MKUU  wa Mkoa wa Ruvuma Christina Mndeme akizungumza kwenye Kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC,) amewaagiza Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA) kupeleka wanyama kwenye kisiwa cha Lundo ziwa Nyasa wilaya ya Nyasa.

Mndeme amesisitiza kuwa kupelekwa kwa wanyama katika kisiwa hicho,kutasaidia kuongeza vivutio kwa watalii kwa lengo la kutangaza vivutio vya utalii vinavyopatikana wilaya ya Nyasa ambayo imetangazwa kuwa kitovu cha utalii katika Mkoa wa Ruvuma.

Mkuu wa Mkoa pia aliwaagiza wadau wa utalii na uhifadhi wakiwemo TAWA  na TANAPA  kuchukua jukumu la kutoa elimu ya uhifadhi na utalii kwa wananchi hasa wa Mkoa wa Ruvuma kuhusu umuhimu wa sekta ya utalii katika kuchochea uchumi.

Mndeme pia ameagiza ushoroba na mapito ya wanyama katika Mkoa wa Ruvuma yaheshimiwe na kulindwa kwa sababu ni moja ya rasilimali za nchi na ameagiza wananchi wote waliovamia maeneo hayo waondolewe haraka.

Kufuatia maagizo hayo wadau wa utalii mkoani Ruvuma wakiwemo TAWA,TANAPA na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania(TFS) wameanza kuchukua hatua ikiwemo azma ya kuanzisha hifadhi ya kufuga wanyamapori katika kisiwa cha Lundo,kifuga ndege katika kisiwa cha Mbambabay(Zambia).

Mshauri wa Maliasili na Utalii Mkoa wa Ruvuma Afrikanus Challe anasema wanatarajia kuanzisha hifadhi ya Mbambabay ambayo inajumuisha visiwa vya Lundo,Mbambabay na milima ya Mbamba,Tumbi na Ndengere wilayani Nyasa.

Challe anaitaja hifadhi ya Mbambabay  itakuwa na ukubwa  wa eneo la hekta 597 na kwamba maeneo hayo yanafaa kwa kufuga wanyamapori na ndege.

Hata hivyo anasema Kati ya hekta hizo, mlima Mbamba una eneo lenye ukubwa wa hekta40,mlima Tumbi hekta 110,kisiwa Mbambabay chenye hekta 27,kitakuwa maalum kwa ufugaji wa ndege na kisiwa cha Lundo chenye ukubwa wa hekta 20,TAWA inatarajia kupeleka wanyamapori jamii ya swala.

“Milima na visiwa hivi vimejaaliwa kuwa na uoto mzuri wa miombo,mawe yanayozunguka visiwa hivi na milima kando kando ya ziwa yana hifadhi samaki adimu wa mapambo zaidi ya aina 400’’,anasisitiza Challe.

Kwa mujibu wa Challe,eneo la hifadhi ya Mbambabay ni muhimu sana kwa upande wa Tanzania  hususan katika matumizi ya shughuli za utalii kama vile utalii wa kuvua samaki,kupiga mbizi,yatching,utalii wa kuendesha mitumbwi na kuweka kambi kwenye fukwe.

Mtalaam huyo wa uhifadhi anasema eneo hilo likihifadhiwa litatumika kwa ajili ya mazalia ya samaki na hivyo kuongeza kipato kwa wananchi wanaotegemea shughuli za uvuvi.

“Mbambabay ikihifadhiwa inaweza kuleta ushindani kibiashara hapa nchini kwa sababu katika nchi yetu hakuna eneo linaloweza kutoa mchanganyiko mzuri wa huduma za kitalii kama zitakazotolewa katika eneo hili’’,anasisitiza Challe.


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...