Mwenyekiti wa Kampuni ya Kamal Gagan Gupta akizungumza Jijini Dar es Salaam jana. Pamoja naye ni meneja uhusiano wa kampuni hiyo Bi. Hedwick Peter.

==========

Kampuni ya Kamal imekuja na mbinu mpya ya uwezeshaji ambayo utawaendeleza wajasiriamali wakitanzania katika kubangua korosho.

Kwa kupitia kampuni yake ya Kamal Agro Limited, kampuni hiyo imekuja na mradi ambao unalenga kuwafanya Watanzania kuwa mstari wa mbele katika kutimiza azma ya serikali ya kujenga uchumi wa viwanda.

“Tumelipata wazo hili baada ya kufanya utafiti kwa miaka mitano ambapo tulibaini kuwa ili tuweze kushiriki kikamilifu katika azma ya Rais John Magufuli ya kujenga uchumi wa viwanda, hatuna budi kuja na mradi ambao utawawezesha Watanzania kutengeneza ajira kwa kuchakata bidhaa zinazozalishwa nchini,” alisema Mwenyekiti wa Kamal, Bw. Gagan Gupta.

Mradi wa kuendeleza ujasiriamali wa kitaifa Tanzania katika sekta ya viwanda vya kuchakata korosho umenuia kutumia mbinu zinazotumika nchini India ili kuongeza thamani kwa korosho ya Tanzania.

“Kule India, asilimia kati ya 70 na 80 ya korosho huchakatwa na viwanda vidogo vidogo kwa kushrikiana na viwanda vikubwa ambavyo husaidia wakati wa kuongeza thamani kabla bidhaa hazijapelekwa nje ya nchi kwa mauzo,” alisema.

Kwa kupitia mpango huo wa uwezeshaji, wajasiriamali wakitanzania watatengeneza maelfu ya ajira za moja kwa moja na kusaidia taifa kuokoa mamilioni ya dola zakimarekani zinazopetea kwa njia ya kuuza bidhaa ghafi nje ya nchi.

“Kama mnavyonijua, mimi ninafanya biashara ya kuzalisha nondo kwa muda mrefu ila nikiona fursa ambayo itasaidia Tanzania katika maeneo mengine huwa sisiti kuangalia jinsi ya kugawana faida zake na Watanzania wote…Kåwangu mimi, hii ni changamoto kubwa kwani endapo wajasiriamali hawa watashindwa itakuwa ni mimi nimeshindwa na siko tayari kuwaangusha,” alisema Bw. Gupta kwa msisitizo.

Mradi wa kuendeleza ujasiriamali wa kitaifa Tanzania katika sekta ya viwanda vya kuchakata korosho umetengenezwa kwa namna ambayo Kampuni ya Kamal Agro itawapatia wajasiriamali wapatao 100 kila kitu wanachokihitaji ili kuendesha viwanda vidogo vidogo 100 vya kuchakata korosho.

Mahitaji hayo ni pamoja na mashine za kuchakata korosho, mashine za kukaushia korosho, mashine za kumenyea, meza za kusagia, umeme, maji pamoja na gharama nyinginezo.

Mjasiriamali atahitaji kuwa na Shilingi milioni 16.92 ambazo zitakuwa sawa na asilimia 20 tu ya jumla ya kiasi cha Shilingi milioni 84.6 zinazohitajika kuendesha kiwanda cha kubangua korosho.

Bw. Gagan anailinganisha pesa ya mtaji ya mjasiriamali kuwa sawa na ada ambayo mwanachuo hulipa anapokwenda kujifunza kazi.

“Tofauti tu ni kwamba hapa unajifunza na kulipa ada lakini pia unapata faida kubwa kila mwaka….Hiin ndiyo maana ya uwezeshaji,” alisema.

Kiasi kinachobakia cha Shilingi milioni 67.68 ambacho ni sawa na asimilia 80 ya mahitaji kitapatikana kwa kupitia mkopo kutoka benki itakayoshirikiana na Kamal katika kudhamini mradi.

“Kwa hesabu za haraka haraka, kila mjasiriamali ataweza kupata faida ya Shilingi milioni 37.8 kwa mwaka baada ya kutoa gharama zote za uzalishaji,” alisema Bw. Gupta.

Faida ya mjasiriamali itaongezeka na kufikia Shilingi milioni 60 kwa mwaka ifikapo mwaka wa tatu wa usindikaji baada ya kumaliza kulipa mkopo wa benki.

“Baada ya kumaliza kulipa mkopo kwa muda wa miaka mitatu, kiwanda cha kubangua korosho kitabaki kuwa ni mali ya mjasiriamali,” alisema.

Tanzania itaokoa hadi Dola Zakimarekani milioni mia tatu (300) kwa mwaka kutokana na kuongeza thamani ya korosho ambayo kwa muda mrefu imekuwa ikiuzwa nje ya nchi bila kuongezwa thamani.

Kila mmoja kati ya wajasiriamali 100 ataweza kutengeneza ajira 20 za moja kwa moja na hivyo kuleta jumla ya ajira zitakazotengezwa kufikia 2,000 kwa awamu ya kwanza ya mradi.

Udhibiti wa ubora wa korosho na ufungaji vitasimamiwa na Kampuni ya Kamal.

Katika awamu ya kwanza ya miaka mitano, mradi utasaidia kubanguliwa kwa tani 15,000 za korosho ya Tanzania kwa mwaka. “Ila, ndani ya miaka kumi hadi 15, tunalenga kuhakikisha kuwa korosho yote inayolimwa Tanzania inabanguliwa hapa hapa nchini ili kutengeneza ajira zaidi,” alisema.

Hivi sasa, zaidi ya asilimia 90 ya korosho inayozalishwa nchini huuza bila kubanguliwa.

Wajasiriamali watakaopenda kuwa sehemu ya mpango huu watatakiwa kujaza fomu itakayopatikana katika tovuti ya https://kamal-group.co.tz/ ambapo watapata maelezo zaidi kuhusu mradi au kupiga simu kwenda: 0742308439. 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...