MGOMBEA wa Ubunge katika jimbo la Kibamba kupitia Chama cha 'Tanzania Labour Party (TLP),Mhandisi Aivan Maganza amemzawaidia ng'ombe mgombea wa Urais kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM) John Magufuli kutoka na utendaji wake mzuri ulioliwezesha taifa kupiga hatua kimaendeleo.

Aidha Maganza ambaye pia ni Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa chama hicho, amemtabiria ushindi unono Rais Magufuli katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika jumatano ya wiki hii kutokana na kukubalika na watanzania wengi.

Akizungumza katika mkutano wake na waandishi wa habari Makao Makuu ya Chama hicho yaliyopo Magomeni jijini Dar es Salaam jana, Maganza alisema kama ilivyokuwa kwa Mwenyekiti wa TLP Augustino Mrema aliyemkabidhi Rais Magufuli zawadi ya mbuzi, yeye pia ameguswa na utendaji wa Kiongozi huyo.

"Tayari zawadi ya Ng'ombe huyo ipo Dodoma ambapo ni nyumbani kwetu, namsubiri amalize ratiba zake za kampeni ili niweze kumkabidhi kama shukrani na pongezi kwa alicholifanyia Taifa hili" alisema Maganza.

Alisema utendaji wa Kiongozi huyo mkuu wa taifa hili haufananishwi kwa vyovyote na  wengine kutokana na mambo mengi mazuri aliyoyafanya katika taifa hili ndani ya kipindi cha miaka mitano cha awamu yake ya kwanza madarakani.

Pamoja na hilo Maganza pia alisema kitendo cha Rais Magufuli kuliwezesha taifa kufikia uchumi wa kati kabla ya muda uliotarajiwa, kinazidi kupaisha sifa zake katika utendaji, jambo lililowafanya watanzania wengi kujenga imani naye.

Aidha akizungumzia mwenendo wa jimbo lake katika mchakato huu wa uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika keshokutwa, Maganza alisema ana imani kuwa atashinda kiti hicho kutokana na mikakati yake mizuri aliyoitoa kwa wananchi hao.

" Ukweli kwa sasa wananchi wanasubiri siku ya keshokutwa ili kufanya maamuzi ila kitu kitu kipo sawa hadi hivi sasa, nina imani kubwa kuwa wananchi wa jimbo langu la Kibamba hawatoniangusha" alisema Maganza.

Aidha aliwaomba wananchi kujitokeza kwa weingi na kutumia nafasi yao ya kikatiba kupiga kura na kuwachagua viongozi mbalimbali kwa kuwa hiyo ndiyo fursa pekee ya wao kupata maendeleo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...