Rais mstaafu wa Burundi na kiongozi wa ujumbe wa uangalizi wa uchaguzi kutoka EAC Sylvestre Ntibantunganya akipeperusha bendera ya Jumuiya hiyo kuashiria amani na mafanikio kwa Tanzania kuelekea uchaguzi mkuu, leo jijini Dar es Salaam.
Na Leandra Gabriel, Michuzi TV
UJUMBE wa uangalizi wa uchaguzi Mkuu kutoka Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) unaoangazia uchaguzi mkuu wa Tanzania unaotarajiwa kufanyika Jumatano ya Oktoba 28 mwaka huu umeridhishwa na hali ya amani katika kuelekea uchaguzi huo huku jumuiya hiyo ikijivunia amani pamoja na ukuaji wa uchumi, siasa na maendeleo ya kijamii.
Akizungumza leo jijini Dar es Salaam Rais mstaafu wa Burundi, Slyvestre Ntibantunganya ambaye ni kiongozi wa ujumbe huo wa uangalizi amesema kuwa, Ujumbe huo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ni mwitikio wa mwaliko uliotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi ya Tanzania (NEC.) Pia ni uamuzi wa baraza la mawaziri la maamuzi ya EAC kuhusu uchunguzi wa chaguzi katika nchi washirika.
Amesema kuwa ujumbe huo utaangalia mazingira ya jumla ya uchaguzi kwa kuhusisha shughuli za kabla ya uchaguzi, siku ya kupiga kura, kuhesabu kura na utangazaji wa matokeo.
Ameeleza kuwa timu hiyo ya uangalizi itatembelea katika Mikoa mbalimbali ikiwemo Dar es Salaam, Morogoro, Mwanza na Kilimanjaro na kuangalia namna mchakato huo unavyoendeshwa na hiyo ni pamoja na kuwahimiza wapiga kura na wadau mbalimbali kushiriki mchakato huo pamoja na kubaini changamoto ambazo watazitolea ufafanuzi baadaye.
Aidha amesema kuwa kupitia uchaguzi huo nchi wanachama watapata nafasi ya kubadilishana uzoefu katika kuendelea kudumisha Demokrasia pamoja na kushirikiana katika masuala ya uchaguzi.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...