Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (wa pili kushoto) akikagua sehemu ya eneo litakapojengwa bwawa la kuzalisha umeme katika bonde la mto Rufiji.
Vibarua wakiendelea na shughuli mbalimbali za ujenzi kulingana na Mpangokazi wa utekelezaji wa ujenzi wa mradi wa bwawa la kuzalisha umeme .
Daraja la muda lililojengwa kurahisha usafiishaji wa vifaa na mahitaji mbalimbali katika upande wa pili wa mto katika eneo litakapojengwa bwawa la kuzalisha umeme.
Kazi ya kupasua miamba na kuondoa vifusi ikiendelea kulingana na mpangokazi wa utekelezaji wa ujenzi wa mradi wa bwawa la kuzalisha umeme.
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (aliyeshika kipaza sauti ) akizungumza na wakazi wa Kijiji cha Kisaki baada ya kusikiliza malalamiko yao mbalimbali ikiwepo fursa za upatikanaji ajira katika mradi wa JNHPP.
uonekano wa baadhi ya nyumba za wafanyakazi wanaotekeleza mradi wa JNHPP zilizokamilika kujengwa katika eneo la mradi.
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (pili kulia) akikagua ubora wa kitasa cha mlango wa moja ya nyumba za kuishi wafanyakazi zilizokamilika kujengwa katika mradi wa JNHPP.
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (katikati) akizungumza mara baada ya kutembelea daraja la muda lililojengwa katika bonde la mto Rufiji kurahisisha usafirishaji wa vifaa na mahitaji mbalimbali ng’ambo ya mto ili kutekeleza shughuli za ujenzi wa bwawa la kuzalisha umeme.
Muonekano wa mtambo wa kusaga mawe ili kupata kokoto za ukubwa wa aina tofauti kulingana na mahitaji zitakazotumika katika shughuli za ujenzi wa bwawa la kuzalisha umeme.


Na Zuena Msuya, Morogoro

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amewataka wakandarasi na wahandisi wanaotekeleza ujenzi wa Mradi Bwawa la kuzalisha umeme kwa kutumia maporomoko ya maji ya Bonde la Mto Rufiji wa Julius Nyerere (JNHPP) kuhamia na kuishi katika eneo la mradi kuanzia Januari 13,2020, baada ujenzi wa nyumba za wafanyakazi kukamilika.

Aidha aliwataka wafanyakazi wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) pamoja na wale Wahandisi washauri wa mradi (TECU) kuhamia katika eneo la mradi kuanzia mwezi ujao baada ya nyumba zao kukamilika pia.

Dkt.Kalemani alitoa agizo hilo, Januari 12, 2020, alipofanya ziara ya kumi ya kukagua maendeleo na hatua iliyofikiwa katika ujenzi wa mradi huo, tangu kusainiwa kwa mkataba na mkandarasi kuanza kufanya kazi wa mradi huo uliopo Rufiji.

Dkt. Kalemani alisema kuwa, kuanzia sasa hakuna sababu ya wafanyakazi wakandarasi wanaotekeleza mradi wa JNHPP, kuishi mbali na eneo la mradi kwa kuwa tayari ujenzi wa nyumba za wafanyakazi umekamilika.

“Hatupendi kuona wafanyakazi wa mkandarasi wanaishi Dar Es Salaam, wakati kazi inafanyika Rufiji, kuanzia kesho (Januari 13,2020) wakandarasi wote wahamie eneo la mradi, na wale wafanyakazi wa TANESCO na TECU wao watahamia kuanzia mwezi ujao baada ya nyumba zao kukamilika,” alisema Dkt.Kalemani.

Alisema tayari nyumba 8 zimekamilika zenye uwezo wa kubeba wafanyakazi 192, lengo la nyumba zinazojengwa ni kubeba zaidi ya wafanyakazi mia nne watakaokuwa wakiishi katika eneo la mradi.

Katika ziara hiyo pia, alimtaka mkandarasi wa mradi huo kuanza kupeleka mitambo tisa ya kufua umeme (Turbine) pamoja na vipuri vingine vinavyohitajika katika eneo la mradi kwa kuzingatia makubaliano ya mkataba, pia aliwataka TANESCO pamoja na TECU kuwa wazalendo katika kuhakiki ubora wa mitambo hiyo kwa manufaa ya Taifa na kuhakikisha inafika eneo la mradi kwa wakati uliopangwa.

Vilevile aliendelea kupiga marufuku wafanyakazi wageni kufanya kazi zinazoweza kufanywa na watanzania zikiwemo za vibarua, ulinzi, wauza vyakula na kadhalika na kwamba yeyote atakayekaidi maagizo hayo atachukuliwa hatua kwa mujibu wa makubaliano ya mkataba.

“Tunataka kuona walinzi ni SUMAJKT au Jeshi la Wanyapori, sitegemei kuona mlinzi kutoka nje ya Tanzania akiwa pale getini,na endapo atakuwepo basi achukuliwe hatua, nawaagiza Kamati ya ulinzi na usalama ya Mkoa simamieni hili,” alisisitiza Dkt. Kalemani.

Akizungumzia usafishaji wa eneo la mradi, Dkt. Kalemani alitoa miezi miwili kwa Wakala wa Misitu Tanzania(TFS), Shirika la Umeme Tanzania(TANESCO), TECU na wote wanaohusika katika kusafisha eneo la mradi lenye ukubwa wa kilometa 914 kuharakisha utekelezaji wa mradi huo kwa kuwa mpaka sasa kazi hiyo haijafanyika.

Aidha aliwaagiza (TFS) kuwatumia watu wenye sifa na uwezo mkubwa wa kufanya kazi hiyo kwa kasi na kiwango cha hali ya juu, hata hivyo aliwashauri kufanya mazungumzo na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) ili kutekeleza kazi hiyo kwa haraka.

Katika ziara hiyo, Dkt. Kalemani, alitembelea eneo la ujenzi wa bwawa, madaraja, mitambo ya kusaga kokoto na kuchanganya zege,na sehemu ya kujenga mitambo tisa( Turbine) ya kufua umeme.

Dkt. Kalemani alisema kuwa ameridhishwa na maendeleo ya utekelezaji ya mradi huo ambao katika kila hatua ya Mpangokazi wa utekelezaji wake umekamilika kwa asilimia 95 kwa kila kazi iliyopangwa, ambapo kwa ujumla katika hatua za awali za utekelezaji wa mradi huo umekamilika kwa asilimia 5 na kazi zinaendelea vizuri, mradi huo unatarajiwa kukamilika Juni 14, 2022.

Katika utekelezaji wa ujenzi wa mradi huo, tayari Mkandarasi alishalipwa kiasi cha shilingi Trilioni moja nukta tano ikiwa ni malipo ya awali.

Mapema akiwa njiani kuelekea eneo la mradi, Dkt. Kalemani alizungumza na wakazi wa Kijiji cha Kisaki na kuwaahidi kutatua malalamiko yao kuhusu utaratibu wa kuwapatia vijana ajira ambao wengi wao walikuwa wakiulalamikia.

Hata hivyo aliwataka vijana wanaopata kazi katika mradi huo, kufanya kazi kwa kujituma na kuzingatia mikataba ya kazi, badala ya kutoroka na kuacha kufanya kazi walizopewa.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...