WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemuagiza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Hamisi Issah awasake na kuwatia mbaroni watu waliohusika na wizi wa tani tano za nondo na kisha wakatoroka.

Alitoa agizo hilo jana jioni, (Alhamisi, Julai 18, 2019) wakati akizungumza na wafanyakazi na wananchi mara baada ya kukagua mradi wa ujenzi wa stendi ya mabasi ya kimataifa ya Moshi, katika kata ya Ngangamfumuni, Manispaa ya Moshi, mkoani Kilimanjaro.

Waziri Mkuu ambaye yuko mkoani Kilimanjaro kwa ziara ya kikazi za siku nne, alisema mradi huo ni maalum kwani uko miongoni mwa miradi ambayo Serikali imekuwa ikiweka utaratibu wa kupelekea fedha kwenye miradi iliyotengwa na Halmashauri.

“Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 9 za kuanzia mradi huu lakini inasikitisha kuona kwamba wanaMoshi mnahujumu kwa kuiba vifaa vya ujenzi. Ninazo taaarifa kuwa hapa zimeibiwa tani tano za nondo na zimeshakamatwa.”

“Ni aibu, ni aibu kwa wana-Moshi. Ninyi wenyewe mnauhujumu huu mradi. Manispaa iweke utaratibu wa ulinzi ili vifaa vingine visipotee zaidi. Mkuu wa Wilaya chukua hatua ya kuwafuatilia wote waliohusika,” alisema.

Kupitia maswali aliyouliza, Waziri Mkuu alibaini kuwa walinzi wawili waliokuwepo siku ya tukio walitoroka ndipo akaamua kumwagiza Kamanda wa Polisi Mkoa, awasake na kuhakikisha wanakamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.

Ujenzi wa stendi hiyo kubwa unafanywa na mkandarasi mkuu ambayo ni kampuni ya CRJE ya China akishirikiana na wakandarasi wasaidizi watano na unatarajiwa kukamilika Januari 2021. Hadi kukamilika, ujenzi huo unatarajiwa kugharimu sh. bilioni 28.8.

Ikikamilika, stendi hiyo ambayo itakuwa na ofisi, maduka, migahawa na hoteli, itakuwa na uwezo wa kuhudumia mabasi 300 kwa siku ambayo yataingia na kutoka. Kati ya hayo, mabasi 72 yanaweza kuegeshwa kwa wakati mmoja. Pia kutakuwa na maegesho ya ya magari binafsi 218, teksi 34 na bajaji na bodaboda 20.

Wakati huohuo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Hamisi Issah amethibitisha kukamatwa kwa watu watano ambao wanatuhumiwa kuhusika na wizi wa tani tano za nondo katika eneo la ujenzi wa stendi hiyo lililopo Ngangamfumuni.

“Hawa watu tumewakamata jana jioni, na kati ya walinzi waliotoroka, tumemkamata mmoja wao tayari akiwemo mkazi wa Rau, Daudi Audifasi mwenye miaka 48 ambaye anadaiwa kutoboa ukuta wa uzio kwa chini, na kukutwa na nondo nyumbani kwake ambako ni mita 10 kutoka eneo la tukio.”

Amesema tukio hilo, lilitokea Julai 6, mwaka huu majira ya saa 2 asubuhi ambapo walinzi wa eneo hilo ambao ni Maxshield company walitoroka baada ya tukio hilo. Kamanda Issah alithibitisha kwamba nondo hizo zimekamatwa na ziko polisi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...