………………………………………………………………………….
NA MWAMVUA MWINYI
BENKI ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) imekikabidhi kikundi cha wakulima wa mboga mboga cha wanawake cha Faraja Women Group hundi ya shilingi milioni nne kwa ajili ya kununua mashine ya kumwagilia ili kuwa na kilimo cha faida na siyo cha kujikimu.
Akikabidhi hundi hiyo kwa kikundi hicho ambacho kiko ndani ya Chama Cha Ushirika wa Umwagiliaji Cha Ruvu (CHAURU) kilichopo Halmashauri ya Chalinze wilayani Bagamoyo mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo alisema kuwa mashine hiyo itawafanya wanachama hao kuwa na kilimo cha uhakika.
Ndikilo alisema kuwa ili wakulima hao wa mboga mboga kuwa na kilimo cha faida na siyo cha kujikimu kwani  mbali ya kufanya biashara pia wataweza kutumia kilimo hicho kama lishe kwa familia na ziada watauza.
“Wanawake ndiyo wakulima wakuu ikilinganishwa na wanaume hivyo wana nafasi kubwa ya kuinua uchumi wa familia na Taifa kupitia kilimo hivyo lazima waungwe mkono kwa hali na mali,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa licha ya wanawake kuwa ndiyo wengi wanaojishughulisha na shughuli za kilimo lakini bado wanakabiliwa na changamoto ikiwa ni pamoja na kutomiliki ardhi, miundombinu duni na kutoshirikishwa kwenye matumizi ya fedha zinazopatikana kwenye shughuli hizo.
“Tunapaswa kuunga mkono juhudi hizo za wanawake kwa kuwasaidia kwa hali na mali ili kuweza kuwaondolea changamoto zinazowakabili ili zisiwe kikwazo kwao katika sula zima la kilimo ambacho ni mkombozi wao na familia zao,” alisema Ndikilo.
Kwa upandewake mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi wa benki hiyo Rosebud Kurwijila alisema kuwa wameamua kuwapatia hundi hiyo ili iwasaidie katika harakati zao za kilimo hicho cha mbogamboga ili waweze kujikwamua kiuchumi.
Kurwijila alisema kuwa benki yao imeona iunge mkono serikali kuyawezesha makundi mbalimbali ili yaweze kujikwamua na kuongeza kipato kwa kuwapunguzia changamoto zinazowakabili ikiwemo hiyo ya vifaa kwa ajili ya umwagiliaji.
Naye mwenyekiti wa kikundi hicho Salma Mponda alisema kuwa wanashukuru kwa msaada huo ila wanaomba kupatiwa mafunzo kwa ajili ya ukopaji na utunzaji wa fedha ili waweze kufikia kuwa wakopaji wakubwa toka wakopaji wadogo.
Mponda alisema kuwa walianzisha kikundi hicho cha mbogamboga baada ya kuona kuwa mara wamalizapo shughuli zao za kilimo cha mpunga hawana jambo la kufanya na kuomba eneo kwa ajili ya kulima mbogamboga na kikundi hicho kilianzishwa mwaka 2016 na kupatiwa usajili na kwa sasa kina wanachama25.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...