Na Asteria Muhozya, Nzega
SERIKALI imesema Ushuru wowote unaotolewa kwenye Maeneo ya Migodi Nchini ni lazima uthibitishwe na Maafisa Madini walioko kwenye maeneo husika.
Tamko hilo lilitolewa Mei 24, 2020 na Waziri wa Madini Doto Biteko wakati akizungumza na Wachimbaji Wadogo wa Madini ya Dhahabu eneo la Lusu Wilayani Nzega Mkoa wa Tabora alipotembelea eneo hilo kuangalia shughuli za uchimbaji madini.
Aidha, tamko hilo linafuatia kuwepo kwa malalamiko toka kwa wachimbaji wanaofanyakazi kwenye Leseni za baadhi ya Wachimbaji ambao walimlalamikia Waziri Biteko kutozwa kodi na wenye leseni hizo na hivyo kuomba ufafanuzi juu ya suala hilo.
Waziri Biteko alisisitiza kwa kuwataka Maafisa hao kuhakikisha Ushuru unaotolewa ni ule tu uliopo Kisheria na kuhakikisha wanasimamia jambo hilo.
Akifafanua kuhusu suala la mrabaha wa mawe unaotozwa na Serikali alieleza kuwa, wachimbaji wasio rasmi wanalazimika kulipia mrabaha wa mawe isipokuwa wenye Leseni wanatakiwa kulipia mrabaha wa dhahabu baada ya kukamilisha hatua zote.
" Wale msio rasmi mjue mkigawana mawe na Serikali itakuwepo mnagawana nayo isipokuwa mwenye Leseni yeye tutamwomba mrabaha wetu mwishoni. Ukitaka kulipa mrabaha mara moja chimba kwenye Leseni, mkichimba bila utaratibu tutagawana kwenye mawe na kwingine," alisisitiza Waziri Biteko.
Pia, aliendelea kuwasisitiza wachimbaji nchini kuyatumia Masoko ya Madini yaliyoanzishwa katika maeneo mbalimbali kufanya biashara ya madini.
Akijibu ombi la wachimbaji hao kupelekewa Wataalam wa masuala ya Utafiti ili kuwawezesha kujua mwelekeo wa miamba na hivyo kuchimba kwa tija, alisema Wizara itaangalia namna ya kufikisha Mtambo wa Kuchoronga katika eneo hilo baada ya Shirika la Madini la Taifa ( STAMICO) kukamilisha kazi za kandarasi za uchorongaji zinazoendelea katika maeneo mengine.
Katika hatua nyingine, alipongeza wachimbaji kwa kulipa mrabaha wa Serikali na hivyo kuwezesha makusanyo ya shilingi Bilioni 2.7 hadi kufikia Aprili 30, sawa na asilimia 122 na hivyo kuvuka lengo la makusanyo ya shilingi bilioni 2.2 zilizopangwa kukusanywa Mwaka wa fedha 2019/2020.
Aidha, aliongeza kuwa, baada ya serikali kutoa eneo hilo kwa wachimbaji wadogo, kwa kipindi cha kuanzia mwezi Desemba hadi sasa madini ya dhahabu ya thamani ya shilingi Bilioni 3 na Milioni 500 yalizalishwa katika eneo hilo la Lusu.
" Watanzania changamkieni Rasilimali hii Ni zenu, chapeni kazi mlipe Kodi," amesema Biteko.
Aidha, alimpongeza Mkuu wa Wilaya hiyo Godfrey Ngupula kwa kusimamia vizuri Sekta ya Madini na kuwa karibu na wachimbaji wadogo.
Awali, katika eneo la Chuo Cha Madini Tawi la Nzega, Mkuu wa Wilaya hiyo Godfrey Ngupula alimweleza Waziri kuwas shughuli ya uchukuaji mchanga wa Dhahabu ulioachwa na Kampuni ya Resolute unaofanywa na Kampuni ya Ashery Construction & Matinje unaendelea vizuri na kuongeza kwamba ifikapo Juni 1 wakati Chuo kitakapofunguliwa zoezi hilo litakuwa limekamilika ns kuongeza kwamba eneo lililotumika linatarajiwa kutengenezwa ujwanj wa mprira.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Wilaya ya Nzega Amos Kanunda ameipongeza Serikali kwa kutoa maeneo 10 kwa ajili ya wachimbaji wadogo Wilayani humo na kusema hivi sasa wachimbaji wanachimba na kuwahimiza kulipa kodi za serikali huku akisisitiza suala la wataalam wa Utafiti ili kuwawezesha wachimbaji kuchimba kwa tija na Serikali inufaike kwa mapato.
Naye, Mwenyekiti wa Wachimbaji Mkoa wa Tabora (TABOREMA) Joseph Mabondo amesisitiza suala la Watalaam wa kupima mwelekeo wa miamba kuwawezesha wachimbaji kuchimba bila kubahatisha. Pia ameipongeza Serikali kuwapatia wachimbaji Mkoani humo maeneo ya kuchimba
Baadhi ya Wachimbaji madini.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...