Na Munir Shemweta, WANMM KILIMANJARO
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline
Mabula ameziwataka idara za ardhi katika halmashauri nchini kuyabainia
mashamba yote yasiyoendelezwa (Mashamba Pori) na kupeleka mapendekezo
ya kufutwa mashamba hayo Wizarani.
Dkt Mabula alisema hayo jana alipokutana na watendaji wa sekta ya
ardhi pamoja na wakurugenzi wa halamashauri zote za mkoa wa
Kilimanajaro akiwa katika zaiara yake ya siku mbili mkoani humo
kukagaua utendaji kazi wa sekta ya adhi.
Dkt Mabula alisema, pamoja na baadhi ya mashamba kufutwa katika maeneo
mbalimbali nchini kutokana na kutoendelezwa lakini kuna maeneo mengine
maafisa ardhi wameshindwa kuyatolea taarifa mashamba yasiyoendelezwa
ili yafutwe kwa sababu wanazozijua wenyewe.
‘’Nataka taarifa ya mashamba yote pori katika halmashauri yabainishwe
na kutolewa taarifa ili tuweze kupeleka mapendekezo ya kufutwa
mashamba hayo kwa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania’’ alisema
Dkt Mabula
Kwa mujibu wa Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi,
taarifa ya kubaini mashamba yote pori katika kila halmashauri ziwe
zimewasilishwa kufikia desemba mwaka huu na Januari 2010 timu maalum
itaundwa kwa ajili ya kazi hiyo.
Dkt Mabula alisema, Afisa Ardhi katika halmashauri yoyote
atakayebainika kuficha ukweli kuhusiana na uwepo mashamba pori katika
eneo lake hatua kali za kinidhamu zitachukuliwa dhidi yake.
‘’Maafisa Ardhi mnashirikiana na baadhi ya wenye mashamba pori na
mnashindwa kuleta mapendekezo ya kufutwa mashamba, sisi tunahitaji
kuona kila ardhi inatumika katika malengo yaliyokusudiwa’’ alisema Dkt
Mabula
Mapema katika kikao hicho, baadhi ya Wakurugenzi wa Halmashauri za
mkoa wa Kilimanajaro pamoja na Maafisa Ardhi alimueleza Naibu Waziri
wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuwa, idara za ardhi katika
halmashauri zao zinakabiliwa na changamoto kubwa za upungufu wa
watumishi katika fani tofauti za sekta ya ardhi pamoja na bajeti
finyu.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Moshi Kastori Msigala
alieleza kuwa halmashauri yake inakabiliwa na upungufu wa watumishi
katika fani za Mipango Miji, Upimaji na Uthamini jambo alilolieleza
kuwa linachangia kwa kiasi kikubwa kutofikia malengo katika sekta ya
ardhi.
Katika hatua Nyingine Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya
Makazi Dkt Angeline Mabula ameridhishwa na maendeleo ya ujenzi wa
Ofisi na Nyumba za Wakala wa Huduma za Misitu TFS katika Shamba la
Miti la Kilimanjaro Kaskazini maarufu kama Rongai lililopo wilayani
Rombo mkoa wa Kilimanjaro
Kwa mujibu wa Kaimu Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa mkoa wa
Kilimanjaro Stanley Msoffe, Ujenzi wa Ofisi na Nyumba za Watumishi wa
TFS unaofanywa na NHC unagharimu zaidi ya milioni 532.9 unatarajiwa
kukamilika mwezi Juni 2020.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akitoa maelekezo kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halamashauri ya Wilaya ya Moshi Kastori Msigala baada ya kukagua Majalada ya Ardhi katika Ofisi za Ardhi za Halamashauri hiyo jana wakati wa ziara yake ya kukagua utendaji kazi wa sekta hiyo mkoani Kilimanjaro. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Moshi Kippi Warioba.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akitoa maelekezo kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Moshi Kastori Msigala kabla ya kuondoka jana wakati wa ziara yake ya kukagua utendaji kazi wa sekta hiyo mkoani Kilimanjaro. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Moshi Kippi Warioba.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akikagua maendeleo ya ujenzi wa Ofisi na Nyumba za Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) katika shamba la Miti la Kilimanjaro Kaskazini (Rongai) uliopo wilayani Rombo mkoa wa Kilimanjaro jana wakati wa ziara yake ya siku mbili mkoani humo. Kulia ni Mhandisi wa ujenzi wa mradi huo kutoka Shirika la Nyumba la Taifa Peter Mwaisabula.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akioongozwa na Kaimu Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa mkoa wa Kilimanjaro Stanley Msoffe (Kulia) kwenda kukagua maendeleo ya ujenzi wa Ofisi na Nyumba za Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) katika shamba la miti la Kilimanjaro Kaskazini (Rongai) uliopo wilayani Rombo mkoa wa Kilimanjaro jana wakati wa ziara yake ya siku mbili mkoani humo.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt
Angeline Mabula akizungumza na wafanyakazi wanaojenga nyumba za
watumishi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) katika shamba
la miti la Kilimanjaro Kaskazini (Rongai) lililopo Rombo mkoa wa
Kilimanjaro wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa Ofisi na Nyumba za
TFS jana wakati wa ziara yake ya siku mbili mkoani humo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...