RAIA wa India ambaye ni meneja wa tawi la kampuni ya Neelkani Salt Limited, Mohammed Alikhan (29) amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi yenye mashtaka mawili.
Katika kesi hiyo namba 114 ya mwaka huu, mshtakiwa anakabiliwa na mashtaka mawili ya utakatishaji wa fedha na wizi wa katoni za chumvi 45,919 zenye thamani ya Sh413, 559,000/_
Akisoma hati ya mashtaka, wakili wa Serikali Mwandamizi, Wankyo Simon amedai Mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Janeth Mtega kuwa kati ya Januari Mosi, 2018 na Julai 29, mwaka huu katika mtaa wa Arusha Ilala, Jijini Dar Es Salaam, Alikhan akiwa Meneja wa tawi la kampuni hiyo aliiba katoni za chumvi 45,871 aina ya Neel Mali ya mwajiri wake zenye thamani ya Sh 412,839,000.
Pia mshtakiwa huyo anadaiwa katika kipindi hicho aliiba kilo moja ya chumvi aina ya Neel Gold yenye thamani ya Sh 720,000. Mshtakiwa huyo anadaiwa pia kuiba jumla ya chumvi 45,919 zenye thamani ya Sh 413,559,000.
Aidha, imedaiwa, siku na mahali hapo, mshtakiwa Alikhan alitakatisha kiasi cha Sh 413,559,000 wakati akijua fedha hizo zimetokana na zao la makosa la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na wizi akiwa mwajiliwa.
Hata hivyo, baada ya kusomewa mashtaka hayo mshtakiwa hakuruhusiwa kujibu kitu chochote kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza Kesi za Uhujumu Uchumi napi shtaka la utakatishaji fedha halina dhamana.
Kwa mujibu wa upande wa mashtaka upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika na mshtakiwa amerudishwa rumande. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Novemba 5, mwaka huu.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...