WAZIRI wa Maliasili na Utalii Dk Hamisi Kigwangalla anatarajiwa kuongoza maelfu ya washiriki wa mbio za Rock City Marathon zinazoratarajiwa kufanyika Oktoba 20, mwaka huu kwenye viunga vya Jengo la Biashara la Rock City Mall, jijini Mwanza.
 
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa mapema hii leo jijini Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya mbio hizo, Bw Clement Mshana, ushiriki wa Waziri Kigwangalla unaenda sambamba na ushiriki wa viongozi wengine waandamizi wa serikali kutoka mikoa ya Kanda ya Ziwa akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Bw John Mongella ambaye tayari amethibitisha kushiriki katika mbio za KM 42.
“Uwepo wa Waziri mwenye dhamana na masuala ya utalii kwenye mbio hizi unatokana na yeye kuunga mkono agenda iliyobebwa na mbio hizi ambayo mbali na kukuza vipaji vya mchezo huo ni kutangaza utalii hususani katika  ukanda wa Ziwa kupitia mchezo wa riadha,’’Alisema
Mbio hizo zilizoanzishwa miaka kumi iliyopita zinatarajiwa kupambwa na burudani mbalimbali zikiwemo ngoma za asili na maonesho ya waadau  mbalimbali wa utalii ikiwemo Wizara ya Maliasili na Utalii, Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) sambamba  na wadhamini wa mbio hizo ambao ni pamoja na  kampuni za TIPER na  Pepsi.
Wadhamini wengine ni pamoja na, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR), CF Hospital, Metro FM,  Mwanza Water, Pigeon Hotel, The Cask and Grill, SDN na Kampuni ya Ulinzi ya Garda World. 
 “Ukanda wa Ziwa una vivutio vingi ambavyo lazima vitangazwe kimataifa kwa nguvu kubwa zaidi na mbio hizi zimekuwa kama chachu ya kufanikisha agenda hiyo hususani kwa mwaka huu ambapo zinatarajiwa kuhusisha wadau wengi zaidi wa masuala ya utalii ambao pamoja na mambo mengine watapata fursa ya kuonesha bidhaa na huduma zao kwenye viunga vya mbio hizo’’ alibainisha. 
Aidha, zikiwa zimesalia siku chache tu kabla ya kufanyika kwa mbio hizo tayari wadau mbalimbali wanaotarajia kushiriki wameonesha kufurahishwa na zawadi zitakazotolewa kwa washindi na washiriki zikiwemo medali na fedha taslimu zaidi ya Sh Mil 30.
“Pamoja na medali washindi wa kwanza wa mbio za kilomita 42 kwa wanaume na wanawake watajinyakulia sh. Mil 4 kila mmoja, sh.mil 2/-  kwa washindi wa pili na sh. Mil 1/- kwa washindi wa tatu, huku washindi wanne hadi kumi na tano nao pia wakiibuka na zawadi  za medali na pesa taslimu.’’
“Kwa upande wa mbio za  Kilomita 21, pamoja na medali washindi wa kwanza kwa wanaume na wanawake watajinyakulia sh.  Mil 2/- kila mmoja, sh. Mil 1/-kwa washindi wa pili na sh. Laki 7/- kwa washindi wa tatu huku pia washindi wanne hadi wa kumi na tano wakiibuka na  zawadi za pesa taslimu na medali kila mmoja.’’ alitaja
Kuhusu mbio za kilomita tano ambazo zitahusisha washiriki kutoka mashirika na taasisi mbalimbali (corporates), Bw Mshana alisema inatarajiwa kuwa zitaongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Dk Philis Nyimbi sambamba na washiriki wenye ualbino ambapo zawadi za fedha taslimu zitatolewa kwa washindi watatu wenye ualbino pekee.
“Kwa washindi wa mbio za kilomita 2.5 zitakazohusisha watoto wenye umri kati ya miaka 7 hadi 10 washindi watapatiwa  fedha taslimu.’’ Alibainisha.
Akizungumzia usajili wa mbio hizo Bw. Mshana alitoa wito kwa washiriki kuendelea kujisajili kupitia vituo na mawakala wa mbio hizo katika mikoa ya Mwanza, Dar es Salaam, Dodoma, Pwani na Arusha
‘’Kwa sasa usajili wa mbio hizo unaendelea kupitia vituo mbalimbali katika mikoa ya Mwanza (Rock City Mall, Pasiansi Afro Twist Gym), Dodoma (Shabiby Bus Terminal), Dar es Salaam (Shamo Tower, Imalaseko Super Market (Posta), Heleana Fashion – Dar Free Market), Arusha pamoja na Bagamoyo mkoani Pwani.’’
 “Pia usajili unaweza kufanyika kwa njia ya  mtandao kupitia website yetu ya Rock City Marathon ambayo ni www.rockcitymarathon.co.tz. ’’ alitaja

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...