Yaahidi kuendelea kudhamni Ligi Kuu ya Taifa 

Tarehe 7 August 2020, Kampuni ya kidigitali na teknolojia ya mawasiliano ya simu inayoongoza Tanzania na mdhamini mkuu wa Ligi Kuu, Vodacom Tanzania leo imewapa tuzo washindi wa Ligi Kuu ya Tanzania kwa msimu wa mwaka 2019/2020.

Akiongea katika hafla iliyofanyika jijini Dar es salaam, Waziri wa Nchi – Ofisi ya Rais, Tawala za mikoa na Serikali za mitaa (TAMISEMI), Mh. Suleiman Jaffo, ameipongeza kampuni ya Vodacom kwa jitihada zao za kusaidia maendeleo ya mpira wa miguu Tanzania kwa miaka mingi.

“Udhamini wa Ligi Kuu ya Taifa unaotekelezwa na kampuni ya Vodacom Tanzania umeweza kukuza vipaji na medani ya mpira nchini. Wito wagu kwa wadhamini wa mpira nikuwekeza katika ngazi za kati na chini ili kuinua mpira kuanzia ngazi za chini”.

Mkurugenzi wa Kitengo cha masuala ya biashara wa Vodacom Tanzania, Linda Riwa amewapongeza washindi wote kutoka katika makundi mbalimbali na kuwahakikishia kwamba Vodacom Tanzania itaendelea kusaidia kukuza kiwango cha mpira wa miguu Tanzania.

“Kama mnavyofahamu kwamba kampuni ya Vodacom Tanzania imeingia mkataba na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ambapo TFF watapokea kiasi cha TZS Bilioni 9 katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2019 – 2020.

Tunaendelea kusaidia maendeleo ya mpira wa miguu Tanzania kwa kulea vipaji na kukuza sekta nzima ya mpira wa miguu jambo ambalo litanufaisha vilabu vya mpira wa miguu, wachezaji, marefa, washika vibendera, makocha, wasambazaji, wakandarasi na kutoa ajira.

Ninawahakikishia tena utayari wa kampuni ya Vodacom Tanzania katika kusaidia maendeleo ya mpira wa miguu na sekta nzima inayozungukia mpira wa miguu Tanzania kwa kudhamini Ligi Kuu. Pia tunatazamia kushuhudia msimu bora zaidi wa Ligi Kuu katika siku zijazo”. Alihitimisha Linda.

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Wallace Karia amesema, “Kiwango cha mpira wa miguu nchini kimekua kufikia kiwango kinachoshuhudiwa sasa ambapo wachezaji wengi wa timu ya taifa wanacheza katika vilabu mbalimbali vya kimataifa, Jambo hili linadhihirisha juhudi za wapenzi wa mpira na wadau wa mpira wa miguu kama vile Kampuni ya Vodacom Tanzania ambao wamefanikisha jambo hili.” 

Mchezaji bora wa mwaka ambaye alikuwa ni Clatous Chama wa klabu ya Simba Sc amesema anafuraha sana kuchaguliwa kuwa miongoni mwa wachezaji bora wa mpira wa miguu nchini na kutoa wito kwa mashirika mengine kusaidia katika kukuza mpira wa miguu Tanzania.

“Nimefurahi kuchaguliwa miongoni mwa wachezaji bora wa msimu huu. Ninawashukuru wadau wote wa mpira wa miguu ikiwemo Vodacom Tanzania ambao wanasaidia mpira wa miguu Tanzania na kuchangia katika kukuza viwango na vipaji vya wachezaji chipukizi.”

Tuzo ya timu bora ilinyakuliwa na Simba SC, kocha bora wa msimu ilikwenda kwa Sven Vanden broek wa Simba SC, beki bora ilikwenda kwa Nico Wadada, kiungo bora ilikwenda kwa Cleutous Chama ambaye alishinda tuzo ya mchezaji bora wa ligi pia. Patson Shikala wa Mbeya City alishinda goli bora, tuzo ya mchezaji bora chipukizi ilikwenda kwa Novatus Dismas wa Biashara United FC na tuzo ya kipa bora ilinyakuliwa na Aishi Manula wa Simba SC.

Tuzo ya timu yenye nidhamu ilichukuliwa na Kagera Sugar FC wakati tuzo ya mwamuzi bora ilichukuliwa na Ramadhan Kayoko wa Dar es salaam na tuzo ya mwamuzi bora msaidizi ilichukuliwa na Frank Komba wa Dar es salaam na mwisho Tuzo ya Mafanikio kwenye maisha (Lifetime Achievement) ilikwenda kwa mchezaji wa zamani wa vilabu vya Pan African, Yanga na timu ya Taifa mzee Sunday Manara.

Jumla ya thamani za tuzo hizi ni zaidi ya TZS 263,000,000.00
Waziri wa TAMISEMI, Mhe. Selemani Jafo (wa pili kushoto) akimkabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya shilingi milioni 30 mwakilishi wa timu ya Azam Popat baada kushika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi kuu ya Vodacom Tanzania (VPL).Wengine ni Mkurugenzi wa biashara Vodacom Tanzania PLC Linda Riwa (kushoto) ambao ndio wadhamini wakuu wa ligi hiyo, na Raisi wa TFF, Wallace Karia. Hafla za tuzo za Vodacom zilifanyika jijini Dar Es Salaam.
Waziri wa TAMISEMI, Mhe. Selemani Jafo (wa pili kushoto) akimkabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya shilingi milioni 45 kwa Kaimu Katibu Mkuu wa Yanga, Patrick Simon baada kushika nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi kuu ya Vodacom Tanzania (VPL). Wengine ni Mkurugenzi wa biashara Vodacom Tanzania PLC Linda Riwa (kushoto) ambao ndio wadhamini wakuu wa ligi hiyo, na Raisi wa TFF, Wallace Karia. Hafla za tuzo hizo zilifanyika jijini Dar Es Salaam
    
Waziri wa TAMISEMI, Mhe. Selemani Jafo akizungumza na wageni waalikwa kwenye Tuzo za Vodacom Premier League VPL
 
 Waziri wa TAMISEMI, Mhe. Selemani Jafo (wa tatu kushoto) akikabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya shilingi milioni 100 kwa kiongozi wa Simba, Mwina Kaduguda (wa tatu kulia)  baada ya kushika nafasi ya kwanza  kwenye msimamo wa ligi kuu ya Vodacom Tanzania (VPL). Wengine ni Mkurugenzi wa biashara Vodacom Tanzania PLC Linda Riwa (kushoto) ambao ndio wadhamini wakuu wa ligi hiyo, na Rais wa TFF, Wallace Karia (wa pili kulia), Nassoro Try Again (wa pili kushoto) na Haji Manara. Hafla za tuzo za Vodacom zilifanyika jijini Dar Es Salaam.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...