Na Karama Kenyunko, Michuzi Tv.
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imewahukumu raia wawili wa China, Li Ling na Chen Guo, kulipa fidia ya Sh milioni 70 baada ya kukiri makosa ya kujihusisha na nyara za serikali na kuishi nchini bila kibali na wameamriwa kuondoka nchini mara moja kwa kuwa sio raia wa Tanzania.
Pia mahakama hiyo imetaifisha gari aina ya Toyota Prado lenye namba za usajili T 982 CDH na mashine mbili za washitakiwa hao na kuwa mali ya serikali.
Akisoma adhabu hiyo Leo Oktoba 9,2019 Hakimu Mkazi Mkuu Huruma Shaidi alisema kuwa mshitakiwa Ling atatakiwa kulipa fidia ya Sh milioni 45 na mshitakiwa Guo atalipa Sh milioni 25 na faini ya Sh milioni moja au kwenda jela mwaka mmoja kwa kosa la kuishi nchini bila kibali.
Hatua hiyo, imekuja baada ya upande wa mashitaka kuwafutia washitakiwa hao mashitaka ya utakatishaji fedha na kuwasomea mashitaka mawili ya kujihusisha na nyara za serikali na kuishi nchini bila kibali.
Hata hivyo, washitakiwa wengine wanne waliokuwa katika kesi hiyo wamegoma kukiri mashitaka yao yanayowakabili hivyo wamerudishwa rumande.
Kabla ya kutolewa adhabu, Wakili wa Serikali, Salim Msemo amedai hawana kumbukumbu ya makosa ya nyuma ya washtakiwa hivyo, aliomba mahakama itoe adhabu kulingana na makubaliano ili iwe fundisho kwao na wengine.
Wakili Msemo amedai kuwa wameingia makubaliano na washitakiwa hao baada ya kukiri kosa la kujihusisha na nyara za serikali na kuishi nchini bila kibali, hivyo wameamua kuondoa kesi ya uhujumu uchumi.
Baada ya kusoma makubaliano hayo, Hakimu Shaidi amewaapisha washitakiwa na kuwauliza kama walisaini kwa hiari yao na kudai walifanya hivyo kwa hiari yao.
Akisoma mashitaka mapya, Wakili Misemo amedai Julai 5,2015 katika Uwanja wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) mshitakiwa Ling alisafirisha nje ya nchi kucha 25 za simba zenye thamani ya Sh 22, 500,000 bila kuwa na kibali.
Amedai katika kosa lingine Julai 5, 2015 katika uwanja wa Kimataifa wa Julius Nyerere mshtakiwa Cheng Guo alisafirisha nje ya nchi meno 21 ya simba yenye thamani ya Sh 12, 500,000 bila ya kuwa na kibali.
Msemo amedai Januari 18, 2015 mshitakiwa Guo alikutwa akiwepo nchini kinyume na sheria.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...