Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya akizungumza  na Wafanyabiashara Wakubwa wa madini (Dealers) na Wadogo (Brokers) kwenye ziara yake Mkoani Shinyanga

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Bi. Zainabu Telack akizungumza na Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya  ofisini kwake kuhusu  mgogoro wa uvamizi katika  Mgodi wa El Hillal Mkoani Shinyanga

Baadhi ya Wachimbaji wadogo wa madini waliovamia mgodi wa mwekezaji katika  Mgodi wa El Hillal  wakisikiliza maelekezo toka kwa Naibu Waziri wa Madini

Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Shinyanga Mhandisi Joseph Kumburu akitoa taarifa kuhusu mgogoro wa uvamizi wa mgodi wa El Hillal  mbele ya kamati ya Ulinzi na Usalama  ya Mkoa

Baadhi ya kamati ya Ulinzi na Usalama  ya Mkoa wa Shinyanga waliohudhuria kikao cha Naibu Waziri wa Madini Prof. Manya Januari 21, 2021 Mkoani Shinyanga

………………………………………………………………………………………….

Na Steven Nyamiti, Shinyanga

# Apinga uvamizi wa maeneo yenye leseni hai

# Asisitiza kuondoka katika kesi za utoroshaji madini na uvamizi wa maeneo

# Aeleza kuheshimu mifumo iliyopo sasa kwenye Sekta ya Madini

# Atoa angalizo kwa Wafanyabiashara na madalali wanaohamasisha uvamizi

Wavamizi wa  eneo la mwekezaji wa kampuni ya El Hillal Limited iliyopo Katika eneo  la Mwang’holo kata ya Mwadui Mkoani Shinyanga wamepewa siku mbili ili kupisha shughuli za mwekezaji huyo kuendelea.

Maagizo hayo yametolewa  leo Januari 21, 2021 na Naibu Waziri wa Madini, Prof. Shukrani Manya alipotembelea eneo hilo na kuitaka kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Shinyanga kuwaondoa wavamizi  ili kulinda eneo hilo la mwekezaji.

Agizo hilo limetolewa baada ya Naibu Waziri wa Madini Prof. Manya kupokea  malalamiko kutoka kwa Kampuni ya El Hillal Minerals Limited yenye leseni ya uchimbaji mkubwa wa madini ya almasi SML 404/2010 kuhusiana na kuvamiwa na wachimbaji wadogo katika eneo lake.

Awali Katika kikao baina ya uongozi wa Wizara na Wachimbaji wakubwa wa Madini ya Almasi, Wachimbaji Wadogo  pamoja na Wafanyabiashara wa madini Prof. Manya ametoa maelekezo maalumu akiwataka kusitisha utaratibu wa kuendelea kudhamini vikundi mbalimbali vya wachimbaji wadogo kuvamia kwenye eneo lenye leseni na kushauri wazingatie Sheria za Madini zilizopo sasa kwa faida ya pande zote.

 “Ninaelekeza wachimbaji wote waliovamia eneo hili la mgodi kuondoka ndani ya siku mbili kwa kuwa mnafanya shughuli za madini kinyume na sharia,” amesema Naibu Waziri.

Prof. Manya ameeleza kuwa ili wawekezaji wajitokeze kwa wingi ni lazima Serikali ilinde haki za wachimbaji wakumbwa, wadogo na wakati. “Sheria ya Madini inasema mwenye leseni anao wajibu wa kuheshimiwa pamoja na kupatiwa Ulinzi na Usalama ili afanye shughuli zake ipasavyo.

Aidha, Prof Manya amemuelekeza  Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga kuhakikisha anaongeza Ulinzi na Usalama wa eneo hilo baada ya siku mbili kukamilika  kuanzia leo.” Ninawataka wachimbaji wote mliovamia eneo hili mfuate utaratibu uliopangwa na namuelekeza Afisa Madini Mkazi  wa Mkoa huu kuhakikisha anawapatia eneo tofauti ili muendelee na uchimbaji lakini mkiwa kwenye taratibu  zinazotambulika kisheria.”

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Bi. Zainabu Teleck amempongeza Prof. Manya kwa kutoa maelekezo kwa wachimbaji  kuondoka ndani ya siku mbili na kutoa maelekezo kwa kamati yake  ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa kuzingatia maagizo hayo ili kutatua mgogoro huo wa uvamizi. 

Naye, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Shinyanga, Mhandisi Joseph Kumbulu amesema kuwa mnamo  tarehe 20/03/2020 Ofisi ya Madini kwa kushirikiana na vyombo vya Ulinzi na Usalama iliwatoa wachimbaji wadogo zaidi ya 400 waliovamia eneo  lenye leseni ya uchimbaji ya mgodi wa mwekezaji huyo.

Ameongeza hadi sasa eneo hilo lina idadi kubwa ya wachimbaji zaidi ya 1,000. Hivyo amesisitiza kusimamia kikamilifu maagizo yaliyotolewa na Naibu Waziri wa Madini ili kulinda haki za muwekezaji kwenye eneo hili na kutatua migogoro inayotokea kwenye maeneo ya kimadini hapa nchini, ameeleza Kumbulu.”

Kumbulu amesema kuwa anaomba elimu itolewe kwa viongozi wa vijiji, vitongoji na Kata kuhusu umiliki halali wa ardhi na Sheria za Madini kwakuwa kumekuwa na changamoto kubwa ya utoaji wa vibali na uuzwaji wa ardhi kwenye maeneo ambayo yanamilikiwa na mgodi kisheria.

Naibu Waziri wa Madini, yupo kwenye ziara ya kutembelea maeneo mbalimbali yenye shughuli za madini hapa nchini na ziara yake katika eneo la mgodi wa Kampuni ya El Hillal limekuwa la faida kwa mwekezaji huyo baada kutoa   maelekezo kwa wavamizi kuhakikisha wanatoka kwenye eneo hilo ambalo ni.leseni halali ya mchimbaji mkubwa wa madini ya almasi

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...