Na Karama Kenyunko Michuzi TV

BAADA ya kukaa mahabusu takribani miaka mitano leo Juni 16, 2021 Mkurugenzi wa a Mashtaka nchini (DPP) ameondoa hati ya kuzuia dhamana kwa aliyekuwa Mkurugenzi wa Kampuni ya Hodhi ya Mali za Shirika la reli (RAHCO), Benhardard Tito na wenzake wawili.

Wakili wa Serikali Mwandamizi, Wankyo Simon amewasilisha maombi hayo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakati kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya kuendelea kusikilizwa.

"Mheshimiwa shauri leo linakuja kwa kuendelea kusikilizwa ila shahidi tunayemtegemea amepata udhuru, kasafiri nje ya Dar es Salaam na pia katika shauri hili, DPP anaitaarifu mahakama kwamba anaondoka hati ya kuzuia dhamana dhidi ya washtakiwa," amedai Wankyo na kuomba maelekezo.

Hakimu Simba alikubali maombi hayo na kuamua kuondoa hati hiyo.

Wakili wa utetezi, Peter Kibatala aliomba mahakama hiyo iridhie kuwapa washtakiwa dhamana kwa sababu kilichokuwa kinazuia ni hati ambayo tayari imeondolewa na kwamba sasa mahakama inamamlaka ya kusikiliza kesi.

Baada ya kuelezwa hayo, Hakimu Simba alisena, kutokana na mfumo wa sheria baada ya kuondolewa hati hiyo mashtaka yaliyopo yanadhaminika hivyo amewataka washtakiwa ili wawe nje kwa dhamana kila mshtakiwa anatakiwa kuwa na wadhamini wawili wenye barua, kila mdhamini atasaini bondi ya Sh 202,223,666, anatakiwa kuwasilisha fedha taslimu kiasi hicho au hati ya mali isiyohamishika yenye thamani ya kiasi hicho cha fedha.

Masharti mengine kila mshtakiwa atawasilisha hati ya kusafiria mahakamani na haruhusiwi kutoka nje ya Dar es Salaam bila kibali cha mahakama.

Washtakiwa hawajafanikiwa kutimiza masharti ya dhamana, kesi imeahirishwa hadi Julai 14 mwaka huu.

Mbali na Tito, washtakiwa wengine ni Mwanasheria wa Rahco, Emmanuel Massawe na mfanyabiashara ambaye pia ni mwakilishi wa Kampuni ya Rothschild (South Africa) Proprietary Limited, Kanji Mwinyijuma.

Katika kesi ya msingi, washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka nane ikiwamo uhujumu uchumi, matumizi mabaya ya madaraka, kula njama na kuisababishia Rahco hasara ya dola za Marekani 527,540.

Wanadaiwa kati ya Septemba Mosi, 2014 na Septemba 30, 2015 kwa nia ya kutenda kosa walikula njama kinyume cha sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa.

Inadaiwa Februari 27, 2015 katika ofisi za Rahaco zilizopo Ilala Tito alitumia madaraka yake vibaya kwa kuiajiri Kampuni ya Rothschild (South Africa) Proprietary Ltd kama mshauri wa mradi wa uimarishaji reli ya kati bila idhini ya Bodi ya Zabuni ya Rahaco.

Tito na Massawe wanadaiwa Machi 12, 2015 katika ofisi za Rahaco Ilala wakiwa katika nyadhifa zao, walisaini barua ya kuihalalisha kampuni hiyo ya Afrika Kusini kuwa mshauri wa mradi wa uimarishaji reli ya kati na kutoa huduma za ushauri wa kifedha kuhusu mradi huo.

Pia Tito na Massawe, wanadaiwa kuwasilisha mkataba wa huduma ya ushauri kati ya kampuni hiyo ya Afrika Kusini na Rahaco. Pia wanadaiwa kutumia madaraka yao vibaya kwa kusaini mkataba wa kutoa huduma za ushauri na kampuni ya Afrika Kusini bila ridhaa ya Bodi ya Zabuni ya Rahaco.

Washtakiwa hao, wanadaiwa kati ya Mei 20 na Juni 20, 2015 walitumia madaraka yao vibaya kwa kushindwa kuwasilisha mkataba walioingia na kampuni ya Afrika Kusini kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.


 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...