Na Amiri Kilagalila
Mwenyekiti
wa umoja wa wanawake wa Chama cha Mapinduzi mkoa wa Njombe (UWT) ambaye
pia ni mkurugenzi wa Kampuni ya Udalali ya ‘Yono Auction Mart’
Scolastika Kevela amempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kuwaongoza
watanzania katika chanjo dhidi ya ugonjwa wa Covid-19 huku akiwataka
wananchi kumuunga mkono.
Akizungumza
na waandishi wa habari, Mama Kevela alisema hatua hiyo ya Rais Samia
Suluhu Hassan imeiidhihirishia Dunia kuwa Tanzania siyo kisiwa na kwamba
haiwezi kujitenga katika kupambana na ugonjwa huo uliopoteza maisha ya
mamilioni ya watu tangu ulipotangazwa kuingia duniani.
Kauli
ya mwenyekiti huyo wa UWT Mkoa wa Njombe imekuja muda mfupi baada ya
Rais Samia Suluhu Hassan kuzindua rasmi chanjo ya ugonjwa huo huku
akiwa wa kwanza kupata chanjo hiyo na baadae kufuatiwa na viongozi
wengine wa kidini, Chama na Serikali, tukio lilifanyika katika Ikulu ya
Dar es Salaam na kurushwa na vyombo mbalimbali vya habari.
“Naungana
na viongozi wengine wengi wa Taifa hili wakiwemo wa Chama changu cha
Mapinduzi(CCM) pamoja na kidini waliojitokeza na kumpa pongezi
Mheshimiwa Rais Samia kwa kuungana na mataifa mengine katika kukabiliana
na ugonjwa huu, hatua hii itatuondolea wananchi kasi ya maambuziki
lakini pia kutuepusha na vifo” alisema Mama Kevela .
Awali
akizindua chanjo hiyo RAIS Samia Suluhu Hassan amesema amejiridhisha
kuwa chanjo ya virusi vya corona ni salama na kwamba kama isingekuwa
hivyo asingekubali kuwaongoza Watanzania kuchanjwa.
Alisema
yeye ni mama wa watoto wanne, mke, bibi wa wajukuu kadhaa, Rais na
Amiri Jeshi Mkuu, ana makujumu na kuna watu wanamtegemea hivyo
asingeweza kufanya jambo la kuhatarisha maisha yake.
“Kama
chanjo sio salama nisingekubali kuchanjwa, nimekubali kuchanjwa kwa
sababu ni salama,” alisema Rais Samia katika Ikulu ya Magogoni Dar es
Salaam jana muda mfupi kabla ya kuongoza viongozi kupata chanjo ya
corona aina ya Johnson & Johnson iliyoletwa nchini Julai 24, mwaka
huu kutoka nchini Marekani.
Alisema
chanjo zilizopo nchini ni kidogo ukilinganisha na idadi ya Watanzania
wanaohitaji kuchanjwa kwa hiyari hivyo serikali itahakikisha
zinapatikana chanjo za kutosha.
“Wapo
wanaozikataa na wapo wanaozikubali, nawaambia chanjo ni salama kama sio
salama nisingekubali kuchanjwa, ninachanjwa baada ya kujiridhisha
usalama wake,” alisema Rais Samia.
Aliongeza
“Hao wanaozikataa huenda familia zao au koo zao haziathiriwa na janga
hili. Ila nendeni Moshi, Arusha na Dar es Salaam kwenye zile koo au
familia zilizopoteza wapendwa wao watawaambia na kama wangepewa fursa
hii ya kuchanja leo (jana), wangekuja hapa kuchanja,”
Alisema
Tanzania si kisiwa ina watu na wengine ni raia wa kimataifa hivyo
muingiliano uko duniani kote na lazima tahadhari dhidi ya corona na
magonjwa mengine ichukuliwe
Mbali
na Rais Samia viongozi wengine waliopata chanjo hiyo ni pamoja na
Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam,Yuda Thadeus
Ruwa'ichi, Mufti wa Tanzania ,Abubakar Zubeir, Mkuu wa Jeshi la Wananchi
Tanzania(CDF) Venance Mabeyo, Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia
Wazee na Watoto Dk Dorothy Gwajima na wengine wengi wakiwemo waandishi
wa habari.
Aidha
akisisitiza hilo, Mwenyekiti huyo wa UWT Mkoa wa Njombe Scolastika
Kevela aliwataka watanzania kuachana na kauli za upotoshaji kutoka kwa
baadhi ya watu kuhusiana na chanjo hiyo akidai kuwa hawana nia njema
na afya pamoja na maisha ya watanzania huku akisisitiza kuwa ugonjwa wa
Corona upo na unaua na kwamba njia pekee ya kukabiliana nao ni kupata
chanjo hiyo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...