WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemaliza mgogoro wa ardhi katika shamba la Chanzuru lenye ukubwa wa ekari 1,598 lililopo wilayani Kilosa, Morogoro kati ya Laizer Maumbi na Ameir Nahad kwa kuagiza likabidhiwe kwa Laizer ili aweze kuliendeleza kwa kulima mkonge.

 

Hata hivyo, Waziri Mkuu ameagiza eneo wanaloishi wananchi ndani ya shamba hilo kikiwemo kitongoji cha viwanja 60 na Chekeleni lihakikiwe na kupimwa ukubwa wake na kisha mkulima huyo akafidiwe eneo jingine na wananchi hao wasibugudhiwe.

 

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumatatu, Novemba 30, 2020) katika kikao chake na Makatibu Wakuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya Ardhi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Viongozi wa mkoa wa Morogoro, wilaya ya Kilosa pamoja na Laizer. Kikao hicho kimefanyika kwenye ukumbi wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Mlimwa jijini Dodoma.

 

“Viongozi wa Serikali simamieni na mratibu vizuri ili wananchi wanaoishi katika vitongoji vilivyomo ndani ya shamba hilo wasibugudhiwe waachwe waendelee kuishi na eneo lililobaki lisilokuwa na mgogoro apewe Laizer. Sehemu hiyo iliyopungua Laizer atafutiwe shamba jingine ili kufidia.”

 

Amesema awali shamba hilo lilikuwa linamilikiwa na Sadruddin Rajabali ambaye alimuuzia Laizer ambaye aliamua kuachana na shughuli za ufugaji na kuanza kulima mkonge, na alipokuwa katika harakati za kubadilisha umiliki shamba hilo liliuzwa kwa mtu mwingine.

 

Waziri Mkuu amewataka watumishi wa sekta ya ardhi wilayani Kilosa wahakikishe suala hilo wanalisimamia vizuri ili haki itendeke kwa mkulima huyo kukabidhiwa shamba lake na watumishi waliohusika katika mgogoro huo wachukuliwe hatua.

 

Pia, Waziri Mkuu ameuagiza uongozi wa mkoa wa Morogoro uhakikishe inabainisha maeneo makubwa yote ambayo hayajaendelezwa na kutoa mapendekezo Serikalini.

 

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Bw. Loatha Sanare ametumia fursa hiyo kumshukuru Waziri Mkuu kwa kumaliza mgogoro huo na kuahidi kwamba atasimamia utekelezaji wa maagizo na maelekezo yaliyotolewa.

 

Naye, Laizer ameishukuru Serikali kwa hatua iliyofikiwa ya yeye kukabidhiwa shamba hilo ambalo ndilo tegemeo lake kwa sasa, kwani aliuza mifugo yake yote na kununua shamba hilo ambalo amepanda mkonge.

 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...