Na Rayson Mwaisemba WAMJW- Dom

Msajili wa Baraza la Famasi nchini Bi Elizabeth Shekalaghe ametoa siku 14 kwa wafamasia wanaosimamia famasi ambazo hazipo katika maeneo yao ya kazi kujisalimisha katika Baraza hilo.

Bi. Shekalaghe ametoa agizo hilo leo wakati akiongea na maafisa habari wa Wizara ya Afya katika ofisi zake zilizo katika jengo la Bima ya Afya Jijini Dodoma.

"Kwa wale wafamasia ambao, wanasimamia famasi ambazo hazipo ndani ya  maeneo yao ya kazi, natoa siku 14 kuanzia leo, kujisimisha Baraza la Famasi, mtu anakaa Morogoro anasimamia famasi Dodoma, lakini taarifa alizotuletea sisi yupo Dodoma, sasa tumeshaanza kufanya ufuatiliaji maalum ili kuwabaini" alisema Bi. Shekalaghe.

Bi Shekalaghe alisema kuwa, Baraza la Famasi limeanza kufanya ufuatiliaji maalum ili kuwabaini wafamasia wote wanaokiuka maadili na Sheria kwa kutoa taarifa za uongo za kuonekana yupo kwenye kituo fulani, wakati uhalisia anakuwa katika kituo kingine.

Kwa upande mwingine Bi Shekalaghe alisema kuwa, “Kifungu Na. 43 cha Sheria ya Famasi, Sura 311 kinaelekeza kwamba, hairuhusiwi mtu yoyote kujihusisha na biashara ya famasi kama sio mfamasia, huku akisisitiza endapo mtu huyo atahitaji kufanya hivyo, atalazimika kutafuta mfamasia ili asimamie huduma hiyo " alisisitiza Bi. Shekalaghe.

Alisema pia kuwa, Kanuni ya 10  ya Kanuni za Utendaji wa Taaluma za Mwaka 2020, zimeelekeza kwamba mfamasia atawajibika na usimamizi wa huduma katika famasi hiyo kila siku, huku akiweka wazi kuwa, kwa kiasi kikubwa bado wafamasia wengi hawawajibiki kwa kiwango cha kuridhisha katika maeneo yao ya kutolea huduma.

Aliendelea kusema kuwa, hivi karibuni kumekuwa na tabia ya wafamasia kuingia mikataba na wamiliki wa maduka ya famasi, huku wakishindwa kutekeleza majukumu yao, jambo ambalo ni kinyume na Kanuni za utendaji wa taaluma na bado wakipokea mishahara ya usimamizi wa famasi hizo bila kufika na kutekeleza majukumu yao ya msingi.

Aidha, Bi Shekalaghe ametoa rai kwa wafamasia wote nchini, kufika katika maeneo yao ya kazi.
"Nitoe rai kwa wafamasia kwamba, hakikisha unakwenda katika famasi unayosimamia kwasababu kanuni ya utendaji wa taaluma inakuelekeza kwamba, una wajibu  wa kufanya shughuli za usimamizi wa huduma za kila siku katika eneo hilo " alisema Bi Shekalaghe.

Mbali na hayo, amewaeleza wamiliki wa famasi kuwa, ni kosa kwa mfamasia kutokufika katika eneo la kazi, huku akisisitiza kuwa Kanuni ya 13 ya Kanuni za Usajili wa Famasi imeelezea kuwa,  kutofika kwa mfamasia katika famasi ni moja ya sababu za kufutwa kwa kibali cha uendeshaji wa huduma hizo kwa sababu ya kukosa usimamizi.  

Pia, Bi Shekalaghe amesisitiza kuwa, dawa si biashara, bali ni huduma ambayo inapaswa kusimamiwa kwa weledi wa hali ya juu na mtaalamu aliyepewa jukumu hilo kisheria na  mwenye vigezo na maadili ya utoaji huduma hiyo.

“Sitakubali kuona uzembe na kutowajibika kwa wafamasia wachache huku wakiendelea kuwaweka wananchi katika hatari ya kupata athari dhidi ya matumizi holela ya dawa. Hilo halikubaliki”

Amewakumbusha wanataaluma wote kusoma Sheria, Kanuni na Miongozo inayosimamia taaluma ya famasi na kuitekeleza pasipo shuruti wakati wanatekeleza majukumu yao. 

Msajili wa Baraza la Famasi nchini Bi Elizabeth Shekalaghe

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...