Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani  (katikati) akizungumza na moja ya wataalam (kushoto), wanaofanya kazi ya kutengeneza baadhi ya mitambo ya umeme katika Kituo cha umeme cha Songas kilichopo Ubungo mkoani Dar es Salaam. Wengine katika picha ni watendaji kutoka Wizara ya Nishati, TANESCO, Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC) na Songas.

Waziri wa Nishati, Dkt.Medard Kalemani ameagiza kuwa, matengenezo ya mitambo mbalimbali ya kufua umeme nchini yakamilike ndani ya siku Tano ili kuhakikisha kuwa wananchi wanapata umeme wa uhakika.

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani  (kushoto) akipata maelezo kuhusu matengenezo ya mitambo miwili ya umeme katika kituo cha umeme cha Songas kilichopo Ubungo mkoani Dar es Salaam. Anayetoa maelezo ni Meneja Mitambo wa Songas, Michael Mngodo.

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani  (wa Pili kulia) akipata maelezo kuhusu mitambo ya umeme katika kituo cha umeme cha Songas kilichopo Ubungo mkoani Dar es Salaam. Anayetoa maelezo ni Mkurugenzi Mkuu wa Songas, Anael Samuel (wa kwanza kushoto.Wa kwanza kulia ni Mwenyekiti wa Bodi ya TANESCO, Dkt. Alexander Kyaruzi.

Mafundi wakiendelea na kazi ya utengenezaji wa moja ya mtambo wa umeme katika kituo cha umeme cha Songas kilichopo Ubungo mkoani Dar es Salaam.

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (katikati) akizungumza na Bodi na Menejimenti za Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC) kabla ya kukagua kituo cha umeme cha Songas kilichopo Ubungo mkoani Dar es Salaam. Kushoto kwake ni Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Mhandisi Leonard Masanja na kulia kwake ni Mwenyekiti wa Bodi ya TANESCO, Dkt. Alexander Kyaruzi.

Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Mhandisi Leonard Masanja (wa kwanza kushoto), Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Edward Ishengoma na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Dkt. Tito Mwinuka wakiwa katika kikao cha Waziri na  Bodi na Menejimenti za TANESCO na Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC) kabla ya kukagua kituo cha umeme cha Songas kilichopo Ubungo mkoani Dar es Salaam

……………………………………………………………………………………………………..

Na Teresia Mhagama, Dar es Salaam

Waziri wa Nishati, Dkt.Medard Kalemani ameagiza kuwa, matengenezo ya mitambo mbalimbali ya kufua umeme nchini yakamilike ndani ya siku Tano ili kuhakikisha kuwa wananchi wanapata umeme wa uhakika.

Dkt. Kalemani ametoa agizo hilo tarehe 2 Machi, 2021 mkoani Dar es Salaam,  mbele ya Bodi na Menejimenti za Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Songas, baada ya kukagua kituo cha umeme cha Songas ambacho mitambo yake miwili inafanyiwa matengenezo na hivyo kuzalisha umeme wa kiasi cha megawati 115 badala ya 180.

Akiwa ameambatana na Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Leonard Masanja, Waziri Kalemani amesema kuwa, hataki kusikia wananchi wakilalamika kukosa umeme kwa sababu tu ya matengenezo ya mitambo, hivyo matengenezo hayo yakamilike ndani ya siku alizoagiza au kwa siku chache zaidi.

Aidha, kuhusu muda wa kufanya matengenezo ya mitambo ya umeme nchini, Dkt. Kalemani ameiagiza TANESCO na Songas kupishanisha muda wa matengenezo ili kutoathiri hali ya upatikanaji wa umeme nchini.

Vilevile, Dkt.Kalemani alisisitiza kuhusu utekelezaji wa agizo alilolitoa kwa TPDC la kuhakikisha kuwa vifaa mbalimbali vinavyotumika kwenye miundombinu ya gesi nchini kama vile valvu na mabomba vinatengenezwa nchini ili kurahisisha upatikanaji wa vifaa husika.

Vilevile, amesema kuwa, Wizara ya Nishati haitaacha kufuatilia kwa karibu utendaji kazi wa Taasisi zilizo chini yake kwani lengo ni kuhakikisha kuwa Taasisi hizo zinafanya kazi kwa ufanisi na wananchi wanapata huduma wanazostahili.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa Songas, Anael Samuel, alimueleza Waziri wa Nishati kuwa, matengenezo ya mitambo miwili ya umeme kwenye kituo hicho, yanaenda sambamba na matengenezo katika bomba la Gesi kutoka Songosongo linalopeleka gesi kwenye mitambo hiyo ya Songas ili kuzalisha umeme.

Alisema kuwa, kutokana na bomba hilo la gesi kutoka Songosongo kufanyiwa matengenezo, kwa sasa megawati 115 zinzozalishwa kwenye kituo hicho zinatokana na mitambo ya gesi ya Shirika la Maendeleo Tanzania (TPDC).

“Nazipongeza Taasisi za TPDC na TANESCO kwa kushirikiana na Songas kwani tulikaa pamoja kama wadau ili kuona namna tutakavyotatua tatizo hili, na ndiyo maana angalau megawati 115 zinaendelea kuzalishwa kwa kutumia mitambo ya TPDC.” Alisema Samuel

Aidha, alisema kuwa, ukarabati wa mitambo hiyo unafanyika kwa ratiba maalum ili kuweza kutoa uhakika wa mitambo hiyo kuendelea kuzalisha umeme kwa muda mrefu zaidi.

Kwa upande wake, Meneja Mitambo wa Songas, Michael Mngodo alisema kuwa kituo cha umeme cha Songas kina mashine Sita ambapo kwa sasa mashine zinazofanya kazi ni nne na zinazofanyiwa matengenezo ni mashine mbili

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...