Mkuu wa Wilaya ya Tunduru , Julius Mtatiro ametatua mgogoro wa muda mrefu kati ya Wananchi wa kijiji cha Chemchem katika kata ya Tuwemacho dhidi ya Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ambao ulianza mwaka 2014.

Mgogoro huo unahusisha madai ya kijiji cha Tuwemacho katika ujenzi wa Barabara Kuu ya Tunduru Songea na Tunduru Masasi miaka 5 iliyopita ambapo kokoto zilizokidhi vigezo na viwango zilichimbwa kwenye mgodi wa mawe wa kijiji hicho kwa ahadi kuwa halmashauri ingelilipa asilimia 20 ya mapato ya ushuru wa kokoto hizo kwa kijiji husika ambazo ni sawa na shs milioni 48 ambazo kama wangelizipata wangelianza ujenzi wa zahanati kijijini hapo.

Mtatiro amemwelekeza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Tunduru kuanza mara moja ujenzi wa zahanati ya kisasa ya shilingi milioni 84 katika kijiji cha Chemchem kama ishara ya kuwalipa wananchi fedha zao ambazo wamezidai bila mafanikio, na kwamba fedha hizo zina riba ambayo ni haki ya wananchi hao.

Pamoja na hatua hizo, Mtatiro ameelekeza Ofisi ya Mkurugenzi na Ofisa Tawala wa Wilaya ya Tunduru, waendelee kufanya mawasiliano na TANROAD ili fedha hizo zipatikane na ameelekeza zitakapotolewa zipelekwe katika kijiji husika moja kwa moja.

Aidha, Mtatiro kwa kushirikiana na mbunge wa jimbo la Tunduru Kusini, Mhe. Mpakate, wameamua kuanzisha ujenzi wa Ofisi ya kisasa ya kijiji ambapo Mtatiro atatoa mifuko 25 ya Simenti, Mbunge atatoa bati 60 na mifuko 25 ya Simenti na wananchi watachangia nguvu zao.

Katika mkutano huo, Mtatiro amesisitiza umuhimu wa kuwatendea haki wananchi na kupambana na shida na kero zao kama anavyofanya Rais Dkt John Pombe Magufuli.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...