mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo

NA MWAMVUA MWINYI,KISARAWE

WAKAZI wa Kitongoji cha King’azi A wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani wako hatarini kukosa haki yao ya msingi ya kujiandikisha kwa ajili ya kupiga kura kwenye uchaguzi wa Mitaa ,Vijiji na Vitongoji Novemba 24 mwaka huu “:,ambapo waliojiandikisha hadi sasa ni wanne kati ya 560 wanaotarajiwa kujiandikisha .

Hatihati hiyo inahofiwa kuchukua nafasi baada ya baadhi ya watu kuwadanganya kuwa wanapaswa kujiandikisha kupitia wilaya ya Ubungo Jijini Dar es Salaam jambo ambalo si la kweli.

Hali hiyo ilibainika wakati wa ziara ya mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo kuhamasisha wananchi kujiandikisha kwenye daftari la wapiga kura kwenye mkoa huo.

Akiwa na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa huo alifika kwenye kituo hicho na kukuta wananchi waliojiandikisha ni wanne tu kati ya 560 wakidai kuwa wao watajiandikisha kitongoji cha King’azi B ambacho kipo upande wa Ubungo.

Alisema baada ya viongozi wa mikoa hiyo na wataalamu mbalimbali waliridhia vitongoji hivyo kugawanywa ambapo walikubaliana King’azi A itabaki mkoa wa Pwani na Kingazi B na sehemu kidogo ni Ubungo Jijini Dar es Salaam.
“Awali kulikuwa na mgogoro lakini Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Tanzania (TAMISEMI) walipitisha mipaka na kugawanya maeneo hayo lakini baadhi ya wananchi wanasema kuwa mitaa yote iko eneo la wilaya ya Ubungo lakini King’azi A ni Kisarawe na King’azi B ni Wilaya ya Ubungo”, alisema Ndikilo.

” Nimesikia kuna mtu anaitwa magodoro ndiyo anayepotosha wananchi wakajiandikishie Ubungo jambo ambalo si kweli na endapo ataendelea kuwapotosha wananchi hatua kali zitachukuliwa dhidi yake kwani ni kinyume cha sheria kuvuruga uchaguzi,”alisema Ndikilo.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Kisarawe Jokate Mwegelo alisema kuwa tayari suala la mipaka ya wilaya ya Kisarawe na Ubungo iliwekwa na wananchi walielezwa.

Akiwa wilayani Mkuranga Ndikilo aliwapongeza viongozi wa wilaya hiyo ambapo hadi juzi walikuwa wameandikisha wananchi 70,000 kati ya wananchi 84,000 wanaotarajiwa kiandikishwa tofauti na wilaya nyingine ambazo zilikuwa bado zina wananchi wachache waliojiandikisha.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...