Na Mwandishi Wetu, Singida
MKUU wa Mkoa wa Singida, Dkt. Rehema Nchimbi amesema jamii ina kila sababu ya kuwatunza, kuwaenzi na kuwahudumia Wazee ikiwa ni sehemu ya kutambua mchango wao katika Ustawi wa Jamii.
DKt. Nchimbi ameyasema hayo katika makao ya Wazee Wasiojiweza Sukamahela, Wilayani Manyoni Mkoani Singida alipokwenda kuwasalimia wazee hao ikiwa ni siku chache kabla ya maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wazee ambayo huadhimishwa kila ifikapo tarehe Mosi ya mwezi Oktoba.
Akiwa katika makazi hayo Dkt. Nchimbi ameitaka jamii kuhakikisha inawajali na kuwahudumia Wazee muda wote kwa kuzingatia mchango mkubwa walioutoa kwa nyakati tofauti wakati wangali na uwezo wa kuzalisha mali.
“Hawa tunaowaona sasa hivi wazee, ndio waliotuzaa wakiwa vijana na wangali katika umri wa kuzaa, Wazee ni neema na baraka na siyo laana” amesema.
Ameongeza kuwa Serikali kwa upande wake imeweka utaratibu na sera nzuri za kumlinda kila mtu katika hatua mbalimbali za maisha hata wakati wa uzee na hasa kwa wazee wasio na ndugu na jamaa kwa kuwatunza na kuwaangalia.
Amewataka Watanzania kuzingatia Kanuni za kupata watoto na kuwatunza vema ili baadaye wawe wazee wenye busara na hekima, kwani jamii isiyowaandaa watoto wake ipasavyo, haiwezi kuwa na Wazee kama hao.
Ameongeza kuwa vizazi vya sasa wakiwemo wanafunzi wanatakiwa kuhimizwa kuwatembelea na kuwasilikiza Wazee wasiojiweza ili wapate uhalisia na uzoefu kutoka kwa wazee wenyewe.
“Tunaposema tumvushe salama tunalenga katika kuboresha afya ya mama na mtoto ili tuweze kupata kizazi salama na hatimaye kuwa na wazee ambao tutawatunza na watafurahia uzee wao” alifafanua.
Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii. Dkt. John Jingu, Kamishna wa Ustawi wa Jamii, Dkt. Naftali Ng’ondi amesema Serikali kupitia Wizara hiyo inawahudumia wazee 281 katika Makao mbalimbali nchini.
Dkt. Ng’ondi amefafanua kuwa pamoja na huduma mbalimbali kwa Wazee, Serikali imeboresha miundombinu ikiwa ni pamoja na kukarabati makazi ya Wazee na kujenga Ofisi ya Utawala.
Akiwa katika makazi ya Wazee Sukamahela, Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Nchimbi amekabidhi zawadi ya vyakula mbalimbali zikiwemo kilo 100 za mchele, mafuta ya kupikia, vifaa kwa ajili ya usafi, mbuzi mmoja pamoja na sabuni za unga.
Akitoa Shukrani kwa niaba ya Wazee, Mwenyekiti wa Umoja wa Wazee Sukamahela, Andrea Yohana ameishukuru serikali kwa msaada wa chakula na matunzo yanayotolewa kwao
“Tunamshukuru Rais Jonn Magufuli na nyie viongozi wetu kuja kututembelea na kutuletea msaada, Mwenyezi Mungu awabariki na kuwaongezea pale mlipotoa kiongezeke, mzidi kutupatia msaada Zaidi” Amesema Mzee Andrea
Siku ya Wazee ya Kimataifa Mwaka 2020 inatarajiwa kufanyika katika ngazi ya mikoa na inaongozwa na Kaulimbiu isemayo“FAMILIA NA JAMII TUWAJIBIKE KUWATUNZA WAZEE.”
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...