Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Selemani Jafo (Mb), akimsikiliza Mkurugenzi wa Barabara za Mijini (TARURA), Mhandisi Mohamed Mkwata alipokuwa akitoa taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa Barabara za Mji wa Serikali (Mtumba) kwa kiwango cha lami zenye urefu wa Km 51.2 jijini Dodoma.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Selemani Jafo (Mb), akizungumza na Wataalamu wa TARURA alipotembelea mradi wa ujenzi wa barabara inayoelekea Hospitali ya Uhuru kwa kiwango cha lami yenye urefu wa Mita 320 katika Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino, mkoani Dodoma.

*************************************

Na. Thereza Chimagu, Dodoma.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhe. Selemani S. Jafo (Mb), ameridhishwa na kasi ya ujenzi wa Barabara inayoingia Hospitali ya Uhuru kwa kiwango cha lami yenye urefu wa Mita 320 kwa njia mbili ambayo inasimamiwa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) katika Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma.

Waziri Jafo alitoa pongezi hizo alipokuwa akifanya ziara ya ukaguzi wa miradi mbalimbali mkoani Dodoma Machi 03, 2021 na kuoneshwa kuridhishwa na kasi ya ujenzi wa Barabara hiyo.

“Tumejenga Hospitali ya Uhuru lakini sehemu hii ya kuingilia ilikuwa na changamoto kubwa, nimekuja hapa kuangalia maendeleo ya ujenzi wa barabara hii na kwa kweli nimeridhika kuona maendeleo ya ujenzi wa barabara hii”, alisema Mhe. Jafo.

Aidha Mhe. Jafo alimtaka Mkandarasi anayetekeleza ujenzi wa barabara hiyo M/S Nyanza Co. Ltd kutumia muda uliopo ili kuweza kukamilisha mradi kwa wakati kutokana na changamoto za mvua zinazoendelea kunyesha.

Akitoa taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa Barabara hiyo, Meneja wa TARURA Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino Mhandisi Nelson Maganga alisema kuwa ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami umefikia asilimia 85 na tayari lami nyepesi imekamilika kwa ajili ya kuweka tabaka la lami nzito.

“Ujenzi wa Barabara umefikia asilimia 85 kukamilika na tunatarajia Mkandarasi kumaliza kazi kulingana na mkataba kufikia Machi 14, 2021, sehemu hii ya barabara imegharimu kiasi cha shilingi Milioni 511”, alisema Mhandisi Nelson.

Katika hatua nyingine Mhe. Jafo alifanya ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi wa Barabara za Mji wa Serikali Mtumba kwa kiwango cha lami zenye urefu wa Km 51.2 na kuonesha kutoridhishwa na kasi ya Mkandarasi anayetekeleza ujenzi wa barabara hiyo Kampuni ya China Heinan International Cooperation Co. Ltd (CHICO) na kumtaka Mkandarasi huyo kuhakikisha anamaliza ujenzi kama ilivyo kwenye Mkataba ifikapo Julai 30, 2021.

“Sijaridhishwa na maendeleo ya ujenzi wa mradi huu kuwa chini ya asilimia 6, leo hii mpo asilimia 63 na mlitakiwa muwe asilimia 69 mimi nilikuja hapa nikijua mpo asilimia 70, sihitaji mjadala wa aina yeyote ninachotaka mradi huu uwe umekamilika kama ilivyo kwenye makubaliano”, alisema Mhe Jafo.

Akitoa taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa Barabara za Mji wa Serikali Mtumba, Mkurugenzi wa Barabara za Mijini TARURA, Mhandisi Mohamed Mkwata alisema kuwa Mkandarasi amefikia asilimia 63 za maendeleo ya jumla ya utekelezaji wa Mradi ambapo alitakiwa kuwa asilimia 69, ameongeza kuwa ujenzi wa tabaka la lami umefikia Km 11.2, uwekaji wa lami nyepesi Km 15.7, ujenzi wa tabaka la pili umefikia Km 15.7, ujenzi wa tabaka la kwanza umefikia Km 15.7, ujenzi wa mifereji Km 6.6, pamoja na ujenzi wa vivuko 64 dhidi ya 130 vinavyohitajika.

Aidha, Mhandisi Mkwata alieleza kuwa katika kipindi cha mwezi Novemba 2020 uhaba wa Saruji pamoja na mvua zinazoendelea kunyesha zilisababisha baadhi ya kazi kusimama na kufanya Mkandarasi kuwa nyuma ya asilimia 6 za utekelezaji wa Mradi na kuongeza kuwa ili kufidia muda uliopita Mkandarasi ameongeza mitambo ili kuweza kumaliza mradi huo kwa wakati uliopangwa.

Mhe. Jafo amefanya ukaguzi katika Barabara ya Mji wa Serikali Mtumba ikiwa ni ziara yake ya tatu kukagua maendeleo ya ujenzi wa barabara hiyo inayosimamiwa na TARURA na mradi unatarajiwa kukamilika ifikapo tarehe 30 Julai, 2021.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...