Yabainisha matokeo ya sensa yatasaidia katika kufikia uchumi wa bluu na kuimarisha usalama wa vyombo hivyo.
Na Chalila Kibuda,Michuzi Tv, Bagamoyo
SHIRIKA la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) kuanza kufanya sensa ya vyombo vidogo vya usafiri majini kwenye maziwa, mito pamoja na bahari ili kujenga kanzidata ya vyombo vidogo vya usafiri na hivyo kuwezesha kupanga mipango ya maendeleo na kuimarisha usalama katika sekta hiyo.
Sensa hiyo itashirikisha Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) pamoja na Wizara ya Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) ambapo sensa hiyo itaanza Oktoba Mosi hadi Oktoba 30 mwaka huu.
Akizungumza wakati wa semina ya siku mbili yenye lengo la kuwajengea uwezo maafisa uvuvi na maafisa wa TASAC, Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa TASAC ambaye ni Mkurugenzi Udhibiti Uchumi wa Shirika hilo Nahson Sigalla amesema sensa hiyo ya nchi nzima pamoja na mambo mengine imelenga kuinua maendeleo ya sekta hiyo kusaidia katika utungaji sera na udhibiti.
Amesema sensa hiyo pia itasaidia kuimarisha usalama kwa kulinda uhai na mali za watumiaji na wamiliki wa vyombo hivyo nchini kote.
Sigalla amesema sensa ya vyombo hivyo itakayofanywa katika maeneo ya bahari, maziwa na mito itasaidia kutambua idadi ya vyombo hivyo na majukumu yake na baadae taarifa zake kuwekwa katika kanzidata maalumu.
"Tanzania inatekeleza uchumi wa bluu unaohusisha masuala yote ya uchumi wa bahari, kanzidata tunayoijenga kupitia sensa hii itatuwezesha kubaini hatua za kuchukua kufanikisha maendeleo na kutatua changamoto zinazokabili sekta hiyo" amesema Sigalla.
Aidha, amesema kwa kuzingatia utaratibu uliopo, sensa hiyo itavishirikisha vyombo vidogo vyenye urefu usiozidi urefu wa mita 24 au uwezo wa kubeba mizigo isiyozidi tani 50 katika maeneo yote ya ukanda wa bahari, maziwa na mito ambako huduma ya usafiri huo hutolewa.
Amesema pamoja na kusaidia kupanga mipango ya kimaendeleo, sensa ya vyombo hivyo pia itawasaidia wataalamu wa vyuo vya elimu ya juu kufanya tafiti mbalimbali ikiwemo namna vyombo hivyo vinavyosaidia katika ukuaji wa maendeleo nchini na dhamira ya Serikali ya kukuza uchumi wa bluu.
Sigalla alisema dhima nyingine ya sensa hiyo imetokana na mahitaji ya upatikanaji wa taarifa kwa ajili ya kusaidia ukuaji wa maendeleo ya sekta hiyo muhimu kwa uchumi.
Mmoja wa walengwa wa mafunzo hayo ambaye pia ni Afisa Uvuvi kutoka Mkoa wa Kagera Maengo Nchimani amesema matarajio mafunzo hayo yatawasaidia kufanikisha malengo yaliyokusudiwa huku akiamini ujio wake ni muhimu katika kuharakisha maendeleo ya taifa.
Nchimani amesema kumekuwepo na vyombo vingi vinavyotoa huduma ya usafiri na ubebaji wa mizigo katika mito, maziwa na bahari huku akiwataka wamiliki wa vyombo hivyo kutoa ushirikiano wa dhati sensa itakapoanza.
Mshiriki wa Mafunzo Afisa Uvuvi Maengo Nchimani akizungumza kuhusiana na mafunzo hayo namna watavyochukua sensa hiyo kwa kwa kisasa
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...