Waziri wa Nishati Dkt Medard
Kalemani (wa tatu kutoka kulia) akisikiliza maelezo ya namna mtambo wa
gesi asilia uliopo eneo la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam unavyofanya kazi
wakati wa hafla ya uzinduzi wa matumizi ya gesi asilia chuoni hapo,
Februari 1, 2020.
Waziri wa Nishati Dkt Medard
Kalemani akikagua migahawa iliyounganishiwa gesi asilia iliyopo Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam pamoja na baadhi ya nyumba zilizounganishiwa
nishati hiyo katika eneo la Mwenge Mlalakuwa, Februari 1, 2020.
…………………………………………………………
Veronica Simba – Dar es Salaam
Waziri wa Nishati Dkt. Medard
Kalemani amezindua matumizi ya gesi asilia katika Chuo Kikuu cha Dar es
Salaam (UDSM), leo Februari 1, 2020 ambapo kwa hatua hiyo ya awali,
migahawa minne chuoni hapo imeanza kutumia huduma hiyo.
Akizungumza katika hafla hiyo ya
uzinduzi, Dkt Kalemani amesema dhamira ya serikali ya kutumia gesi
asilia inayopatikana nchini kwa maendeleo ya Taifa iko palepale tofauti
na wanavyoamini baadhi ya watu kuwa nishati hiyo haipewi kipaumbele
katika matumizi yake.
“Gesi hii tutaendelea kuitumia sambamba na matumizi mengine ya nishati ikiwemo kuzalisha umeme ili kujenga uchumi wa viwanda.”
Akifafanua, Waziri amesema
mathalani, takribani asilimia 80 ya gesi inayozalishwa kwa sasa hapa
nchini inatumika kuzalisha umeme na kwamba umeme unaozalishwa na gesi
asilia kwa Tanzania ni asilimia 57 sawa na megawati 892, akibainisha
kuwa huo ni mchango mkubwa sana wa sekta ya nishati kwenye uchumi wa
nchi.
Hata hivyo amesema, pamoja na
kiasi kikubwa cha gesi kutumika kuzalisha umeme, kiasi kingine
kinatumika katika shughuli nyingine mbalimbali ambazo ni pamoja na
kuunganisha viwandani, kwenye makazi ya watu na migahawa kwa ajili ya
kupikia pamoja na kutumika katika magari.
Katika kuweka msisitizo wa
matumizi ya gesi asilia katika magari, Dkt Kalemani ametoa agizo kwa
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati pamoja na watendaji wakuu wa Taasisi
zote zilizo chini yake, kuhakikisha magari yote yanayoagizwa kuanzia
sasa, yawe ni yale yenye mfumo wa kutumia gesi badala ya petroli na
dizeli.
Akizungumzia faida za kutumia gesi
asilia kwa shughuli mbalimbali, amesema ni pamoja na utunzaji wa
mazingira kutokana na uwepo wa kiasi kidogo cha hewa ya ukaa pamoja na
gharama nafuu kwa mtumiaji ambayo inakadiriwa kuokoa asilimia 40
ikilinganishwa na gharama za aina nyingine za nishati.
Kuhusu mipango ya serikali
kusambaza gesi asilia kwa matumizi ya kupikia, Waziri ameeleza kuwa,
mpango huo umeanza kutekelezwa katika mikoa ya Dar es Salaam, Lindi,
Mtwara na Pwani na baadaye mikoa mingine pia itafikiwa.
Amekipongeza Chuo Kikuu cha Dar es
Salaam kwa uamuzi wa kutumia gesi asilia na kuvitaka vyuo vingine na
taasisi za umma kuiga mfano huo.
Awali, akitoa taarifa ya
utangulizi mbele ya Waziri, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo
ya Petroli Tanzania (TPDC), Dkt. James Mataragio amesema kuwa uzalishaji
wa gesi asilia hapa nchini umefikia wastani wa futi za ujazo milioni
200 kutoka futi za ujazo milioni moja, mwaka 2004 ambapo ndipo
uzalishaji wake ulianza rasmi nchini.
Aidha, ameeleza kuwa usambazaji wa
gesi asilia unafanywa kupitia wakandarasi binafsi na pia kampuni yake
tanzu ya GASCO. “Nia yetu ni kuwafikia walaji wengi kadri iwezekanavyo.”Vilevile, ameongeza kuwa, kwa
kutumia gesi asilia, viwanda vilivyopo nchini vinapata umeme wa uhakika
tofauti na miaka ya nyuma ambapo kulikuwa na changamoto ya umeme
kukatika mara kwa mara kutokana na kutegemea chanzo cha maji ambayo
wakati wa kiangazi huadimika.
Naye Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha
Dar es Salaam, Profesa William Anangisye amesema, kwa kutumia gesi
asilia katika maeneo yote isipokuwa uzalishaji wa umeme, Chuo hicho
kitaokoa takribani shilingi milioni 479.5 kwa mwaka.
Amesema mradi huo wa kuunganisha
gesi asilia chuoni hapo umelenga kuhusisha nyumba za wafanyakazi,
migahawa, karakana, maabara za utafiti na kufundishia pamoja na jenereta
za dharura.Profesa Anangisye ameishukuru
Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Wizara ya Nishati kwa kutoa fursa ya
kupeleka mradi huo wa gesi asilia katika Chuo hicho.
Wengine walioshiriki katika hafla
hiyo ni Kamishna wa Petroli na Gesi nchini, Adam Zuberi pamoja na baadhi
ya viongozi na wafanyakazi wa Wizara ya Nishati pamoja na TPDC.Sanjari na tukio hilo la uzinduzi
wa matumizi ya gesi asilia UDSM, Waziri pia amekagua baadhi ya makazi
ambayo yalikwishaunganishiwa nishati hiyo katika maeneo ya Mwenge
Mlalakuwa na Mikocheni.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...