ikiwa ni pamoja na kuhamasisha wawekezaji wengi kutoka Uingereza kuwekeza Tanzania kama moja ya hatua za kuiunga mkono Serikali ya Awamu ya Tano ili iweze kufikia azma yake ya kuwa nchi ya uchumi wa kati na viwanda ifikapo 2025.

Waziri wa Masuala ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Uingereza katika Idara ya Ushirikiano wa Maendeleo, Mhe. Harriett Baldwin ameyasema hayo wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi, Jijini London, Uingereza kwa nia ya kujadili masuala mbalimbali ya maendeleo na ushirikiano baina ya Tanzania na Uingereza.

Katika mazungumzo hayo Waziri Harriett na Prof. Kabudi wamezungumzia kuhusu hali ya ushirikiano wa ubia wa maendeleo uliopo hivi sasa na kuonesha kuridhishwa na Serikali ya Tanzania inavyosimamia utekelezaji wa miradi mbalimbali inayofadhiliwa na Serikali ya Uingereza katika sekta za elimu,afya, maji, kilimo pamoja na miundombinu ya barabara hususani vijijini ikiwemo maboresho ya mifumo ya fedha,utumishi wa umma, serikali za mitaa miongoni mwa miradi mingine mingi.

Pia, Waziri Harriett ameipongeza Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli katika kupambana na rushwa,kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma katika sekta ya umma, kuongeza uwajibikaji na utawala bora mambo aliyoyataja kama hatua muhimu ya kufikia malengo ya haraka na kuondoa umasikini.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof Palamagamba John  Kabudi ameishukuru Serikali ya Uingereza kwa kuwa mbia mkubwa wa maendeleo na kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza kwa uwekezaji,biashara na utalii nchini Tanzania.

Aidha, Prof Kabudi amemhakikishia Waziri Harriett nia thabiti ya Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ya kufanya mageuzi muhimu ya kiuchumi na kiutawala yanayolenga kuifikisha Tanzania katika mojawapo ya nchi za uchumi wa kati.

Miongoni mwa maboresho hayo, Waziri Kabudi ameyataja kuwa ni pamoja na kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji na biashara,maboresho katika usimamizi wa utendaji wa Serikali katika kuwahudumia wananchi na utoaji huduma za kijamii hususani sekta zinazowagusa wananchi wengi hususani wa kipato cha chini.

Akihitimisha mazungumzo hayo Waziri wa masuala ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Uingereza, Mhe. Harriett Baldwin amemhakikishia Waziri Kabudi kuwa Uingereza inafuatilia kwa ukaribu mageuzi na maboresho ya kiutendaji yanayofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli yakiwemo, kuimarisha mazingira ya uwekezaji na biashara,kukuza demokrasia na utawala bora na hivyo Tanzania itegemee ongezeko la wawekezaji kutoka Uingereza.
 
  Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi akiwa katika mazungumzo na Waziri wa Masuala ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje wa Uingereza, Mhe. Harriett Baldwin,London Uingereza.
 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi akiwa katika picha ya pamoja na Waziri wa Masuala ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje wa Uingereza, Mhe. Harriett Baldwin mara baada ya kumaliza kufanya mazungumzo baina yao kuhusu masuala mbalimbali kati ya Tanzania na Uingereza. Mazungumzo hayo yamefanyika London Uingereza.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi akiwa katika picha ya pamoja na Waziri wa Masuala ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje wa Uingereza, Mhe. Harriett Baldwin mara baada ya kumaliza kufanya mazungumzo baina yao kuhusu masuala mbalimbali kati ya Tanzania na Uingereza. Mazungumzo hayo yamefanyika London Uingereza. Pembeni kushoto ni Balozi wa Tanzania Nchini Uingereza Dr. Asha -Rose Migizro. July 12, 2019.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...