Mratibu wa Kitengo cha Kifua Kikuu na Ukoma kutoka hospitali ya wilaya ya Tunduru Mkoani Ruvuma, Dkt. Mkasange Kihongole amewatahadharisha wananchi katika wilaya hiyo kuacha kunywa maziwa ya Ng’ombe holela kutoka kwa wafugaji wanaoingia katika maeneo yao na kwamba Maziwa hayo yanaweza kuwa na vimelea ambavyo ni chanzo kikubwa cha kuenea kwa Ugonjwa wa Kifua kikuu kwa lugha ya kitaalamu ‘BOVINE TUBERCULOSIS’

Dkt Kihongole ametoa kauli hiyo jana ,wakati akiongea na wakazi wa kijiji cha Semeni kata ya Mtina katika uzinduzi wa kampeni maalumu ya uhamasishaji na uchunguzi wa vimelea vya ugonjwa wa Kifua Kikuu kwa wananchi wa kata hiyo,

Dkt. Kihongole alisema licha ya wilaya ya Tunduru kuwa na maambukizi makubwa ya ugonjwa wa kifua kikuu, hali hiyo inachangiwa pia na unywaji holela wa maziwa ya Ng’ombe yasiyopimwa ambayo ni hatari zaidi kwani usababisha kwa kiwango kikubwa kuenea kwa ugonjwa huo unaotajwa kuwa ni kati ya magonjwa kumi yanayoongoza kuuwa Watu wengi Duniani.

Kwa mujibu wa Kihongole,siku za hivi karibuni kumekuwa na mwingiliano mkubwa wa wafugaji katika maeneo mbalimbali wilayani humo wanaoingia kutoka mikoa mingine hapa Nchini, wakiwa na Ng’ombe ambao hawajapimwa jambo linalo changia kuongezeka kwa maradhi ya kifua kikuu pale wananchi wanapokunywa maziwa ya Ng’ombe wasiopatiwa tiba sahihi.

Alisema, ndiyo maana Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na wadau wengine ikiwemo Global Fund imeanza kuchukua hatau ya kutokomeza Ugonjwa huo ifikapo mwaka 2030 na kusisitiza kuwa, ni muhimu jamii kuchukua tahadhari kuhusiana na ugonjwa wa Kifua kikuu.

Kihongole alitaja makundi yaliyo katika hatari ya kupata maradhi hayo ni Wazee kwani kadri Binadamu umri unavyokuwa mkubwa kinga za mwili zinapungua,watoto walio chini ya umri wa miaka mitano,wasafiri,watu walio katika msongamono kama vile wafungwa na wale wanaoishi kwenye nyumba ambazo hazina hewa na mwanga wa kutosha kwani wadudu wa kifua kikuu upendelea kuishi kwenye giza .

Alisema, ugonjwa wa kifua kikuu ni hatari zaidi kuliko Ukimwi,kwa sababu mgonjwa mmoja anaweza kuambikza watu kumi na tano kwa wakati mmoja na Tb inayoogoza kuambukiza kwa haraka ni Tb ya mapafu ambayo mtu anapata kupitia mfumo wa Hewa.

Kihongole alitaja dalili za mtu aliyeambukizwa Tb ni kukohoa kwa wiki mbili au zaidi,kutokwa na jasho jingi hasa nyakati za usiku,kupungua uzito,kupoteza hamu ya kula, na kwa watoto wadogo kuchelewa kukua,kulia lia na kuwa na homa za mara kwa mara.

Dkt Kihongole,amewakumbusha wazazi na walezi kuwa na utaratibu wa kupeleka watoto wao katika vituo vya kutolea huduma kwa ajili ya uchunguzi wa Afya zao mara kwa mara,badala ya kuamini mambo ya kishirikina ambayo usababisha kupoteza maisha ya watu wengi hasa watoto wadogo.

Kwa upande wake,Muuguzi Mkuu wa Halmashauri ya wilaya ya Tunduru Renatus amewataka watu wanaofanyiwa vipimo na kubainika kuwa na vimelea vya ugonjwa wa Tb ni vema kuhakikisha wanamaliza dozi(Dawa)wanazopewa na kuepuka kukatisha dawa kwani ni hatari sana kwa Afya zao na watu wengine.

Aidha,ameitaka jamii kuwaibua watu wanaohisiwa kupata ugonjwa huo na magonjwa mengine yanayoambukiza na kuwafikisha katika vituo vya kutolea huduma ili kupata tiba itakayowasaidia kuwa na Afya njema na uwezo wa kushiriki katika ujenzi wa Taifa.

Amewakumbusha akina mama pindi wanapoona dalili za ujauzito ni vema kwenda kliniki haraka na wenza wao kupata ushauri wa wataalam na kuhakikisha wanatumia zahanati na vituo vya Afya kujifungulia badala ya kubaki nyumbani kwani ni hatari kwa afya zao na watoto wakati wa kujifungua.

Hata hivyo,mmoja wa wakazi wa kijiji hicho Hamza Malembo ameiomba Serikali kupeleka Dawa na vifaa tiba vya kutosha ili kuwasaidia kwani baadhi ya Zahanati hasa zile za maeneo ya pembezoni zina upungufu mkubwa na wanapofika vituoni wanaelekezwa kwenda kununua kwenye maduka ya watu binafsi,jambo linalowakatisha sana tamaa.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...