Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) akiwa na Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe Juma Homera wakikagua ghala la mbolea kujionea kiasi kilichopo katika ghala la Tarimo lililopo Mpanda mkoani Katavi leo tarehe 13 Octoba 2019. 
Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) akisisitiza jambo wakati akihutubia wananchi waliojitokeza kwenye maadhimisho ya siku ya mbolea Duniani ambayo Kitaifa yamefanyika leo tarehe 13 Octoba 2019 katika viwanja vya shule ya msingi Kashaulili Wilayani Mpanda mkoani Katavi. (Picha Zote Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo)
Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe Juma Homera akitoa tathmini ya hali ya uzalishaji wa chakula katika mkoa huo kadhalika kuhusu hali ya upatikanaji wa mbolea wakati wa maadhimisho ya siku ya mbolea Duniani ambayo Kitaifa yamefanyika leo tarehe 13 Octoba 2019 katika viwanja vya shule ya msingi Kashaulili Wilayani Mpanda mkoani Katavi.
Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) akiwa ameongozana na Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe Juma Homera wakikagua mabehewa ya kubeba mazao mbalimbali kwa ajili ya kuyasafirisha katika kituo cha reli Mpanda mkoani Katavi leo tarehe 13 Octoba 2019.

Sehemu ya washiriki wakisikiliza hotuba ya Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) wakati wa maadhimisho ya siku ya mbolea Duniani ambayo Kitaifa yamefanyika leo tarehe 13 Octoba 2019 katika viwanja vya shule ya msingi Kashaulili Wilayani Mpanda mkoani Katavi.
Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya udhibiti wa mbolea Tanzania Dkt Steven Ngailo akitoa taarifa kuhusu hali ya upatikanaji wa mbolea wakati wa maadhimisho ya siku ya mbolea Duniani ambayo Kitaifa yamefanyika leo tarehe 13 Octoba 2019 katika viwanja vya shule ya msingi Kashaulili Wilayani Mpanda mkoani Katavi.



Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Katavi

Kutokana na kuwepo kwa mfumo wa ununzi wa mbolea kwa pamoja (BPS) serikali imeviagiza Vyama vya ushirika vya msingi (AMCOs) na vyama vikuu (FCU) kuanza kushiriki kwenye ununzi wa mbolea kwa pamoja (BPS) ili kuhakikisha upatikanaji wa mbolea kwa bei nafuu na kwa wakati.

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) ametoa agizo hilo wakati akizungumza kwenye maadhimisho ya siku ya mbolea Duniani ambayo Kitaifa yamefanyika leo tarehe 13 Octoba 2019 katika viwanja vya shule ya msingi Kashaulili Wilayani Mpanda mkoani Katavi.

Amesema kuwa ili kuongeza matumizi ya mbolea nchini, Wizara ya kilimo kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) imeweka mikakati mbalimbali ya kuhakikisha mbolea inapatikana kwa wakati na kwa bei nafuu ikiwemo mfumo wa unuzi wa mbolea kwa pamoja (BPS).

Pia, imeendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo kutoa elimu kwa njia tofauti kwa lengo la kuongeza uelewa wa umuhimu na kuongeza matumizi ya mbolea nchini hivyo ili tija na uzalishaji viongezeke vyama vya ushirika havina budi kushiriki kwenye ununuzi wa mbolea ili kuwarahisishia wanachama wao ambao ni wakulima kupata mbolea kwa wakati na kwa bei nafuu.

Mhe Hasunga ametoa mwito kwa wafanyabiashara wa mbolea kuuza mbolea kwa bei elekezi iliyopangwa na serikali na wazingatia bei hizo kwa mbolea za kupandia (DAP) na kukuzia (UREA) ambazo zinaingizwa nchini kwa mfumo wa Uingizaji wa Mbolea kwa Pamoja yaani Bulk Procurement System BPS.

“Kama mnavyofahamu, Serikali imeendelea kuratibu utoaji wa mikopo yenye riba nafuu kupitia Benki ya Maendeleo ya Kilimo (Tanzania Agriculture Development Bank-TADB), Benki ya Uwekezaji (Tanzania Investment Bank TIB) na Mfuko wa Pembejeo wa Taifa. Hivyo, nitoe wito kwa wakulima wote wa Mkoa wa Katavi na Mikoa mingine kujiunga katika ushirika ili kuweze kutumia fursa zinazotolewa na taasisi hizi ili kujiletea maendeleo” Alikaririwa Mhe Hasunga

Waziri Hasunga amesema kuwa ili kuwa na matumizi sahihi ya mbolea, ufahamu juu afya ya udongo ni muhimu; hivyo, ameiagiza Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) kutoa taarifa ya afya ya udongo kwa wakulima na wadau wengine ili matumizi ya mbolea yaendane na mahitaji ya zao na udongo husika.

Niwakumbusha wafanyabiashara wakubwa kuwa mbolea zinahitajika zaidi mikoani; hivyo ni wakati muafaka wa kuanza kusambaza mbolea mikoani haraka iwezekanavyo. Pia ni wakati sahihi wa kufungua matawi ya mauzo na maghala mikoani badala ya mbolea nyingi kurundikana kwenye maghala yaliyoko Dar es salaam ambako mahitaji yake ni madogo.

Ameongeza kwa kusema kuwa ili mbolea iweze kuwafikia wakulima kwa wakati, amelitaka shirika la reli Tanzania (TRC) kutoa kipaumbele katika usafirishaji wa mbolea kwa mikoa ya Tabora, kigoma na Katavi huku akiitaka Mamlaka ya udhibiti wa mbolea (TFRA) kuhakikisha inasimamia ubora wa mbolea kuanzia bandarini inapoingia hadi kwa muuzaji anayemuuzia mkulima.

Kauli mbiu ya maadhimisho haya ni ‘matumizi sahihi ya mbolea kwa uhakika wa chakula na uchumi wa viwanda’. Ambapo lengo la maadhimisho ya siku ya mbolea duniani nchini Tanzania ni kupata wigo mpana zaidi kwa Wadau kuelezea masuala mbalimbali katika tasnia ya mbolea. 

Masuala hayo ni pamoja na mafaniko ya tasnia ya mbolea nchini, kuwahabarisha wadau wa mbolea hususani wakulima na wafanyabiashara wa mbolea mifumo mbalimbali ya upatikanaji na usambazaji wa mbolea; pia kutoa elimu kuhusu sheria, kanuni na taratibu zinazosimamia tasnia ya mbolea.

Siku ya mbolea duniani ilianza kuadhimishwa kwa mara ya kwanza tarehe 13 Oktoba, 2016 huko nchini Uingereza. Siku hii ilianzishwa mahsusi kwa lengo la kuhamasisha Wadau wa tasnia ya mbolea duniani kote kutambua jukumu kubwa walilonalo la kuhakikisha kuwa wakulima wanatumia mbolea bora na sahihi ili kuleta mapinduzi ya kijani kwa uhakika wa chakula.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe Juma Homera amesema kuwa tayari serikali imetangaza bei elekezi ya mbolea hivyo wafanyabiashara watakaokiuka na kuanza kuuza kwa bei zaidi ya hiyo watachukuliwa hatua za kisheria.

Amesema kuwa serikali inayoongozwa na Mhe Rais Dkt John Pombe Magufuli imedhamiria kuwanufaisha wakulima kwenye sekta ya kilimo hivyo kukiuka maelekezo ya serikali kwa wafanyabiashara wa mbolea hawana tofauti na wahujumu uchumi.

Akizungumzia kuhusu uzalishaji wa mazao ya chakula amesema kuwa mkoa wa Katavi kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo utahamasisha wakulima kulima mazao mengi kwa tija ili kuongeza uzalishaji utakaoimarisha usalama wa chakula nchini.

Kwa upande wake Kaimu Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Mbolea Tanzania (TFRA) Dkt Steven Ngailo amesema kuwa mbolea kwa ajili ya kukuzia na kupandia tayari imewasili nchini hivyo wakulima wana fursa mahususi kabisa ya kujitokeza na kuendeleza sekta ya kilimo katika kuongeza uzalishaji wa chakula kwa ajili ya biashara.

Ameitaja kuwa siku ya mbolea Duniani ni kumbukizi ya maadhimisho ya uvumbuzi wa mbolea aina ya Amonia uliofanywa na Bwana Fritz Haber mwaka 1908. Uvumbuzi huo ulichochea mapinduzi ya kijani katika karne ya 20 yaliyowezesha kuongezeka kwa uzalishaji wa mazao kutokana na matumizi ya mbolea yaliyosaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa janga la njaa na kuleta uhakika wa chakula katika nchi nyingi duniani.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...