Meneja Mahusiano na Mawasiliano wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Titus Kaguo akizungumza na wandishi wa habari jijini Dodoma leo wakati akitoa taarifa ya hali ya mafuta nchini.
Charles James, Michuzi TV
MAMLAKA ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA) imewataka watanzania kuondoa hofu ya kukosa mafuta kwani tangu Julai 29 mwaka huu hadi Agosti 31 kuna jumla ya Meli sita za Petroli zinategemewa kuingia.
Sanjari na hilo EWURA imetangaza kupanda kwa bei za mafuta nchini ambazo zitaanza kutumika rasmi kesho Agosti 5.
Jijini Dar es Salaam bei ya Petroli imepanda kutoka Sh 1693 hadi 1832, Tanga imepanda kutoka Sh 1654 hadi 1868, Mtwara Sh 1612 hadi 1875 wakati kwenye Dizeli Mkoa wa Tanga yamepanda kutoka Sh 1693 hadi 1778 na Mtwara yakitoka Sh 1731 hadi 1799.
Imeelezwa kuwa licha ya kupanda kwa bei hizo tayari meli tatu kati ya sita zinazotarajiwa kuingia zimeshaingia zikiwa na jumla ya Lita Milioni 89.5 kwa ajili ya soko la ndani na zitatosheleza matumizi ya siku 18.
Meli nyingine tatu zitawasili kati ya Agosti 17 hadi 31 zikiwa na takribani Lita Milioni 100 ambazo zitatosheleza mahitaji ya Nchi kwa muda wa siku 22.
Akizungumza na Wandishi wa Habari jijini Dodoma, Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa Mamlaka hiyo, Titus Kaguo amesema mafuta ya dizeli yapo ya kutosha na Meli tatu za mafuta hayo zenye jumla ya lita milioni 193.391 zinategemewa kuingia nchini Agosti mwaka huu.
Kaguo amesema,kiasi hicho cha mafuta hayo yatatosheleza mahitaji kwa zaidi ya siku 30 na ili kuwa na utoshelevu wa mafuta nchini, kuanzia Septemba mwaka huu, EWURA imeongeza makadirio ya matumizi ya mafuta kwa siku kuwa lita milioni 4.812 kwa petroli na lita milioni 6.082 kwa dizeli.
Akitoa ufafanuzi juu ya changamoto ya upatikanaji wa mafuta nchini kuanzia mwishoni wa Julai, Kaguo amesema, jambo hilo limechangiwa na kuchelewa kwa meli moja iliyokuwa ifike nchini kati ya Julai 22 na 24 na badala yake iliingia nchini Julai 29.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...