Benki ya NMB imekuwa benki bora nchini Tanzania kwa mara ya nane mfululizo baada ya kuzibwaga benki zingine 40 nchini.

Tuzo hiyo imetolewa na Euromoney, ambalo ni jarida la kimataifa la masuala ya kifedha linaloongoza duniani lenye makao makuu yake jijini London, Uingereza.

Tuzo hii inaonesha kuwa Benki ya NMB ni zaidi ya taasisi inayotoa huduma za kifedha na kuwa kichocheo muhimu cha mabadiliko ya kiuchumi kupitia utoaji huduma za kibenki kwa njia ya kidigitali.

Akiongea wakati wa kukabidhiwa tuzo hiyo, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Benki ya NMB – Dk. Edwin Mhede alisema baada ya Tanzania kufikia uchumi wa kati, Benki ya NMB inaahidi kuendelea kutoa ushirikiano wa karibu ili kuchangia zaidi katika ukuaji wa uchumi kwenda katika hatua ya juu zaidi.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NMB - Ruth Zaipuna alisema: “Leo hii tunajulikana kama benki imara zaidi, yenye huduma za ubunifu wa kiteknolojia. Tumedhamiria kuwa zaidi ya taasisi ya huduma ya fedha kwa kuendelea kuchochea mabadiliko ya kiuchumi katika nchi yetu na kuboresha maisha ya Watanzania wenzetu kwa kutoa huduma zinazowafaa na kukidhi mahitaji na mipango yao.”

Tuzo hiyo hutolewa kwa kuzingatia vigezo kadhaa kwa benki zilizopendekezwa ukiwamo ufanisi wa hesabu za fedha na utendaji kwa ujumla, mkakati wa huduma za kidijitali, huduma jumuishi za fedha, usalama wa huduma za kimtandao na wajibu wa benki kwa jamii inayoihudumia. Vigezo vingine vilivyotumika ni mtaji wa benki, mapato yatokanayo na biashara ya hisa, mapato yatokanayo na mali za kampuni, pato litokanalo na riba, uwiano wa fedha na gharama za uendeshaji, kiwango cha amana za wateja, Kiwango cha Mikopo katika soko, Uwiano kati ya mikopo na amana za wateja, uwiano wa mikopo chechefu, uwiano wa hasara itokanayo na mikopo chechefu.

Akizungumzia mchakato wa kumpata mshindi wa tuzo ya benki bora nchini, mhariri wa Jarida la Euromoney, Clive Horwood alisema: “Tunaendelea kuzitambua taasisi bora zaidi katika kila nchi zinazotoa huduma za fedha. Kwa kila mwaka, ukubwa ni muhimu lakini sio kigezo muhimu zaidi. Faida ya benki husika ni muhimu kama ilivyo uwezo wa kuthibitisha uwezo wa kukua, ufanisi wa kiutendaji ikilinganishwa na washindani wake sokoni na uwezo wa kukabili mazingira ya soko yanayobadilika pamoja na kukidhi mahitaji ya wateja.”
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya NMB Dk.Edwin P. Mhede, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NMB- Ruth Zaipuna na Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB – Filbert Mponzi wakiifurahia Tuzo walioipokea kwa kuwa Benki Bora Tanzania.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya NMB Dk. Edwin P. Mhede, akikabidhiwa Tuzo ya Benki Bora na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NMB- Ruth Zaipuna. Akishuhudia ni Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB – Filbert Mponzi.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya NMB Dk. Edwin P. Mhede (Katikati) akizungumza mbele ya Waandishi wa Habari (hawapo pichani),kuhusu Benki ya NMB kuwa benki bora nchini Tanzania kwa mara ya nane mfululizo baada ya kuzibwaga benki zingine 40 nchini,kushoto ni  Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NMB- Ruth Zaipuna na kulia ni Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB – Filbert Mponzi.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NMB - Ruth Zaipuna alisema akizungumza mbele ya Waandishi wa Habari (hawapo pichani) wakati akitoa taarifa ya  Benki ya NMB kuwa benki bora nchini Tanzania kwa mara ya nane mfululizo baada ya kuzibwaga benki zingine 40 nchini,katikati ni Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya NMB Dk. Edwin P. Mhede pamoja na Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB – Filbert Mponzi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...