Na Mwandishi wetu, Mirerani
Wanawake
wachimbaji wa madini ya Tanzanite wa Mji mdogo wa Mirerani Wilayani
Simanjiro Mkoani Manyara, wameiomba Serikali kuwaruhusu waingie ndani ya
migodi yao wanayoichimba.
Wanawake
hao wachimbaji wametoa ombi hilo kwenye semina ya ya uchimbaji madini
iliyofanyika jana mji mdogo wa Mirerani na kuandaliwa na shirika la
mazingira na haki za wanawake la Envirocare.
Mmoja
kati ya wanawake wanaomiliki mgodi wa madini Stella Shayo amesema
wanawake pia wana haki ya kuingia kwenye migodi yao pindi wakiwa
wanaichimba.
"Tunapaswa
kupata ruhusa ya kuingia katika migodi yetu tunayochimba kwani hakuna
tatizo lolote pindi wanawake wakizamia migodini kwani wapo waliowahi
kufanya hivyo," amesema Shayo.
Mmoja
kati ya watoa mada Dk Curtis Msosa amesema hakuna ubaya kwa wanawake
kuruhusiwa kuingia mgodini kwani mmiliki mmoja Pili Hussein alishawahi
kuingia mgodini na hakudhurika.
"Pia
wapo waandishi wa habari wanawake walishawahi kuingia ndani ya mgodi wa
madini ya Tanzanite na hakupata tatizo lolote lile pindi wakiwa
mgodini," amesema Dk Msosa.
Hata
hivyo, ofisa mazingira wa Tume ya madini, Nelusigwe Mwakatobe amesema
hakuna sheria ya madini inayokataza wanawake kuingia katika migodi
wanaochimba.
Mwakatobe
amesema wanawake hao wanapaswa kuingia ndani ya migodi ambayo ni imara
na yenye usalama ili isitokee ajali pindi wakiingia mgodini.
Mjumbe
wa chama cha wanawake wachimbaji madini nchini (Tawoma) Rachel Njau
amesema miongoni mwa changamoto zinazowakabili wanawake hao ni kulipia
leseni ambayo wanachangia na wanaume.
"Unakuta
kwenye zile mita 50 kwa 50 kuna migodi hata minne ya watu tofauti hivyo
wanawake huwa ndiyo wanalipa ada ya leseni badala ya kulipa wote kwa
pamoja," amesema Njau.
Meneja
mradi wa shirika la kutetea haki za wanawake na mazingira (Envirocare)
Amos Mbwambo amesema wamefanya mafunzo kama hayo kwenye mikoa ya
Shinyanga na Mbeya.
Mbwambo
amesema lengo la mradi huo wa miaka miwili ni kushirikisha jinsia zote
mbili ili ziweze kumiliki rasilimali zilizopo na kuwainua kiuchumi
wanawake katika madini.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...