Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania(TIC), Geoffrey Mwambe amesema kuwa Miundombinu iliyojengwa na Serikali imewezesha kituo hicho kupiga hatua kubwa na kulete wawekezaji wengi katika Sekta ya uwekezaji hasa kwenye sekta ya Viwanda.



Akizungumza katika mkutano na Waandishi wa Habari Jijini Dar es Salaam, Mwambe amesema miundombinu iliyojengwa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt.John Pombe Magufuli kwa kipindi hiki cha miaka mitano imekuwa ni mishipa ya kituo hicho kufanikisha sekta hiyo muhimu nchini.



“Miundombinu iliyojengwa na Serikali kwenye hii miaka mitano sisi kwetu kama kituo cha uwekezaji inatumika kama mishipa ya damu, kwani inapunguza gharama ya usafirishaji, kwa hiyo imetusaidia  ndani ya miaka hii mitano ya Rais Magufuli tokea Juni 2016 hadi Juni 2020 tumeweza kusajili miradi 1, 312 yenye thamani ya dola za Kimarekani Bilioni 20”, Alisema Mwambe.



Alibainisha kuwa asilimia 54 ya miradi hiyo ipo sekta ya viwanda ambayo imeisaidia Tanzania kuingia uchumi wa kati na katika uwekezaji wa miradi yote asilimia 28 ni uwekezaji wa wazawa, asilimia 43 wageni na asilimia 29 ni uwekezaji  wa mashirikiano kati ya wazawa na wageni.



Mwambe alisema kuwa katika utekelezaji wa kuimarisha uwekezaji TIC wameanzisha ofisi zingine kikanda kusogeza huduma kwa wawekezaji kwenye maeneo mbalimbali ya uwekezaji ikiwemo kanda ya Magharibi ikijumulisha mikoa ya Kigoma, Katavi na Tabora.



Aliongeza kuwa kanda zingine ni zile za Pwani kwa Mikoa ya Dar es Salaam na Pwani, lakini pia kanda ya kati yenye mikoa ya Morogoro, Singida na Dodoma na kanda ya ziwa yenye mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Mara na  Kagera  na kanda zingine ambako kila huduma kwa wawekezaji zinapatikana kwa urahisi.



Aidha, Mwambe alieleza mageuzi makubwa ambayo TIC wamefanya kwa miaka mitano ya Serikali ya Awamu ya Tano Ikiwemo kuimarisha mifumo ya huduma kwa wawekezaji kama vile Mfumo wa utoaji wa cheti cha uwekezaji kwa njia ya kieletroniki, Mfumo wa Usajili wa makampuni na Mfumo wa Ulipaji Serikalini (MUSE).



Mwambe alisema kuwa sekta ya uwekezaji katika viwanda ni kubwa kuliko sekta yeyote ile kwa hiyo Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Rais Dkt.John Pombe Magufuli inatekeleza kwa vitendo Sera ya Uchumi wa kati wenye Viwanda ambapo Julai 1, 2020 Tanzania ilitangazwa rasmi kuwa moja ya nchi yenye uchumi  wa kati duniani.



“Tumefanikisha kwa kiasi kikubwa sana kwenye uwekezaji wa viwanda, na hii inatupa faraja sana kuwa Serikali inatekeleza na kusimamia Sera yake ya uchumi wa Viwanda, lakini pia tafsiri ya viwanda imeweza kuendana na uchakataji wa mazao yetu kwenye maeneo mbalimbali nchini”, Alisema Mwambe.
 Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania(TIC), Geoffrey Mwambe akionesha moja ya jarida linalochapishwa na kituo hicho,likieleza taarifa mbalimbali kuhusu mambo ya uwekezaji,mbele ya Waandishi wa Habari leo jijini Dar.Picha zote na Michuzi JR-MICHUZI MEDIA.

 Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania(TIC), Geoffrey Mwambe akizungumza mbele ya Waandishi habari leo jijini Dar,alipokuwa akitoa taarifa ya mafanikio ya kituo hicho cha TIC katika kipindi cha miaka mitano ya Serikali ya awamu ya Tano
 Baadhi ya Waandishi wa Habari na Viongozi waandamizi wa Kituo hicho wakimsikiliza  Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Geoffrey Mwambe alipokuwa akifafanua mambo mbalimbali ikiwemo mafaniko ya kituo hicho kwa miaka mitano ya Rais Dkt John Pombe Magufuli.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...