Kazi ya uchimbaji wa msingi kwa
ajili ya kusimika nguzo za chuma katika Mradi wa njia ya kusafirisha
umeme kutoka Bulyanhulu hadi Geita ikiendelea. Taswira hii ilichukuliwa
Januari 20, mwaka huu wakati Kamishna Msaidizi wa Umeme, Mhandisi
Innocent Luoga alipotembelea Mradi huo.
Kamishna Msaidizi wa Umeme,
Mhandisi Innocent Luoga (katikati), akitoa maagizo kwa Mkandarasi
anayetekeleza Mradi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka Bulyanhulu hadi
Geita.
Hatua iliyofikiwa katika ujenzi wa kituo cha kupoza umeme cha Bulyanhulu.
Kamishna Msaidizi wa Umeme
Mhandisi Innocent Luoga, amefanya ziara ya kukagua utekelezaji wa Mradi
wa ujenzi wa Njia ya Kusafirisha Umeme ya msongo wa kilovoti 220
inayoanzia Bulyanhulu hadi Geita na kumtaka Mkandarasi kuanza kazi ya
kusimika nguzo za chuma ifikapo Februari 2020.
Mhandisi Luoga alifanya ziara
hiyo Januari 20, 2020 kukagua Mradi huo ambao unahusisha pia ujenzi wa
vituo vya kupoza Umeme katika eneo la Bulyanhulu, Wilayani Kahama na
katika Mkoa wa Geita, pamoja na kusambaza umeme katika vijiji 10
vinavyopitiwa na Mradi huo.
“Nimeridhishwa na kasi ya
ujenzi wa vituo vya kupoza umeme vya Bulyanhulu na Geita lakini
sijaridhishwa na kazi ya usimikaji wa nguzo za kusafirisha Umeme ambapo
misingi 52 kati ya misingi 161 imekamilika na hakuna nguzo
iliyosimamishwa. Nawataka Mkandarasi na Mhandisi Mshauri kujipanga upya
ili Mradi huo wenye lengo la kuimarisha upatikanaji wa umeme katika
Wilaya za Kahama, Geita, Chato, Biharamulo na Ngara pamoja na
kuunganisha Mkoa wa Geita katika Gridi ya Taifa ukamilike kwa wakati.”
Aidha, Mhandisi Luoga
alimuagiza Mkandarasi kufanya kazi siku zote, kuongeza idadi ya mafundi
na vifaa maalum vya kuchimba katika miamba ili kuhakikisha nguzo
zinaanza kusimamishwa ifikapo Februari 2020 na Mradi huo unakuwa tayari
kusafirisha umeme .
Akitoa maelezo kwa Kamishna,
Mhandisi wa Mradi Ramadhani Kidunda alisema Mradi huo unatarajiwa
kukamilika tarehe 30 Mei 2020 na utahusisha pia kusambaza Umeme katika
vijiji 10 vinavyopitiwa na Mradi husika pamoja na Vituo vya kupoza Umeme
katika eneo la Bulyanhulu na GEITA .
Kamishna Luoga aliwataka
Mameneja wa TANESCO wa Mikoa ya Shinyanga na Geita kuhakikisha wanafanya
usanifu wa kutosha ili migodi iliyopo katika Mikoa ya Geita na
Shinyanga ikiwemo Geita Gold Mining (GGM), Bulyanhulu na STAMIGOLD
inapatiwa umeme wa uhakika pamoja na vijiji vyote vinavyopitiwa na Mradi
huo ambavyo havina Umeme na kuvipatia umeme kupitia Mradi huo bila
kuruka kijiji chochote.
Aidha, aliitaka TANESCO
kumsimamia Mkandarasi kikamilifu ili kuhakikisha Mradi unatekelezwa
katika ubora na viwango vinavyotakiwa.
Katika ziara hiyo, Kamishna
Msaidizi wa Umeme Mhandisi Innocent Luoga, aliambatana na Mhandisi wa
Mradi huo, Mhandisi Ramadhani Kidunda, Meneja wa TANESCO wa Mkoa wa
Shinyanga, Meneja wa Wilaya ya Kahama pamoja na Mkandarasi anayetekeleza
Mradi huo ambaye ni M/s CAMC Engineering Co Ltd ya China na Mhandisi
Mshauri M/s SHAKER ya Misri.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...