• Kayanga ni miongoni mwa mji 28 iliyonufaika na sh. tril. 1.2 za miradi hiyo

 

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Kassim Majaliwa amesema Serikali imetekeleza miradi ya maji 1,423 ikiwemo mradi wa kupeleka maji kwenye miji 28 unaotekelezwa kwa sh. trilioni 1.2.

 

“Kayanga imepata sh. bilioni 58, ni miongoni mwa miji 28 iliyopata fedha za mradi wa maji kitaifa ambao unajumuisha mikoa mingi,” amesema.

 

Ametoa kauli hiyo leo (Jumanne, Septemba 29, 2020) wakati akizungumza na wakazi wa kata ya Kayanga, katika mikutano uliofanyika kwenye uwanja wa Changarawe, wilayani Karagwe, mkoani Kagera.

 

Mikoa inayohusika na mradi huo miji yake kwenye mabano ni Tanga (Handeni/Korogwe, Muheza na Pangani); Njombe (Njombe, Wanging’ombe na Makambako); Kagera (Kayanga); Mtwara (Nanyumbu na Makonde); Singida (Manyoni); Ruvuma (Songea); Tabora (Sikonge, Urambo-Kaliua); Mbeya (Rujewa na Chunya); Kigoma (Kasulu); Lindi (Kilwa Masoko); Mara (Mugumu, Rorya/Tarime); Geita (Geita na Chato); Singida (Singida Mjini na Kiomboi); Katavi (Mpanda); Dodoma (Chamwino na Chemba); Iringa (Mafinga); na Morogoro (Ifakara).


Aidha, Mheshimiwa Majaliwa amewataka watanzania wamchague Dkt. John Pombe Magufuli kwa sababu anatoka katika chama ambacho kina mikakati inayotokana na mawazo ya wananchi.

 

"Dkt. Magufuli anatoka kwenye Chama ambacho kina utaratibu katika kuendesha nchi, chama ambacho kinaratibu kero za wananchi, ambacho kinasikiliza wananchi mpaka ngazi ya chini," amesema.

 

Ametoa wito huo leo (Jumanne, Septemba 29, 2020) wakati akizungumza na wakazi wa kata ya Nkwenda, akiwa njiani kuelekea Isingiro wilayani Kyerwa, mkoani Kagera.

 

"Tumemjaribu na amefanya mambo makubwa katika wizara alizoziongoza na ndiyo maana namleta kwenu Dkt. Magufuli na kumuombea miaka mingine mitano ili alete maendeleo zaidi."

 

Mheshimiwa Majaliwa ambaye yuko mkoani Kagera kumuombea kura mgombea Urais kwa tiketi ya CCM, Dkt. Magufuli alitumia fursa hiyo kumnadi mgombea ubunge wa jimbo la Kyerwa, Bw. Innocent Bilakwate, mgombea udiwani wa kata ya Nkwenda, Bw. Edward Katunzi na wagombea wa CCM wa kata za jirani.

 

Amesema CCM ni chama kinachoongozwa na Ilani ya Uchaguzi na kuna mambo yamethibitika katika ilani inayoishia 2020. "Leo tunaleta kitabu kingine cha Ilani ya 2020 - 2025. Kama tuliweza kufanya makubwa ndani ya miaka mitano na kile kitabu kidogo, je huko tuendako itakuwaje?"

 

Akiwa Isingiro kwenye mkutano wa hadhara, Mheshimiwa Majaliwa alisema Serikali ilibadilisha sheria tangu mwaka 2017 na ikazuia uuzaji wa madini ya bati nje ya nchi kwa kutumia njia za panya.

 

"Sheria inatutaka tutenge ekari kadhaa kwa ajili ya wachimbaji wadogo. Leo hii ekari 38,000 zimetolewa kwa wachimbaji wadogo wa madini mbalimbali. Pia tumeanzisha masoko ya madini 26 na vituo vidogo 28 vya kuuzia madini," alisema.

 

Akifafanua kuhusu vitambulisho vya Taifa, Mheshimiwa Majaliwa alisema Tanzania ni nchi ya amani na wengi wanatamani kuja kuishi nchini.

 

Alisema wilaya za Kyerwa, Karagwe na Missenyi ni za mipakani kwa hiyo zina changamoto za uhamijai na masuala ya kiraia. "Ndiyo maana Serikali  inakuwa makini katika uhakiki. Tutaimarisha usimamizi ili kila Mtanzania  apate kitambulisho.”

 

Pia amewaonya maafisa wanaohusika na utaoaji vitambulisho vya uraia ambao wanapokea hongo na kuwapa vitambulisho hivyo watu wasiostahili.

 

Wakati huohuo, Mheshimiwa Majaliwa amempokea aliyekuwa mgombea ubunge wa jimbo la Karagwe kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Bw. Princepius Rwazo ambaye ameamua kurejea CCM. 

 

Akizungumza kwenye mkutano huo, Bw. Rwazo alisema alikuwa mgombea ubunge kwenye uchaguzi mkuu uliopita na aliisumbua sana CCM lakini sasa ameamua kurejea kwani ameona mazuri yanayofanywa na Chama hicho.

 

"CCM imejibu kiu zetu, kimekuwa kama chama cha upinzani, na wapinzani sasa wamelala. Nimerudi CCM, sihitaji cheo chochote, shida yangu ni kujiunga na watu wanaochapa kazi. Nitamuunga mkono Dkt. Magufuli na ndugu yangu Bashungwa," alisema na kushangiliwa.

 

Mheshimiwa Majaliwa anaendelea za ziara yake katika wilaya za Karagwe na Missenyi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...