MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es salaam, imekataa kutoa amri kwa spika wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ya kutomuapisha Mbunge Mteule wa singida mashariki Miraji Mtaturu (CCM) kwa kuwa inaweza kuharibu maamuzi kesi ya msingi.

Jaji Sirilius Matupa amesema hayo leo Septemba 2, 2019 usiku huu, baada ya kusikiliza kusikiliza kesi ya Mwanasheria Mkuu wa CHADEMA, Tundu Lissu dhidi ya Spika wa Bunge kuhusu kutetea ubunge wake wa jimbo la Singida Mashariki kwa zaidi ya Massa 10.

Kesi hiyo iliyoanza kusikilizwa saa 4 asubuhi mbele ya Jaji Sirilius Matupa ambapo Lissu aliwakilishwa na Mawakili wanne, Kiongozi wa jopo akiwa Peter Kibatala na kwa upande wa Spika na Mwanasheria Mkuu uliwakilishwa na Mawakili 15, waliokuwa wakiongozwa na Wakili Mkuu wa Serikali Dk. Clement Mashamba.

Kabla ya kuahirishwa kwa kesi hiyo Jaji Matupa amesema, kuna wabunge wengi walishawahi kuapishwa lakini baada ya kesi kuisha walitolewa bungeni na kupatiwa wenye haki hivyo kutoa maamuzi ya haraka kwa hoja zilizotolewa na pande zote mbili zinaweza kuharibu kesi ya msingi. Pia amesema inatakiwa kupatikana muda wa kuweza kuchambua hoja zote kwa makini zilizowasilishwa ili maamuzi sahii yaweze kupatikana.

"Siwezi kutoa kwa sasa uamuzi wa kuzuia kuapishwa kwa huyo mbunge, hata akiapishwa sio tatizo uamuzi ukitolewa anaweza kuvuliwa ubunge wake pamoja na kiapo chake, hivyo uamuzi wangu nitautoa Septemba 9, mwaka huu, " amesema Jaji Matupa.

Aidha Jaji Matupa alisema hakubaliani na hoja ya Serikali ya kumtaka Wakili Magai ambaye ndio aliyeshuhudia kiapo cha Lissu kuja mahakamani kwani yeye alifanya kushuhudia tu. 

Wakili wa mleta Maombi, Peter Kibatala ndiye alikuwa wa kwanza kuwasilisha hojabzake wakati wa usikilizwaji ambapo amedai hatua zilizochukuliwa na Spika wa Bunge, Job Ndugai kutangaza kuwa jimbo analoliongoza Lissu la Singida Mashariki lipo wazi lilifanyika bila haki ya Lissu kusikilizwa na pia mchakato wa kumvua Lissu ubunge haukuwa shirikishi kwani hakuwahi kutaarifiwa rasmi sababu za yeye kutenguliwa ubunge wake bali alisikia barabarani. 

"Spika anatekeleza majukumu yake kwa kuongozwa na kanuni za Bunge, katiba pamoja na kupitia maamuzi ya Maspika waliopita, hata hivyo kanuni hizo zinamtaka kutoa uamuzi kwa kuzingatia haki bila upendeleo," ameeleza Kibatala. 

Wakili Kibatala aliongeza kuwa, mbunge asipoudhuria vikao kwa mujibu wa kanuni upewa adhabu, hivyo alihoji ni adhabu gani inayotolewa bila ya kumpatia mtu haki yake ya kumsikiliza kwanza, na kumuomba Jaji aangalie matilio waliyompatia kwani kupatia Jaji, kwani Lissu ameadhibiwa bila ya kupewa haki yake ya kusikilizwa.

Aidha wakili Kibatala katika hoja sake, ameiomba Mahakama hiyo itoe amri kwa Spika Ndugai kusimamisha kwa muda kuapishwa kwa mbunge mteule Miraji Mtaturu hadi kesi hiyo itakapomalizika kusikilizwa mahakamani na kuongeza kudai kuwa wakati Lissu anakwenda mahakamani ratiba za Bunge zilikuwa bado hazijapangwa hivyo kilichotangulia ni maombi ya Lissu na ratiba ndio ikafuatia. 

"Kikao cha Bunge kinaanza kesho na kabla ya kuanza lazima Spika awaapishe kiapo cha uadilifu wabunge wapya, hivyo tunaiomba Mahakama itoe amri ya kumzuia Spika kwa muda kumuapisha Mtaturu wakati mashauri yaliyopo mahakamani yatakaposikilizwa mbele yake Jaji ili tusiweze kupoteza maana ya kesi hii, " ameeleza Kibatala. 

Amedai kuwa kama mchakato wa kuapishwa kwa mbunge huyo utaruhusiwa kuendelea utafanya kazi ya mahakama kuwa ngumu. 

Wakijibu hoja hizo, wakili wa Serikali Mkuu, Aboubakary Mrisha amedai kuwa hati ya kiapo iliyowasilishwa mahakamani hapo inamapungufu kwani kimsingi Mleta maombi (Lissu) hajaonyesha ni kwa sababu zipi haki zimepotea, hivyo maombi hayo hayana msingi wa Mahakama kuyasikiliza na kudai kuwa maombi yaliyowasilishwa mahakamani hapo na aya zilizoendolewa kwenye hati ya kiapo ni maoni yao kwamba hayakidhi vigezo kwa kuwa vinahitajika kuangaliwa kwa umoja wake.

Wakili Mrisha ameendelea kudai kuwa mapungufu mengine yapo katika kipengele cha Allute Mughwai ambaye kiapo chake amekielezea kuwa kina aya nane wakati si kweli.

Katika Maombi ya ya Lissu yaliyofunguliwa ja kaka yake Alute Mughwai chini ya hati ya dharura, dhidi ya Spika wa Bunge la Tanzania na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), anaomba mahakama kibali cha kufungau shauri la maombi maalum kwa lengo la kupata amri mbalimbali kuhusiana na uamuzi huo wa kuvuliwa ubunge.

Amri hizo kwa mujibu wa hati ya maombi na hati ya maelezo yake ni pamoja na mahakama kumwamuru Spika Ndugai awasilishe mahakama taarifa ya kumvua ubunge, aliyoitoa bungeni, ili iweze kuupitia na kisha iamuru kuutengua na kuutupilia mbali.

Nyingine ni mahakama imwamuru Spika ampatie yeye Lissu nakala ya taarifa ya kumvua ubunge pamoja na itoe amri ya kusitishwa kuapishwa kwa mbunge mteule Mtaturu .

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...