Veronica Simba – Chato

Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Chato kimekiri kuridhishwa na utendaji kazi wa Waziri wa Nishati ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo hilo, Dkt Medard Kalemani.

Ameyasema hayo Katibu wa Siasa na Uenezi wa CCM, Wilaya ya Chato, Ramadhani Ndaki na kuongeza kuwa kwa utendaji kazi wake mahiri, Dkt Kalemani ameitendea haki Ilani ya Chama hicho ambacho ndicho kinaongoza nchi.

Kiongozi huyo wa Chama alikuwa akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya Waziri Kalemani kuwasha rasmi umeme katika kijiji cha Bukamila, Kata ya Kigongo, Februari 22, 2020.

“Utendaji kazi mzuri wa Dkt Kalemani umetupa matumaini sisi viongozi kuwa Ilani ya Chama inatekelezwa ipasavyo na kwakweli wakati ukifika, tutamtendea haki,” amesema Ndaki.

Akifafanua zaidi kuhusu utendaji kazi wa Dkt Kalemani, Ndaki alieleza kuwa, akiwa ni Waziri mwenye dhamana ya nishati, pamoja na mambo mengine, amefanya bidii kubwa kuhakikisha wananchi hasa walioko vijijini nchi nzima wanafikiwa na umeme.

Kwa upande wa Chato, Ndaki alieleza kuwa Dkt Kalemani amefanya makubwa katika sekta ya nishati ambapo mpaka sasa Kata zote 23 za Jimbo hilo zimekwishafikiwa na umeme.

Awali, akizungumza katika mkutano wa hadhara na wananchi wa kijiji hicho cha Bukamila, Dkt Kalemani alibainisha kuwa hadi sasa jumla ya vijiji takribani 9,000 vimekwishaunganishiwa umeme nchini kati ya 12,268 vilivyopo, sawa na asilimia 74.

Aliwahakikishia watanzania kuwa hadi kufikia Oktoba mwaka huu, jumla ya vijiji 10,446 vitakuwa vimeunganishwa na umeme na kwamba ifikapo Juni 2021, vijiji vyote vya Tanzania Bara vitakuwa vimefikiwa na nishati hiyo.

Alimpongeza na kumshukuru Rais John Magufuli kwa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya umeme nchini na akaahidi kuwa yeye na viongozi wenzake waandamizi wa Wizara, wataendelea kusimamia vyema matumizi yake kwa maendeleo ya wananchi na Taifa kwa ujumla.
 Katibu wa Siasa na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi, Wilaya ya Chato, Ramadhani Ndaki, akizungumza wakati wa hafla ya kuwasha umeme katika kijiji cha Bukamila, Chato. Mgeni Rasmi katika hafla hiyo iliyofanyika Februari 22, 2020 alikuwa ni Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (hayupo pichani).
 Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (katikati), akifurahia mara baada ya kuwasha umeme katika kijiji cha Bukamila, wilayani Chato, Februari 22, 2020.
 Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani akizungumza wakati wa hafla ya kuwasha umeme katika kijiji cha Bukamila, wilayani Chato, Februari 22, 2020.
 Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (kushoto), akiwatambulisha viongozi waandamizi kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Wakala wa Nishati Vijijini (REA), mbele ya wananchi wakati wa hafla ya kuwasha umeme katika kijiji cha Bukamila, wilayani Chato, Februari 22, 2020.
 Kazi ya kuunganisha umeme katika kijiji cha Bukamila, wilayani Chato ikiendelea. Taswira hii ilinaswa Februari 22, 2020 wakati Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (hayupo pichani), alipokuwa akiwasha rasmi umeme katika kijiji hicho.
 Baadhi ya viongozi waandamizi kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Wakala wa Nishati Vijijini (REA), wakimsikiliza Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (hayupo pichani), alipokuwa akizungumza na wananchi wakati wa hafla ya kuwasha rasmi umeme katika kijiji cha Bukamila, wilayani Chato, Februari 22, 2020.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...