Na  Woinde Shizza, ARUSHA

Kati ya Mikoa kumi ya Tanzania bara iliyofanyiwa Utafiti na chama Cha wafanyabiashara Nchini (TCCIA), Mkoa wa Songwe umebainika kuongoza kwa wafanyabiashara kufunga biashara zao kutokana na  matatizo mbalimbali ikiwemo utitiri wa Kodi.

Utafiti huo umefanywa kwa miaka miwili kupitia Mradi wa kuboresha mazingira rafiki ya kibiashara Tanzania(Building Bridges) unaotekelezwa kwa ubia na shirika la Trias na  TCCIA, chini ya ufadhili wa jumuiya ya Ulaya (EU).

Akiongea na vyombo vya habari mratibu wa Mradi huo ,Nebart Mwapwele alisema lengo la Mradi ni kujenga daraja Kati ya sekta binafsi na Umma ili kuboresha mazingira ya biashara na wamefanya utafiti huo kwa kuwahoji wafanyabiashara wapatao 3000 nchini mzima.

Alisema wafanyabiashara waliohojiwa kupitia Mradi huo walidai kuwepo kwa changamoto kubwa ambayo ni pamoja na ukadiriaji wa Kodi kubwa ,utitiri wa Kodi katika biashara moja na ukosefu wa masoko jambo lililosababisha baadhi yao kushindwa kuendelea na biashara.

"Baadhi ya Wafanyabiashara waliohojiwa wamelalamikia utitiri wa Kodi katika biashara ya aina moja ,ukadiriaji mkubwa wa Kodi kabla hata hawajaanza biashara"alisema

Naye afisa mtendaji wa TCCIA  Elijah Simbeye kutoka Mkoa wa Songwe alisema kuwa utafiti uliofanyika kuanzia January mwaka Jana katika Mikoa kumi ,Mkoa wa Songwe ndio unaongoza kwa wafanyabiashara kufunga biashara zao kutokana na Mamlaka mbalimbali za serikali ikiwemo TRA kutokuwa rafiki na wafanyabiashara hao.

"Baada ya tafiti kufanyika kwa kuongea na wafanyabiashara katika Mikoa kumi,Mkoa wa Songwe ambao natoka Mimi ndio unaongoza kwa wafanyabiashara kufunga biashara"alisema

Aidha alisema utafiti umeonyesha kuwa wafanyabiashara wengi hawaelewi utendaji kazi wa mamlaka za serikali zinazohudumia wafanyabiashara zikiwemo Osha,Latra,serikali za mtaa,TMDA ,Fire na zingine Jambo linalosabahisha kuwepo kwa malalamiko.

Kwa upande wake mwakilishi wa shirika la Trias, Beatrice Minde ambao ni watekelezaji wa Mradi huo alisema wamefanikiwa kupitia kumbukumbu za tafiti zilizokusanywa kwa wafanyabiashara 3000 waliohojiwa na kwamba shirika hilo litayafikisha mapendekezo hayo ngazi ya serikali .

Alisema kuwa tafiti hizo zimefanyika katika Mikoa 10 ambayo ni Mwanza,Dar es Salaam ,Arusha,Mtwara ,Shanyanga , Dodoma,Kigoma,Songwe ,Mbeya na Mara.

Naye mkurugenzi was TCCIA Mkoa wa Dodoma na Makamu wa Rais Biashara wa TCCIA,Dkt Ezekiel Meshack walisema Matokeo ya tafiti yatarejeshwa kwa Kila mamlaka husika za serikali ili kuona namna ya kuyafanyia kazi matatizo  yaliyoibiliwa.



Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...