* Yaelezwa kuwa  asilimia 90 ya viwanda vinategemea huduma ya maji kutoka bonde la Wami/Ruvu

Na Leandra Gabriel, Michuzi TV
LEO Septemba 10, jukwaa  maalumu la wadau wanaotumia maji katika bonde la Wami/Ruvu limezinduliwa rasmi na hiyo ni pamoja na kujadili hali ya maji katika bonde hilo pamoja na kujadili changamoto na utatuzi wake ili kuendelea kutunza hazina hiyo ya maji kwa kizazi cha sasa na baadaye.

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo leo jijini Dar es Salaam Kaimu Mkurugenzi wa Rasilimali za maji kutoka Wizara ya maji Rosemary Rwebugisa  amesema kuwa jukwaa hilo limewahusisha wataalamu kutoka sekta mbalimbali na wananchi ambao ndio walengwa wakubwa wa rasilimali hiyo, na kueleza kuwa ili malengo yaweze kufikiwa lazima wataalamu na wananchi washirikiane ili kuweza kuleta maendeleo endelevu hasa ya kiviwanda kupitia rasilimali ya maji.

Amesema kuwa Wizara itaendelea kushirikiana na sekta na wadau mbalimbali katika kuhakikisha vyanzo vya maji vinatunzwa na kuhifadhiwa na hiyo ni pamoja na mamlaka husika kusimamia matumizi ya maji kulingana na uwepo wake pamoja na kutatua migogoro inayohusu  rasilimali ya hiyo.

Mwenyekiti wa bonde la Wami/Ruvu Hamza Sadick amesema kuwa bonde hilo la Pwani ambalo ni moja kati ya mabonde tisa yanayopatikana Tanzania bara ni muhimu sana katika kukuza na kuendeleza viwanda na hiyo ni kutokana na maeneo mengi kutegemea maji kutoka bonde hilo na hiyo ni pamoja na jiji la Dar es Salaam, Dodoma na miji ya Kibaha na Bagamoyo ambayo imesheheni viwanda ambavyo hutegemea rasilimali maji katika kujiendesha.

Hamza amesema kuwa wataendelea kuimarisha usimamizi madhubuti wa maji yaliyokuwepo kwa kizazi cha sasa na kijacho na kueleza kuwa changamoto kubwa inayokabili usimamizi wa rasilimali hiyo ni pamoja na uvamizi katika hifadhi za maji, ukataji miti, uchimbaji wa madini na mchanga katika hifadhi za maji pamoja na kuendesha shughuli za kilimo katika hifadhi za maji na kupitia jukwaa hilo hilo wanaamini changamoto hizo zitakomeshwa ili kuendelea kuhifadhi vyanzo vya maji.


Amesema kuwa matumizi ya maji yamekuwa makubwa majumbani na viwandani huku changamoto ya uchafuzi wa vyanzo hivyo ukipelekea maji kupungua, maji kubadilika na kuwa ya chumvi pamoja na kuchafuliwa kwa vyanzo hivyo kupitia maji ya viwandani na chemba za maji taka zilizoelekezwa kwenye vyanzo vya maji, ambapo amewashauri wananchi kutojihusisha na shughuli ambazo zitapelekea kuharibu vyanzo hivyo na watakaokiuka taratibu kwa kuharibu vyanzo hivyo watachukuliwa hatua za kisheria.

Bonde la Wami/Ruvu lilianza mwaka 2002 likihudumia Mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Manyara na jiji la Dodoma pamoja na Mbuga za Mikumi, Selous, Saadan na milima ya Tao na limeendelea kuhudumia na kuhakikisha viwanda na wananchi wanaotegemea bonde hilo wanapata huduma faaafu kulingana na matumizi yao na uwepo wa rasilimali hiyo.
 Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Wizara ya Maji Rosemary Rwebugisa akizungumza wakati uzinduzi wa jukwaa la watumiaji maji lililofanyika jijini Dar es Salaam.
 Mwenyikiti wa Bodi ya Bonde la Wami/Ruvu Hamza Sadiki akitoa maelezo kuhusiana na bonde  na wanavyotekeleza katika Uhifadhi wa vyanzo vya maji  katika uzinduzi Jukwaa la watumiaji maji lililofanyika jijini Dar es Salaam.
 Afisa wa Bonde la Wami/Ruvu Mhandisi Simon Ngonyani akizungumza kuhusiana hali ya Maji na hatua wanazozichukua kwa watumiaji  katika uzinduzi wa Jukwaa la watumiaji Maji lililofanyika jijini Dar es Salaam.

 Mhandisi wa Bonde la Wami/Ruvu Halima Abdallah akitoa maada katika mkutano wa Jukwaa la watumiaji maji lililofanyika jijini Dar Salaam.
 Baadhi wadau katika uzinduzi wa Jukwaa la watumiaji maji lililofanyika jijini Dar es Salaam.
Picha ya pamoja ya Mkurugenzi Msaidizi wa Wizara ya Maji Rosemary Rwebugisa na watendaji wa Wami/Ruvu pamoja na wadau katika uzinduzi wa Jukwaa la watumiaji maji lililofanyika jijini Dar es Salaam.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...