Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi
Mhe. Abdallah Ulega akifungua eneo lililowekwa jiwe la msingi kuashiria
ufunguzi rasmi wa FETA Kampasi ya Mikindani, Mkoani Mtwara.
Baadhi ya wahitimu wa kozi fupi za
ufugaji samaki wakimsikiliza mgeni rasmi Naibu Waziri wa Mifugo na
Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega wakati wa ufunguzi wa FETA Kampasi ya
Mikindani, Mkoani Mtwara.
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi
Mhe. Abdallah Ulega (wa tatu kutoka kulia) akikata utepe kuashiria
kufunguliwa rasmi kwa FETA Kampasi ya Mikindani, Mkoani Mtwara
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi
Mhe. Abdallah Ulega akizungumza na wahitimu wa kazo fupi za ufugaji
samaki (hawapo pichani) wakati wa ufunguzi wa FETA Kampasi ya
Mikiandani, Mkoani Mtwara.
*********************************
Na. Edward Kondela
Serikali imesema
inahakikisha sera yake ya kuhamasisha wananchi kufuga samaki
inatekelezwa kote nchini ili kutosheleza mahitaji ya soko la samaki
nchini pamoja na kukuza pato la taifa na mtu mmoja mmoja.
Akizungumza Mjini
Mtwara, wakati akifungua tawi la Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi
(FETA) Kampasi ya Mikindani Mkoani Mtwara, Naibu Waziri wa Mifugo na
Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega ameiagiza FETA kwa kushirikiana na Idara ya
Ukuzaji Viumbe kwenye Maji kutoka katika wizara hiyo, kuandaa mitaala ya
ufugaji viumbe kwenye maji wakiwemo samaki, kaa, majongoo bahari na
Kambakochi kwa ajili ya wananchi wa Ukanda wa Pwani ili waweze kuongeza
vipato vyao kupitia fursa ya ufugaji.
Mhe. Abdallah Ulega – Naibu waziri wa Mifugo na Uvuvi
Aidha Mhe. Ulega
ameagiza uundwaji wa vikundi vya uzalishaji kaa, Kambakochi, majongoo
bahari pamoja na wazalishaji wa zao la mwani ili iwe rahisi kwa vikundi
hivyo kutambulika rasmi pindi mazao yao yanapohitajika sokoni, na watu
waweze kufika katika mashamba yao ya ufugaji kwa ajili ya kuvua samaki
na viumbe vingine wakiwemo kaa, kambakochi na majongoo bahari ambao
wamekuwa na soko kubwa sana na mahitaji yake kuongezeka katika baadhi ya
maeneo zikiwemo hoteli za kitalii.
Kwa upande wake
Mkurugenzi wa Mafunzo kutoka FETA Bw. Ambakisye Simtoe amesema chuo
hicho kimepanga kuzalisha wagani kwa ajili ya kuendeleza na kukuza
tasnia ya uvuvi nchini pamoja na kununua mashine ya kuzalisha vifaranga
bora ili iwe rahisi kwa wananchi wa Ukanda wa Pwani kupata vifaranga
hivyo kwa bei nafuu huku katika risala ya wanafunzi hao wakisema mafunzo
waliyoyapata yakiwemo ya ufugaji wa samaki yatawawezesha kujiajiri.
Bw. Ambakisye Simtoe – Mkurugenzi wa Mafunzo FETA
Bi. Monica Mfaume – Msoma risala kwa niaba ya wanafunzi
Jumla ya
wanafunzi 62 wamehitimu kozi fupi ya ufugaji samaki katika chuo cha FETA
Kampasi ya Mikindani Mkoani Mtwara na kukabidhiwa vyeti na mgeni rasmi
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega ambaye amekifungua
rasmi chuo hicho chenye uwezo wa kudahili wanafunzi 240 kwa mwaka.
Kwa mujibu wa
takwimu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi mahitaji ya soko la samaki
nchini ni Tani 700,000 hadi 800,000 kwa mwaka huku uzalishaji ukiwa
wastani wa Tani 400,000 hadi 450,000 hali ambayo Naibu Waziri Ulega
amesisitiza kwa chuo cha FETA Kampasi ya Mikindani Mkoani Mtwara kuwa
kampasi ya mfano katika kutoa mafunzo ya ufugaji samaki, kaa, kambakochi
na majongoo bahari ili wananchi waweze kutosheleza soko la ndani na
kukuza vipato vyao na taifa kwa ujumla.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...