Wakati Watanzania takribani milioni 22 sawa na asilimia 52 wanaugua ugonjwa wa kichocho na  minyoo ya tumbo,Kanda ya Ziwa inaongoza kwa kuwa na maambukizi ya asilimia 50 hadi 80  ya magonjwa hayo yaliyokuwa hayapewi kipaumbele.

Mratibu wa Magonjwa yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele (NTD) Mkoa wa Mwanza, Dkt. Mabai Leonard, alisema  kuwa ugonjwa wa kichocho na minyoo ya tumbo bado ni tatizo kubwa mkoani humu.

Dkt.Mabai alisema kuwa, takribani Watanzania milioni 22 wanaugua kichocho na minyoo ya tumbo, ili kukabiliana na tatizo hilo Mkoa wa Mwanza umeandaa zoezi la utoaji wa  kingatiba kwa watoto wa umri wa kwenda shule kuanzia miaka 4 hadi miaka 15 wa shule za msingi zote ambapo sh. 288,474,400 zimetengwa kwa ajili ya zoezi hilo.

Aidha,aliongeza kuwa ugonjwa wa kichocho na minyoo ya tumbo hauna dalili za haraka kabla ya kupata matibabu hivyo zoezi la kutoa  kingatiba inalenga kudhibiti na kutibu magonjwa hayo kwenye jamii.

Hata hivyo alisisitiza kuwa, halmashauri zote mkoani Mwanza zihakikishe watoto watakaopewa  kingatiba  wamepata chakula saa mbili kabla ya kumeza alizitaja Kingatiba hizo ni aina ya Albendazole kwa ajili ya minyoo ya tumbo na Prazequantel ya kichocho.

 "Tatizo la ugongwa wa kichocho na minyoo ya tumbo mkoani Mwanza linasababishwa na jiografia yake ya kuwa na maji mengi, shughuli za kilimo (majaruba ya mpunga) asili ya madimbwi ya maji na hivyo wananchi wako kwenye hatari ya kupata magonjwa hayo," alisema Dkt.Mabai.

Naye Profesa Huphrey Mazigo wa Chuo Kikuu Katoliki cha Sayansi na Tiba za Afya Bugando(CUHAS), alisema magonjwa 17 yakiwemo kichocho na minyoo yaliyo Ukanda wa Tropiki yanaikumba jamii masikini vijijini hasa zinazoishi chini ya Dola 2 na zisizo na uwezo wa kugharamia tiba na athari kwa watoto wa umri wa kwenda shule.

“Tanzania ni moja ya nchi zilizoathiriwa na ugonjwa wa kichocho hasa bonde la Ziwa Victoria hasa wakulima, wavuvi na watoto na watu bilioni 2 duniani wameathirika na minyoo ya tumbo, zaidi ya watu milioni 300 wameathirika sana huku 155,000 kila mwaka duniani hufariki kutokana na magonjwa hayo,”alisema Profesa Mazigo.

Kwa upande wake Kaimu Mratibu wa Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Magonjwa Yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele, Oscar Kaitaba, alisema yapo magonjwa  yanasababisha madhara kwa binadamu kama madhara ya kudumu, kuathiri maendeleo na makuzi ya watoto, kupunguza uwezo wa utendaji na hivyo kusababisha umasikini kwenye jamii.

Hata hivyo, licha ya changamoto mbalimbali yapo  mafanikio katika utoaji  kingatiba kwenye halmashauri 184 nchini ambapo kiwango cha maambukizi kimepungua kwenye halmashauri 71 bado halmashauri 6.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. John Mongella, akifungua kikao kazi Cha uhamasishaji wa  magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele yaliyofanyika Jijini Mwanza, alisema  ongezeko la magonjwa hayo  yanapunguza utimamu wa afya ya jamii na kusababisha familia kutumia rasilimali nyingi kukabiliana na magonjwa hayo.

“Ni wajibu wetu kila mmoja kwa nafasi yake kuunga mkono juhudi za serikali na wadau kwenye maeneo yetu ili kupambana na mgonjwa hayo yakiwemo ya kichocho na minyoo ya tumbo,nia ni kulifanya taifa liwe na watu wenye afya bora ili washiriki shughuli za maendeleo,”alisema Mongella.


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...